Pengo ataka Taifa liombewe amani


Claudia Kayombo

Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo
ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, ametaka Watanzania kuendelea kuliombea Taifa amani na utulivu.

Alitoa kauli hiyo jana Dar es Salaam kwa waumini wa Kanisa hilo, waliofurika katika ibada ya kumbukumbu ya Wafia Dini katika Kituo cha Hija Pugu.

“Tunapofanya ibada hii tulioombee Taifa letu, ili tuendelee kuishi kwa amani na utulivu,” alisisitiza Kadinali Pengo.

Alisema amefurahi kushiriki ibada hiyo katika eneo hilo la kwanza kuhubiriwa imani Katoliki katika Jimbo Kuu la Dar es Salaam mwaka 1888 walipoingia Wamisionari kutoka Ujerumani.

Mahali hapo ndipo wafikia wafia dini watatu; Mtawa Martha na mabruda Petrus na Benedikti waliouawa na wafuasi wa Bushiri aliyekuwa kiongozi wa Wakoloni Waarabu Afrika Mashariki wakati huo.

Kadinali Pengo alisema eneo hilo ni takatifu kwa sababu ndilo chimbuko la Kanisa hilo nchini, ambapo Wafia Dini hao kutoka Ujerumani wa Shirika la Mtakatifu Otilien, walifika kwa moyo mkunjufu kuhubiri Ukristo.

“Nawashukuru kila mmoja wenu aliyefika hapa Pugu kushiriki ibada hii. Tulianza ibada yetu kama mbegu ndogo ya haladali lakini sasa tupo wengi, Mungu ndiye aliyetukusanya,” alibainisha.

Aliwataka waamini wa Kanisa hilo, kujitoa katika mambo mbalimbali wakiiga yaliyofanywa na Wamisionari hao waliojitoa kueneza dini hiyo bila kujali changamoto walizokuwa wakikutana nazo.

Wakati huo huo, Kadinali Pengo aliwaomba msamaha waamini wa Parokia tarajiwa ya Msewe kwa kuwa hakuitaja miongoni mwa nyingine alizozitaja Januari 6.

Alisisitiza kuwa hakufanya hivyo kwa makusudi na aliitaja Parokia nyingine tarajiwa ya Baruti.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu hilo, Eusebius Nzigilwa aliyeongoza ibada hiyo, alisema wakati Kanisa hilo likifanya kumbukumbu hizo, Taifa lilifanya sherehe ya Mapinduzi ya Zanzibar, hivyo aliwaomba waamini waitumie fursa hiyo kuliombea Taifa amani na upendo.

Alisema wafia dini hao waliitika sauti ya Mungu, hivyo Watanzania wawe tayari kujitoa kutekeleza majukumu ya jamii bila kulazimishwa.

Abate Platidius Mtunguja wa Abasia ya Ndanda alisema Wamisionari hao wa Ujerumani walifika eneo hilo kwanza kabla ya Mt. Joseph mwaka huo.

Alibainisha kuwa wakiwa hapo walisimika mahema waliyotumia kusali na kuishi, mazingira ambayo yalikuwa magumu kwao, lakini walivumilia.

Alibainisha kuwa Januari 13, 1889, siku ya sherehe ya toleo la Bwana, Wamisionari hao watatu waliuawa na yatima saba waliokuwa wakiwalea.

Alisema kulingana na ushuhuda uliotolewa na miongoni mwa Wamisionari waliofanikiwa kutoroka, ulikuwa wakati ambao walikuwa wakisali.

Alifafanua, kuwa Bruda Petrus ndiye alikuwa wa kwanza kuuawa kwa kupigwa risasi kisha Bruda Benedikti aliyeuawa karibu na Tabernakulo wakati akijaribu kumeza Ekaristi Takatifu, wakati Mtawa Martha aliuawa na mtoto aliyekombolewa utumwani.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo