Lowassa amuomba JPM atafakari misimamo yake



Mwandishi Wetu, Misenyi
Edward Lowassa
WAZIRI Mkuu wa zamani na Mjumbe wa Kamati ya Kuu ya Chadema, Edward Lowassa, amemtaka Rais John Magufuli, kutafakari hoja na ukosoaji wa wananchi na wapinzani dhidi yake.

Akizungumza katika Mkutano Mkuu Maalum wa Chadema wilayani Misenyi mkoani Kagera uliyofanyika jana katika eneo la Bunazi, Lowassa alimtaka Rais Magufuli kutozipuuza hoja zinazotolewa kuhusu masuala mbalimbali ya nchi.

“Tunamuomba Rais atafakari kwa ungwana hoja za watu wengine. Tunamuheshimu ni Rais, lakini tunamuomba atafakari hoja hizi watu wasiendelee kuumia sana,’’ alisema Lowassa.

Kuhusu na hali ya ukame nchini, Lowassa alisema kuwa hali ya chakula nchini hivi sasa ni mbaya.

"Eneo moja ambalo hakika Rais anatakiwa kusikia hoja za watu wengine ni suala la njaa. Nimeshuhudia mwenyewe pale Longido na maeneo mengine. Hali ya mvua ni mbaya, hali ya chakula ni mbaya, watu wako hoi bin taaban halafu wanaambiwa hakuna kuwapelekea chakula,” alionesha mshangao Lowassa.

Akizungumzia madhila na waathirika wa tetemeko la ardhi mkoani Kagera, Lowassa alielezea kushangazwa kwake na hatua ya Rais kuamua kutopeleka misaada kwa waathirika hao akisema hata Mungu anashangaa.

"Mimi nakaa nasema mfano kama ni mama yako pale kijijini, halafu amekumbwa na janga hili, anaambiwa ajisaidie mwenyewe si atakushangaa hata Mungu atashangaa,’’ alisema kwa masikitiko.

Kwa upande wake Mbunge wa Bukoba Mjini, Wilfred Lwakatare (Chadema), alisema hali ya chakula katika mkoa wa Kagera ni mbaya.

Lowassa akiambatana na wajumbe wengine wa Kamati Kuu ya Chadema, akiwemo Profesa Mwesiga Baregu, ameendelea na ziara katikia mkoa wa Kagera ya kuimarisha chama chao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo