JPM mbioni kufungia magazeti mawili


Charles James na Celina Mathew

Rais John Magufuli
RAIS John Magufuli amekemea vyombo vya habari vinavyoandika uchochezi hasa magazeti aliyotaja kuwa yako mawili, huku akisisitiza kuwa siku zao zinahesabika.

Kauli hiyo aliitoa mjini Shinyanga jana wakati akizindua kiwanda cha chakula cha Jambo Food Product, kinachomilikiwa na Mbunge wa Meatu, Salum Mbuzi, ambapo alisema kwa kiasi kikubwa magazeti hayo yamekuwa yakigeuza habari na kuandika uchochezi jambo   linalohatarisha amani ya nchi.

“Serikali ya kutumbua majipu haiwezi kuacha kutumbua magazeti yanayofanya mambo ya uchochezi, hatuwezi kuiacha Tanzania ikawa dampo la eneo la kuweka maneno ya uchochezi, chini ya utawala wangu hilo halitakuwepo.

“Kuna magazeti mawili tu kila ukisoma wao ni kuchochea tu ikizungumzwa habari hii, wao wanageuza hii, nasema nataka wanisikie siku zao zimeshafika kama wanasikia wasikie wasiposikia wasisikie lakini magazeti mengine na vyombo vyote vingine vinatoa uchambuzi mzuri sana,” alisema.

Akitolea mfano namna vyombo vya habari vilivyohatarisha amani ya nchi, Rais Magufuli alisema mauaji ya Rwanda kwa kiasi kikubwa yalichochewa na wanahabari waliosababisha vifo vya mamilioni ya watu.

"Kuna nchi jirani (ambayo hakuitaja), watu walikufa kutokana na hao hao wanahabari waliokuwa wanaandika habari za kichochezi, naomba watambue kuwa hapa nchini sitakuwa tayari kuona amani inachezewa," alisisitiza.

Alisema kwenye utawala wake hatakubali kuifanya Tanzania kuwa nchi isiyo na amani kwa ajili ya vyombo vichache vya habari vinavyotumiwa na wanasiasa kuvuruga amani.

"Kwenye utawala wangu sitakubali kuona nchi inapoteza amani yake kwa ajili ya vyombo vichache vinavyotumiwa na wanasiasa, kwa kuwa hata Wakiristo kwenye maandiko kuna maneno wanayosema kuwa amani nawaachieni hivyo tutambue kuwa amani hainunuliwi, tuilinde," alisema.

Rais Magufuli alitaka vyombo vilivyobaki kutoandika habari za kichochezi kwa kuwa vinafanya kazi kwa weledi wa hali ya juu, viendelee hivyo hivyo.

Kuhusu kiwandi hicho kinachotengeneza bidhaa mbalimbali za vyakula na vinywaji, Rais Magufuli alimpongeza Mbunge huyo kwa kumsifu kuwa amemuanzishia mwaka vizuri.

Rais Magufuli alisisitiza kuhusu azma yake ya kuwa na Tanzania ya viwanda ikiwa na lengo la kuimarisha uchumi na kutoa ajira kwa idadi kubwa ya wananchi.

Alimsifu Mbuzi kwa uzalendo aliouonesha wa kuanzisha kiwanda katika ardhi ya nyumbani kwake, ambapo licha ya kukuza pato la Taifa lakini pia ametoa idadi kubwa ya ajira kwa Watanzania wenzake, huku akitoa wito kwa wawekezaji wengine kuchukua mfano wa mbunge huyo.

“Nakaukiwa maneno ya kuongea kutokana na hiki nilichokiona hapa, nimepita kukagua na kujionea ubora wa kiwanda pamoja na kushuhudia uzalishaji wa kisasa ambao ni nadra sana kuonekana katika nchi za Kiafrika, hakika Mbuzi ninakusifu na ninaahidi kukupa ushirikiano wa dhati.

“Nikiwa na watu kama ninyi naamini lengo la Tanzania ya viwanda niliyoihubiri katika kampeni zangu litatimia, tayari kule Pwani viwanda 48 vimeshaanzishwa na jana nimefungua kiwanda kingine cha utengenezaji wa chaki kule Meatu, hii ni kuonesha jinsi gani kazi inafanyika,” alisema Rais Magufuli.

Aliwapongeza viongozi wa mkoa kwa namna ambavyo wamekuwa wakipambana kuhakikisha wanajenga Shinyanga ya viwanda na kuwataka kuharakisha kufufua kiwanda cha nyama, ambacho mwekezaji wake ameshindwa kukiendesha kwa muda mrefu bila kuwa na sababu ya msingi.

“Tunahitaji wawekezaji wazalendo kama Mbuzi, siyo wale wengine ambao fedha zao wanaenda kuzificha nje ya nchi na wakifa zinapotelea huko huko, nikusifu wewe kwa kutoa ajira kwa Watanzania wenzako lakini kama haitoshi hata bei ya vinywaji vyako naambiwa ni rahisi,” alisema.

Alimtaka Mbuzi kuhakikisha anajali maslahi ya wafanyakazi wake kwa kuwalipa mishahara mizuri huku akimtoa wasiwasi kuwa yale yote yanayohihusu Serikali amuachie na hata suala la kodi anaweza kuangalia jinsi gani ya kumpunguzia.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo