Asali yasababisha mototo ‘kuua’ babaye


Frankius Cleophace, Mara

JESHI la Polisi linamsaka mkazi wa kijiji cha Kitenga wilayani hapa, Bakari Bakari (32) kwa tuhuma za kumpiga baba yake mzazi kichwani kwa kitu chenye ncha kali na kumsababishia kifo.

Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Tarime/Rorya, Andrew Satta alithibitisha jana kutokea kwa tukio hilo na kumtaja aliyeuawa kuwa ni Shaban Ramadhan (56), aliyemfumania kijana wake akiiba asali kwenye ghala.

Satta alisema tukio hilo lilitokea Kitenga Januari 11 saa 4 usiku wakati Shaban ambaye ni mfanyabiashara wa asali, akifungua mlango wa ghala lake kwa lengo la kuhifadhi asali.

Alisema wakati akiingia, mwanawe huyo aliyekuwa ndani ya chumba hicho akiiba asali, alimvamia baba yake na kumpiga kichwani kwa kitu chenye ncha kali na kumsababishia kifo papo hapo.

Mhudumu wa mochari ya Hospitali ya wilaya, Samwel Marindi alisema siku hiyo saa 4 usiku alipigiwa simu na polisi wakimtaka afike eneo lake la kazi kupokea mwili wa marehemu, ambao umehifadhiwa kwenye chumba hicho.

Shuhuda wa tukio hilo, Alex Chacha alisema walisikia mayowe wakatoka nyumbani kwenda kusaidia, lakini wakakuta mwili wa marehemu kwenye chumba alimokuwa akihifadhi asali na kupiga simu Kituo cha Polisi cha Sirari.

“Polisi walikuja wakafanya uchunguzi na kuchukua mwili kuupeleka Bomani ulikohifadhiwa,” alisema Chacha.

Chacha ambaye ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Buriba, kata ya Sirari alisema Shaban alikuwa akikusanya asali na kuisambaza kwa wanunuzi wilayani hapa na nje ya Tarime.

“Hatujajua kwa nini aliamua kumshambulia baba yake hadi kumsababishia mauti, kwangu hii ni familia rafiki na ni msiba mkubwa,” alisema Chacha.

Desemba 29 mwaka jana, Robert Mwikwabe alimpiga risasi usoni Maite Amilly (17) mwanafunzi wa kidato cha tatu wa sekondari ya Sirari na kumuua papo hapo wakigombea pumba za mchele.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo