Lissu adai kifungo cha Mbunge ni vita


Fidelis Butahe

Tundu Lissu
WAKATI Mbunge wa Kilombelo, Peter Lijualikali (Chadema), akiwa na siku mbili jela baada ya kuhukumiwa kifungo cha miezi sita juzi, Mwanasheria Mkuu wa Chama hicho, Tundu Lissu ameeleza kuwa hukumu hiyo inatokana na vita vya kisiasa kati ya Chadema na CCM.

Akizungumza na waandishi wa habari jana kwenye ofisi za makao makuu ya chama hicho Dar es Salaam, Lissu alisema Mbunge huyo alianza kusakamwa siku nyingi, ikiwa ni pamoja na kufunguliwa kesi, ikiwamo ya kupinga ushindi wake wa ubunge.

Alisema licha ya ‘vita’ hivyo, timu ya wanasheria wa Chadema imeanza mchakato wa kuandaa notisi ya rufaa na maombi ya dhamana ya dharura wakati uamuzi juu ya rufaa yake ukisubiriwa, kwamba taratibu zote zitakamilika Jumatatu.

“Lijualikali na Lema (Godbless-Arusha Mjini) ambaye yuko rumande kutokana na kunyimwa dhamana akituhumiwa kutoa lugha ya uchochezi, wote hawa ni wafungwa wa kisiasa,” alisema Lissu.

Juzi, Mahakama ya Wilaya ya Kilombero alimhukumu Lijualikali kifungo cha miezi sita jela kwa kufanya vurugu na kusababisha taharuki kwenye mkutano wa uchaguzi wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji mdogo wa Ifakara.

Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Timothy Lyon alisema kutokana na Lijualikali kuwa na kesi tatu siku za nyuma na kutiwa hatiani, Mahakama iliona ana hatia ya kutumikia kifungo hicho huku ikimhukumu kifungo cha nje mtuhumiwa wa pili, Stephano Mgata ambaye ni dereva wa Mbunge huyo.

Katika ufafanuzi wake jana, Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, alidai kuwa kesi iliyofunguliwa dhidi ya Mbunge huyo ilikuwa ya kisiasa, ili kutekeleza malengo  ya CCM dhidi ya Chadema.

“Adhabu ya kifungo bila faini imetolewa kwa sababu za kisiasa. Kwanza walimshitaki mara mbili; wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu ili wamfunge na asiweze kuendelea na kampeni. Haikuwezekana kumfunga na alishinda ubunge,” alisema.

“Baadaye walimfungulia kesi ya uchaguzi Mahakama Kuu ambako nako tuliwashinda vibaya. Wamekata rufaa Mahakama ya Rufani ya Tanzania nako tutawashinda na wanajua hivyo,” aliongeza.

Alisema waliamua kumfunga Mbunge huyo bila faini wakiamini kuwa uamuzi huo utamfanya akose sifa za kuwa Mbunge.

Huku akinukuu Ibara ya 67 (2) (c) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Lissu alisema adhabu hiyo haina athari yoyote, kwa maelezo kuwa mtu anakosa sifa za kuwa Mbunge iwapo atafungwa gerezani zaidi ya miezi sita.

“Si kifungo tu cha miezi sita, pia lazima awe amekutwa na hatia ya kosa lolote, vyovyote linavyoitwa, linaloambatana na utovu wa uaminifu,” alisema.

“Adhabu ya kifungo aliyopewa Lijualikali haijazidi miezi sita. Pia kosa la kumpiga askari Polisi, hata kama lingekuwa la kweli, si la utovu wa uaminifu.”
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo