Rais Magufuli chondechonde njaa kali—Profesa Lipumba


Mwandishi Wetu

Profesa Ibrahimu Lipumba
KILIO cha hali ngumu ya maisha tangu kuanza kwa utawala wa Serikali ya Awamu ya Tano, kimemgusa mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa nchini, Profesa Ibrahim Lipumba.

Profesa Lipumba ametoa wito maalumu kwa Rais John Magufuli kusikiliza kilio hicho cha wananchi kwa kulegeza kamba ya kubana matumizi na kuwaandalia wananchi mazingira mazuri ya kumudu maisha yao.

Profesa Lipumba alitoa wito huo juzi katika mkutano wa hadhara wa kumnadi mgombea Udiwani wa Kata ya Kijichi iliyoko Temeke jijini Dar es Salaam kupitia chama hicho, Khalid Shamas.

Lipumba ambaye ni profesa aliyebobea katika taaluma ya uchumi, alisema sera ya kubana matumizi haina ubaya, lakini jambo hilo, lazima liendane na mpango wa kuwasaidia wananchi katika kujipatia riziki zao.

“Watu wanapigika na wengine wanalazimika kufunga bila kunuia, halafu tunajigamba tumefanikiwa kukusanya fedha nyingi kwa kubana matumizi. Hiyo inatusaidia nini wapiga kura wako, mheshimiwa rais?” alihoji Profesa Lipumba.

Profesa Lipumba ambaye aliwahi kuwa mshauri wa mambo ya uchumi katika Serikali ya Awamu ya Pili na mtaalamu aliyewahi kutumiwa na mataifa mengi, ikiwamo Uganda kushauri masuala ya uchumi, alisema uchumi unaokua bila kuonekana mifukoni mwa watu hauna tija.

“Hizo sera (za kubana matumizi) zinaweza kuwa nzuri sana, lakini umesahaulika mpango wa kuona ni kwa namna gani wananchi wanasaidiwa kumudu maisha yao. Leo vijana wanapigika na hakuna msaada.”

Profesa Lipumba aliishauri Serikali kuwatengenezea wananchi mazingira mazuri ili waweze kuboresha maisha yao na kujenga mazingira ya kutafsiri ukuaji huo wa uchumi katika maisha ya wananachi wa kawaida.

Hata hivyo, kauli hiyo ya Profesa Lipumba imekuja ikiwa tayari Rais Magufuli ameeleza kuwa mpango huo wa kukata mirija ya upatikanaji fedha kiholela, umelenga kuwafanya watu wafanye kazi.

Rais Magufuli ambaye Serikali yake inaongozwa kwa kauli mbiu ya ‘hapa kazi tu’ alisema anataka kila Mtanzania ale kwa kipato chake halali. Akaamua kusitisha vikao na semina za taasisi za Serikali mahotelini na kupunguza safari za nje za mawaziri, huku akiboresha ukusanyaji kodi kama moja ya hatua ya kutaka taifa lijitegemee.

Amnadi mgombea wake

Profesa Lipumba aliwaomba wakazi wa Kijichi kumchagua Khalid Shamas kuwa diwani wa kata hiyo katika uchaguzi mdogo uliopangwa kufanyika Januari 22, ili apeleke kilio cha ugumu wa maisha katika vikao vya halmashauri.

“Siyo rahisi CCM kusema ukweli kuhusu jambo hilo. Hapa tunahitaji mtu mwenye misimamo tofauti kidogo. Mchagueni Shamas akawakumbushe CCM kwamba pamoja na mipango yake, watu wanapigika… Hakiii...”

Akizungumza katika mkutano huo, Shamas aliomba achaguliwe akieleza kuwa amekuja na mipango mbadala ya kuwaletea wakazi wa Kijichi maendeleo endelevu.

“Wagombea wote hakuna aliyefika hapa na kablasha la kazi. Mimi ninalo, hili hapa,” alisema Shamas akionyesha karatasi aliyoishika mkononi.

Aliendelea “Humo kuna mambo mengi. Mkinichagua nitaanza na elimu. Nitahakikisha nasimamia sera ya CCM ya elimu bure itoe elimu bora na siyo bora elimu. Nitasimamia ujenzi wa maabara katika shule zote za Sekondari, ujenga soko katika kila mtaa, mabweni kwa wanafunzi wa kike na umeme mashuleni.

Uchaguzi mdogo wa Kijichi unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wa kata hiyo kupitia CCM, marehemu Underson Charles.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo