JPM asisitiza hakuna njaa nchini


Mwandishi Wetu

RAIS John Magufuli amesema taarifa zinazoenezwa kuhusu nchi kukumbwa na njaa si za kweli na kuwataka Watanzania kufanya kazi kwa bidii ili kujipatia chakula.

Akihutubia wananchi wa Bariadi jana alikokwenda kuwashukuru na kuzindua ujenzi wa barabara na hospitali ya mkoa wa Simiyu, Rais alituhumu baadhi ya wafanyabiashara walioingiza mahindi nchini na kutafuta njia ya kuyauza.

“Kuna wanasiasa na baadhi ya waandishi wa habari wanaotumika na wafanyabiashara walioingiza mahindi kwa njia zao na sasa wanatumia kisingizio cha njaa ili kuuza mahindi hayo,” alisema Rais.

Alisisitiza kulima mazao yanayostahimili ukame na wenye uwezo wa kumwagilia wafanye hivyo ili kuondokana na njaa kama itatokea mvua zisinyeshe.

“Inashangaza mtu kulima mahindi ambayo yanahitaji maji mengi na kuacha kulima mtama ambao hauhitaji maji mengi, mtu analima mahindi kandoni mwa ziwa, lakini anashindwa hata kuchukua ndoo kuchota maji na kumwagilia,” alisema Rais.

Akisisitiza taarifa za madai ya njaa, rais alitolea mfano wa ng’ombe 17,000 kufa kwa njaa wilayani Mvomero, mkoani Morogoro, akisema hiyo ni taarifa ya kutunga.

“Haiwezekani unaona ng’ombe mmoja anakufa, wa pili, 100… ng’ombe elfu…wanakufa unaangalia tu kwa nini usiwauze ukanunua chakula, ukanunua mahindi? Hii haiingii akilini,” alisema Rais Magufuli na kusisitiza kutokuwapo njaa nchini.

Hata hivyo, alirudia kauli yake kwamba serikali haina shamba hivyo watakaokumbwa na njaa kutokana na kutolima, wasitarajie Serikali iwapelekee chakula na badala yake wafanye kazi ya kujizalishia chakula.

“Hata Baba Askofu yuko hapa, anajua kwamba maandiko yanasema asiyefanya kazi na asile … usipofanya kazi ukakosa chakula basi ufe tu,” alisema Rais na kuwataka watanzania kujiandaa kusikia na kuukubali ukweli.

“Kama mlizoea kusikia mazuri tu na sasa mjiandae pia kusikia mabaya, mimi nitasema ukweli daima, siwezi kuita jiwe mchanga uliojikusanya,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo