Wahimizwa kunywa kahawa kila mara


Joyce Anael, Same

WATUMISHI wa umma ofisini na wananchi kwa ujumla wameshauriwa kuanza utaratibu wa kunywa kawaha ili kukuza uchumi wa mkulima na pato la Taifa.

Mbali na kukuza uchumi, pia unywaji wa kahawa unaburudisha mwili na kupunguza uwezekano wa magonjwa ya saratani ya ngozi na ini.

Majid Kabyemela ambaye ni Ofisa Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika wa Wilaya ya Same, alisema hayo jana kwenye maadhimisho ya Siku ya Unywaji Kahawa wilayani humo na kuongeza kuwa faida ya unywaji kahawa ni pamoja na kuchangamsha mwili pia kusaidia kufikiria kwa haraka na kupunguza kisukari.

Alisema wananchi wanaokunywa kahawa wanapata faida nyingi ikiwa ni pamoja na kuzuia ugonjwa wa kutetemeka, gauti, magonjwa ya moyo kwa wazee na kupunguza mafuta mwilini kwa wenye uzito mkubwa, hivyo kuna haja ya wananchi kujijengea utamaduni wa kunywa kahawa.

Kabyemela alisema kahawa ni moja ya mazao ya biashara nchini na huliingizia Taifa kiasi cha fedha za
kigeni ambapo mwaka 2014/15 zao hilo, liliingizia Taifa dola 135,768,630 za Marekani huku msimu wa mwaka 2015/16 hadi Aprili Taifa lilipata   dola 132,319,519.

Alisema kahawa humwingizia mkulima kiasi cha Sh 2,310,300 kwa ekari moja kwa mwaka kwa mkulima anayetunza shamba vizuri kwa kufuata kanuni nane za kilimo cha kahawa na amri 10 za usindikaji kahawa ili kupata daraja la juu ambalo lina bei nzuri.

Ofisa huyo alitaja sababu zinazochangia kushuka kwa uzalishaji wa zao hilo, kuwa ni pamoja na bei ndogo ya zao hilo inayowakatisha tamaa, baadhi ya wakulima wanaotaka kujiingiza kwenye kilimo cha kahawa, upatikanaji wa pembejeo kwa wakulima wenye uwezo mdogo na mabadiliko ya tabianchi yanayosababisha uhaba wa mvua na hivyo kuathiri uzalishaji.

Alitaja sababu zingine za kushuka kwa uzalishaji wa kahawa ni pamoja na wakulima kukimbilia mazao ya biashara ya haraka yenye faida kubwa kama tangawizi  na kuacha kulima kahawa, uwezo mdogo wa wakulima kununua miche ya kahawa na kubadili mibuni mikongwe na wadudu waharibifu.

Wilaya ya Same ina wakulima 1,722 huku hekta zinazolimwa kahawa zikiwa ni 1,600 ambapo mwaka 2015/16 jumla ya tani 320 zililimwa na kuwaingizia kipato wakulima na  pato la Taifa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo