Mbunge CCM ahoji utajiri wa Makonda


Fidelis Butahe, Dodoma

MBUNGE wa Geita Vijijini (CCM), Joseph Msukuma, ametaka Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda achunguzwe kwa maelezo kuwa amepata utajiri ndani ya muda mfupi, ikiwa ni pamoja na kujenga nyumba kadhaa na kumiliki magari ya kifahari.

Msukuma ambaye juzi alihoji vita dhidi ya biashara ya dawa za kulevya iliyoanzishwa na Mkuu huyo wa Mkoa, akimtaka aanze kukamata aliowapangisha nyumba za kuishi wanaotajwa kujihusisha na biashara hiyo, akihoji sababu za mawaziri kushikwa kigugumizi kuzungumzia vita hivyo.

Akizungumza bungeni juzi baada ya kuomba Mwongozo wa Spika, Msukuma alisema dalili za kumhisi mtu anayejishughulisha na biashara hiyo ni mwenendo wake bila kujali wadhifa wake.

“Mwaka juzi Makonda alikuwa akiishi kwa Membe (Bernard- aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje). Amekuwa Mkuu wa Mkoa ndani ya mwaka mmoja, lakini anatumia gari la Lexus la Sh milioni 400 tena linalotumia mafuta ya petroli,” alisema Msukuma.

“Kama hiyo haitoshi, ofisi yake ya Dar es Salaam imekarabatiwa kwa zaidi ya Sh milioni 400 bila kufuata utaratibu wa ununuzi wa umma, ana magari Toyota V 8, amejenga maghorofa kwa mwaka mmoja, hivi ni akina nani hasa wanaotakiwa kujadiliwa na kufanyiwa uchunguzi?” Aliendelea kuhoji.

Alisema wakati hayo yakiendelea, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utawala Bora, Waziri wa Katiba na Sheria na wa Mambo ya Ndani ya Nchi wamepigwa ganzi.

“Mnalifanya suala hili ni la Rais kuhangaika na Mkuu wa Mkoa. Hata kama anachangiwa na wahisani, sheria ya maadili inatutaka anayetuchangia tumtangaze, lini amewatangaza wanaomchangia fedha?” Alihoji.

“Naomba Mwongozo wako Naibu Spika, kama wengine wanaweza kufanya mambo ya hovyo na wakawa na kinga na mawaziri wakapigwa ganzi, hawawezi kufuatilia, utuelekeze tunataka Makonda achunguzwe mali alizonazo,” alisema.

Alisema haiwezekani ndani ya mwaka mmoja Mkuu wa Mkoa amudu kununua magari ya bei kubwa sambamba na kutembelea nchi mbalimbali Ulaya na Marekani.

“Wala si suala la kuogopa, niko tayari kuwasaidia mawaziri na vyombo vya usalama tuwaoneshe, tukitaka kumaliza wauza dawa tuanze na mizizi, tusishike matawi,” alisema.

Hata hivyo, Naibu Spika Dk Tulia Ackson alipangua Mwongozo wa Mbunge huyo kwa maelezo kuwa alizungumza jambo ambalo ni kinyume na kanuni za chombo hicho cha kutunga sheria.

“Umetoa maelezo mengi siwezi kuyarejea hapa, maana nitakuwa kama natoa msisitizo jambo ambalo kanuni zetu zinakataza kwa maana mambo aliyoyataja, yule mtu aliyemtaja na wengine waliohusika, kama jambo alilolisema si sahihi wanaweza kuja bungeni,” alisema Dk Tulia.

“Kama msimamizi wa leo kanuni ya 68 (7) zinataka niombwe Mwongozo kwa mambo yaliyotokea bungeni mapema, kwa kuwa lilitokea jana (juzi) tumia kanuni nyingine kuleta hoja yako.”

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo