Kigwangalla aingia mzima mzima vita dawa za kulevya


Mwandishi Wetu

Dk Hamis Kigwangalla
NAIBU Waziri wa Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Hamis Kigwangalla, ameagiza hospitali zote za kanda, zianzishe vituo vya kutoa matibabu kwa waathirika na dawa za kulevya ndani ya miezi sita kuanzia jana.

Akizungumza katika kituo cha kuwahudumia watu wanaotibiwa ili kuachana na matumizi ya dawa hizo kilichopo Hospitali ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam, Dk Kigwangalla alitoa maagizo mengine manne na kusisitiza kuwa wauza dawa hizo sasa wamebuni mbinu mpya ya kuwarubuni walioacha kutumia.

Operesheni ya kupambana na utumiaji na biashara ya dawa za kulevya nchini iliyoanza takribani wiki tatu zilizopita, imeshika kasi na kusababisha dawa hizo kuwa adimu mitaani, jambo lilosababisha waliokubuhu katika matumizi kupata athari na kusaka matibabu katika vituo hivyo.

“Kituo hiki kinatoa huduma kwa kuwapatia dawa za methadone. Nimefanya ziara hii kwa sababu kuna ongezeko kubwa la wateja siku za hivi karibuni, kutokana na kuongezeka udhibiti.

“Kuna taarifa kwamba wanaouza dawa za kulevya wameathiriwa sana kwa kupoteza mapato ya mabilioni ya fedha kwa uwepo wa vituo hivi, ambavyo kwa sasa vinahudumia wateja 335, wameanza kubuni mbinu za kuwarudisha kwenye matumizi kwa mbinu mbalimbali ikiwemo kudai kuwa methadone haifanyi kazi,” alisema.

Alisema mbali na hospitali za kanda kuwa na vituo hivyo, hospitali zote za mikoa nchini zinapaswa kuanzisha kliniki ya kutoa methadone ndani ya miezi sita.

Pia alimuagiza Katibu Mkuu (Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto), ahakikishe kuna daktari bingwa wa afya ya akili kwenye kila mkoa, ili kuanzisha na kusimamia vituo vya kutoa tiba ya methadone.

“Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Kinondoni aongeze eneo la kliniki na watumishi kwenye kituo hiki,” alisema.

Naibu Waziri huyo alisema Kamishna wa Polisi wa Operesheni Maalum, naye anapaswa kufuatilia wateja wanaotoka kliniki, ili kudhibiti mkakati wa wanaouza dawa za kulevya, wanaolenga kuwarubuni na kuwarudisha kwenye matumizi baadhi ya watu wanaotibiwa, ili kuachana na matumizi hayo.

Dk Kigwangalla pia alitembelea kituo kama hicho kilichopo katika Hospitali ya Temeke.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo