Mbowe mikononi mwa polisi, Lowassa arejea kufuatilia


Fidelis Butahe na Abraham Ntambara

Freeman Mbowe
HATIMAYE Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam jana limefanikiwa kumkamata Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na kumhoji kwa saa kadhaa kabla ya kuondoka naye ikielezwa kuwa amekwenda kupekuliwa nyumbani kwake.

Mbowe amekuwa akisakwa na jeshi hilo kwa takriban siku 10 tangu alipotajwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alipotaja majina ya watu 65 waliodaiwa kujihusisha na dawa za kulevya.

Taarifa kutoka ndani ya jeshi hilo zilizolifikia gazeti hili na kuthibitishwa na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Chama hicho zinaeleza kuwa Mbowe alikamatwa eneo la Kawe jijini humo.

Februari 10 mwaka huu, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro alisema Mbowe anatakiwa kuripoti kituo kikuu cha Polisi na kwamba asipofanya hivyo bila kutoa taarifa yoyote ya hudhuru, atasakwa popote alipo.

Sirro alitoa kauli hiyo saa chache baada ya Mbowe kuzungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma kubainisha kuwa hatakwenda kuripoti katika Kituo Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam hadi atakapopewa wito maalum wa kisheria unaomtaka afike kituoni hapo.

Mbowe ni miongoni watu 65 waliotajwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na kutakiwa kuripoti kituo kikuu cha polisi kwa ajili ya mahojiano kuhusu biashara na autumiaji wa dawa za kulevya.

Utaratibu huo tata wa kutaja majina ilikuwa ni awamu ya pili baada ya ule ya kwanza kuwalenga wasanii zaidi,

Waliotajwa katika awamu hiyo ya pili ni wafanyabiashara wadogo na wakubwa, viongozi wa dini na wamiliki wa hoteli na migahawa, huku Makonda akieleza kuwa wanaweza kuwa na taarifa zitakazosaidia polisi kuwabaini wauzaji wa dawa hizo.

“Alikuwa akitoka nyumbani kwake kuelekea polisi kuitikia wito wao, lakini alipofika eneo la Kawe alimkamata na kumpeleka kituoni,” alisema Makene.

“Mpaka sasa (jana jioni) hatujui amekamatwa kwa kosa lipi na nini ambacho kinaendelea isipokuwa tu katika mahojiano hayo yupo pamoja na wakili.”

Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Zanzibar, Salum Mwalimu naye alisema Mbowe alikamatwa saa tisa alasiri, kubainisha kuwa anahojiwa na kikosi kazi maalumu cha Jeshi la Polisi.

“Mimi nikiambatana na Wakili wa chama, Frederick Kihwelo tumefika kituoni hapa muda mfupi baada ya Mbowe kufika, lakini tumezuiwa kumuona, tukielezwa tutaruhusiwa kufanya hivyo atakapomaliza mahojiano au hatua ya kurekodi mahojiano,” alisema Mwalimu.

Taarifa zaidi zinaeleza kuwa Waziri Mkuu wa zamani na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa amekatisha mapumziko yake kijijini kwake Monduli kufuatilia kukamatwa kwa Mbowe na anatarajiwa kuwasili jijini humo leo.

Gazeti hili lilipomtafuta Sirro kwa njia ya simu, ilipokelewa na msaidizi wake na kubainisha kuwa Kamanda huyo alikuwa katika mkutano.

Habari zaidi zinaeleza kuwa jana saa 11 jioni, ulinzi uliimarishwa katika kituo kikuu hicho cha polisi na baada ya nusu saa Mbowe aliondolewa eneo hilo na polisi kwa kutumia gari namba T 886 BMX aina ya Land Cruiser.

Licha ya polisi kutotoa maelezo yoyote mpaka gazeti hili linakwenda mitamboni, taarifa zaidi zinaeleza kuwa mbunge huyo wa Hai na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni alikuwa akipelekwa nyumbani kwake kupekuliwa.

Siku chache baada ya Mbowe kutajwa katika orodha hiyo, Chadema kilifungua kesi ya kikatiba Mahakama Kuu dhidi ya Makonda kwa kukiuka sheria na taratibu katika kushughulikia watuhumiwa wa biashara ya dawa za kulevya.

Katika mkutano wake na wanahabari mjini Dodoma Mbowe alipinga vikali kujihusisha na biashara hiyo akiwa sambamba na wabunge wa upinzani.

“Nina mambo matatu ya kuzungumza; kwanza, ninakanusha kwa nguvu zote kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya kwa sababu katika maisha yangu, sijawahi kujihusisha na biashara hiyo au hata kutumia dawa za kulevya,” alisema Mbowe katika mkutano huo

“Pili, sisi kama wapinzani, tunakubaliana na mapambano dhidi ya dawa hizo kwa sababu ni hatari katika maisha yetu na tunaona vita hii ilitakiwa ipiganwe miaka mingi iliyopita, lakini kutokana na sababu mbalimbali, haikupiganwa.”

Jambo la tatu, Mbowe alisema Makonda siyo polisi na kwa mujibu wa sheria, hana mamlaka ya kuita mtu polisi ingawa yeye ni kiongozi wa mkoa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo