Wabunge wamsubiri Makonda bungeni


*Spika Ndugai asema kila kitu kiko tayari
*Mbunge amwomba JPM avunje Bunge

Waandishi Wetu

WABUNGE wamemshukia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, juu ya kauli yake ya kutaka wawakilishi hao wa wananchi kupimwa ulevi.

Wawakilishi hao wamebainisha kuwa matamshi tata ya mteule huyo wa Rais yanaashiria yanawafanya wanamvutia pumzi hadi Bunge lijalo ili ajieleze kwao.

Wakati wabunge hao wakieleza hayo, Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema hawezi kumjibu Makonda kwani ni mapema mno na taratibu zinafanyika kumwita bungeni.

Akitoa maoni yake kuhusu Makonda, Mbunge wa Geita Vijijini (CCM), Joseph Msukuma alikwenda mbali zaidi na kubainisha kuwa kama inaonekana wabunge hawatekelezi vyema majukumu yao, Rais John Magufuli avunje Bunge.

Ndugai ambaye ni Mbunge wa Kongwa, pia alibainisha kuwa taratibu za kuhakikisha Makonda na Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Alexander Mnyeti wanahojiwa na Bunge kwa kutoa kauli za kuingilia haki na madaraka ya mhimili huo, zipo katika hatua nzuri.

Makonda alitoa kauli hiyo juzi Dar es Salaam katika hafla maalumu ya kumkabidhi orodha mpya ya watuhumiwa wa biashara ya dawa za kulevya na kumkaribisha Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rodgers Siyanga.

Katika hafla hiyo, Makonda alimkumbusha Ndugai kutekeleza kauli yake ya Mei mwaka jana bungeni, kuhusu kusudio lake la kuanza kuwapima wabunge ili kubaini kama wanatumia ulevi kabla hawajaingia ukumbi wa chombo hicho cha kutunga sheria.

Katika maelezo yake, Msukuma alisema kauli zinazotolewa na Makonda zinalidhalilisha Bunge, akiwamo Waziri Mkuu ambaye ndiye kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni.

“Anavyosema wabunge wapimwe maana yake hata Majaliwa naye anapaswa kupimwa kama anatumia dawa ama la! Ina maana hata Ndugai naye anapaswa kupimwa? Huku ni kulitukana Taifa maana wabunge tumechaguliwa na wananchi,” alisema Msukuma.

“Ina maana sisi (wabunge) tukipimwa kwa kuhisiwa kuwa tunatumia dawa maana yake wananchi wamechagua wabwia ‘unga’. Makonda amedhalilisha Taifa,” alisema.

Mbunge huyo ambaye alimshambulia Makonda katika mkutano wa sita wa Bunge uliomalizika Ijumaa iliyopita, alisema wabunge watapambana kwa kauli hiyo katika Bunge lijalo.

“Rais analihutubia Bunge ina maana na yeye anakuja kuhutubia ‘mateja’…, kama inaonekana Bunge halifanyi kazi yake vizuri basi Rais alivunje kuliko kudhalilisha wabunge,’’ alisema Msukuma.

Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche (Chadema) alisema, “siamini kama Makonda anafanya mambo haya maana anajua majukumu yake kulingana na wadhifa wake. Lazima tujiulize nani yuko nyuma yake, anayemtuma lengo lake nini?”

Alisema haiwezekani kwa Mkuu wa Mkoa kujiamini kulishambulia Bunge, wabunge na kuhoji mamlaka ya chombo hicho cha Dola bila kuwa na watu nyuma.

“Bunge ni chombo kikubwa sana na kina kiongozi wake, kama Makonda anataka kushauri Bunge angeweza kumshauri Spika si kukishambulia chombo hiki hadharani na kuwaaminisha watu kuwa Bunge si lolote si chochote,” alisema Heche.

Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo) alisema Makonda anatakiwa kutekeleza majukumu yake na kuwaacha wabunge kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria na taratibu.

“Mkoa wa Dar es Salaam una changamoto nyingi sana ikiwamo ya elimu baada ya shule sita kati ya 10 zilizofanya vibaya mtihani wa kidato cha nne kutokea mkoani humo. Atatue hizo kwanza si kuingilia mhimili mwingine,” alisema Zitto.

Mbunge wa Viti Maalumu, Susan Lyimo (Chadema) alisema, “Makonda hajui chochote kwa nafasi aliyonayo. Hana mamlaka yoyote ya kumwomba au kumwagiza Spika na kama atafanikiwa hilo ipo siku ataagiza Mahakama
kupima majaji na mahakimu.”

Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa (Chadema) alisema Mkuu wa Mkoa hana weledi katika utendaji wake wa kazi.

“Kuendelea kumjadili ni kupoteza muda, maana kuna mambo mengi ya msingi ya kujadili yanayohusu wananchi. Tukiendelea kumjadili tunampa umaarufu wa bure ni mtu,” alisema.

Kuhusu Makonda kumkumbusha Ndugai juu ya wabunge kupimwa alisema, “hajui mipaka yake ya kazi anaingilia majukumu yasiyomhusu.

“Naunga mkono vita vya dawa za kulevya ila tatizo langu ni kauli za Makonda hasa kuingilia majukumu ya Spika…, kukumbusha kwa namna ile ni kuagiza! Spika hapewi maagizo anatekeleza mambo aliyoyaanzisha.”

Makonda, Mnyeti

Jumatano iliyopita Bunge lilipitisha maazimio manne likiwamo la kuitwa kwa wateule hao wa Rais baada ya kutoa kauli za kuingilia madaraka ya chombo hicho jambo ambalo Ndugai alisema taratibu zinaendelea, taratibu zikikamilika vyombo vya habari vitajulishwa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo