…Makonda ashindwa kutaja orodha mpya


Suleiman Msuya

Paul Makonda
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, jana alishindwa kutaja majina ya vigogo wa dawa za kulevya, badala yake akamkabidhi Kamishna wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rogers Sianga majina 97 akisema ni ya vigogo na ya watoto wa viongozi.

Katika mkutano wake uliojumuisha viongozi wa idara na taasisi za Serikali na viongozi wa dini, Makonda alisema operesheni ya kutafuta wauzaji, wasambazaji na watumiaji inaendelea mkoani humo, huku akibainisha kuwa na orodha ya nyumba, hoteli, klabu za muziki na vijiwe vinavyohusisha na dawa za kulevya.

“Kuna nyumba 200, hoteli 67, klabu za muziki zaidi ya 20, vijiwe 107 na wauza vitumbua wanaojihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya, vyote navifahamu,” alisema Makonda.

Alifafanua kwamba majina aliyokabidhi kwa Kamishna Sianga ni ya watuhumiwa wa tangu Serikali ya Awamu ya Pili na yanahusisha pia wanasiasa, wafanyabiashara na viongozi wenyewe, hivyo ni dhahiri yatatikisa nchi.

Makonda alisema kundi hilo limejenga mizizi kwa muda mrefu na kujiona kuwa ndilo lenye nguvu ya kufanya jambo lolote, hivyo ni jukumu la wananchi wote kushirikiana na Kamishna kuhakikisha kuwa mapambano hayo yanafanikiwa.

Alisema majina hayo ni awamu ya tatu ya harakati anazozisimamia akishirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa na wadau wengine na kuwa anaendelea na mchakato huo kwa awamu saba.

“Kamishna leo sitataja ila nakukabidhi majina ya vigogo wa dawa za kulevya, ambao wamekuwa wakisababisha vijana wetu kuangamia, lakini sisi tunaendelea na mchakato ambapo matarajio yetu ni hadi awamu ya saba tunaamini kuwa tutakuwa tumekamilisha operesheni,” alisema.

Mkuu huyo alisema kampeni hiyo ya dawa za kulevya haitaishia serikalini na kuwa itakwenda hadi katika familia huku akisisitiza wazazi na wenyeviti wa mitaa kuendelea kutoa taarifa.

Makonda alisema hatoonewa mtu katika mchakato huo kwa alichodai kuwa hadi wanamwita kumhoji mtu wamemchunguza vya kutosha.

Alisema sheria ikitumika ipasavyo, itasaidia kuondoa changamoto ambazo zinakabili nchi kukabiliana na hali hiyo, hivyo kuwataka wananchi kushiriki kwa nguvu zote.

Makonda alisema katika mkoa wake na Serikali hii ya awamu ya tano hataki kuona mbwembwe, kwani hazina nafasi.

Alisema wapo wauzaji ambao wanafanya biashara hiyo bila kushiriki moja kwa moja, tofauti na kutumia simu na baada ya kukamilisha kazi wanatupa simu husika na inafikia mahali hutumia majina ya wanawake kusajili simu.

Makonda aliwasha taa nyekundu kwa viongozi wa dini zote kuwa moto utawawakia bila kuacha yeyote anayehusika.

“Hili ni jiwe litahakikisha kuwa linasaga mawe yote ili yawe unga na kumaliza adha hii ambayo inawasibu wananchi wa Dar es Salaam, pia natoa mwito kila mmoja ashiriki kutoa taarifa,” alisema.

Kwa upande mwingine Makonda alisema katika hoteli  hasa za fukweni kuna wateja wa kudumu ambao wanatia shaka.

Alisema pia katika uchunguzi wao wamegundua nyumba nyingi za wanasiasa za Dar es Salaam zinahusika na biashara hiyo na kuahidi kuwa hataachwa mtu.

Mkuu wa Mkoa alisema biashara hiyo inagawanyika katika makundi makuu matatu; la mnufaika ambaye anapata faida, waliopata kura kupitia walaji na wale ambao wametumia, kuona dunia ni yao na ambao hawaelewi kinachofanyika.

“Ukitaka kuvusha watu kwenye maji usishauriane nao kwani wanaweza kukushauri vibaya kwani wakati Rais Jakaya Kikwete anakabidhiwa majina ya wauza dawa na kutakiwa ataje hakutaja, nimeamua kutaja watu wanaanza kulalamika, hii vita hairudi nyuma ni endelevu ni lazima tumalize,” alisema.

Alisema ni vema kila kiongozi na wananchi kubadilika na kutambua kuwa matumizi ya dawa za kulevya ni janga la Taifa hivyo isitokee mtu kujaribu kukwamisha jitihada hizo.

Makonda alisema watumiaji wa dawa za kulevya wako tayari kuua, kubaka, kuiba au kufanya jambo lolote ambalo linakwenda kinyume na maadili ya nchi na utamaduni.

Aidha, alitoa ushauri kwa wazazi kununua kipimo cha 5 Panel Mult Drug Test 15, 15 kupima vijana wao ili kubaini kuwa wanatumia dawa au la.

Alisema kipimo hicho kina uwezo wa kupima dawa za kulevya zaidi ya saba, hivyo ni vema wazazi wakavinunua ili kuokoa jamii.

Maduka ya fedha

Makonda pia alisema ongezeko la maduka ya kubadilisha fedha ni moja ya vyanzo vya biashara hiyo ya dawa za kulevya.

Alisema kwa sasa Dar es Salaam ina maduka hayo zaidi ya 250 hali ambayo inachangia utakatishaji fedha haramu kupitia maduka hayo, hivyo kumwomba Kamishna kuangalia njia ya kutatua.

Kufukuza watu

Alisema kutokana na hali hiyo kuonekana kushika kasi anaweza kumfukuza mtu yeyote kwenye mkoa huo iwapo watabaini kuwa anakwenda kinyume na maadili ya nchi.

“Sheria inaniruhusu nikiona huendani na maadili ya mkoa wangu au ni hatari naweza kukuhamisha muda wowote na hakuna wa kunihoji,” alitamba.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo