Wadhamini NCCR wamtetea Mbatia madai ya kujimilikisha mali za chama


Suleiman Msuya

James Mbatia
BARAZA la wadhamini la chama cha NCCR-Mageuzi, limewataka wanachama na wapenzi wa chama hicho, kupuuza taarifa zinazosambazwa mitandao, zikimhusisha Mwenyekiti wao James Mbatia, kujimilikisha mali za chama.

Mwenyekiti wa Baraza hilo, Mohammed Tibanyandera, alitoa kauli hiyo jana katika taarifa yake iliyotolewa kwenye vyombo vya habari.

Kauli hiyo ya Tibanyendera imetolewa siku moja baada ya kada wa chama hicho, Faustine Sungura, kujitokeza katika vyombo vya habari na kutangaza kusudio la kumfikisha mahakamani Mbatia na Katibu Juju Danda, akiwatuhumu kuuza na kujimilikisha mali za chama kinyume na taratibu.

Tibanyendera alisema tuhuma hizo si za kweli na kwamba wanazozisambaza, wana mpango maalumu ambao wadhamini hawawezi kuuvumilia.

Alisema NCCR-Mageuzi ni chama kinachofanya uamuzi kupitia vikao vilivyoainishwa kikanuni na habari hizo hazina baraka za vikao halali vya chama.

Kwa mujibu wa Tibanyendera, Katiba ya chama hicho ya mwaka 1992 toleo la saba la mwaka 2014, imeagiza usimamizi wa mali za chama kuwa chini ya uangalizi wa Baraza la Wadhamini, kama ilivyotamkwa katika ibara 26 (7) (a) na (b).

“Tunapenda umma wa Watanzania na wanachama wote, watambue kuwa Mwenyekiti au kiongozi yoyote asiyekuwa mjumbe wa Baraza, hana mamlaka wala hawezi kuuza au kubatilisha umiliki wa mali za chama, bila ridhaa ya Baraza la Wadhamini,” alisema.

Kuhusu mali zinazoondosheka, alisema haziwezi kuwa mali za chama bila kuwepo kwa mikataba halali, inayosainiwa na mnunuzi na muuzaji.

Alisema uuzwaji wa mali zinazohamishika, hufanywa na Bodi ya Wadhamini kwa mujibu wa sheria inayosimamia muunganisho ya wadhamini kifungu 318 ya mwaka 2002.

“Baraza lina uhakika kuwa hakuna mali yoyote iliyotwaliwa binafsi inayomhusu Mwenyekiti, ingawa ana haki ya kumiliki, kununua au kumiliki mali iwapo aliyoipata kihalali,” alisema.

Mwenyekiti huyo alisema hakuna mwanachama yoyote aliyewahi kuwasilisha uthibitisho au kielelezo chochote cha uwepo au umiliki wa shamba, kiwanja kilichouzwa au kumilikiwa na Mbatia.

Katika tuhuma za Sungura, alitaka chama kitoe tamko rasmi kuhusu mali mbalimbali za chama, ikiwemo nyumba mbili katika eneo la Bunju B wilayani Kinondoni mkoani Dar es Salaam, pamoja na shamba la ekari 54 katika kijiji cha Kiromo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.

“Barua zangu za Novemba 30, 2016 na Desemba 06, 2016 kwa Katibu Mkuu, zilizonakiliwa kwa Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini la NCCR – Mageuzi na ambazo hazikujibiwa, nakala zake zimeambatanishwa. Ninaomba kurasa zake zipitiwe kwa umakini tafadhali,” alisema.

Sungura alidai baada ya kuchukua hatua hiyo, mmoja wa viongozi wa karibu na Mwenyekiti, alimtumia ujumbe wa simu akimwambia kuwa anaota ndoto, anapotea, ataharibikiwa, ana njaa, hana akili, aache roho mbaya kuangalia mali za watu kwa husuda na ana familia inayomtegemea.

Kada huyo aliomba uuzwaji wa nyumba ya vyumba 11 wilayani Tarime (Mara), nyumba ya vyumba sita Sumbawanga mjini (Rukwa) na nyumba ya vyumba vitatu Mpanda (Katavi), usitishwe hadi tamko la juu litolewe.

Alisema ni vema wanachama na wananchi wakaelewa ukweli, kwani juhudi zake za kufatilia mali za chama kiofisi (kwa kuandika barua), zimeshindikana badala ya kujibiwa kiofisi na baadhi ya viongozi walio karibu na Mbatia wanatumia nguvu kuchafua jina lake.

“Ikibainika kama ninasema uongo, niko tayari kuwajibika (kufukuzwa uanachama) kama ambavyo uongozi wako unavyotakiwa kutoa kauli juu ya chama kumiliki mali hizo au la,” alisema.

JAMBOLEO lilifanikiwa kumpata Katibu wa chama hicho, Danda ambaye alisema kinachofanywa na Sungura ni utovu wa nidhamu kwa kile alichodai kuwa anajua taratibu zinazohitajika kufuatwa kwa hilo analolidai.

“Kimsingi barua yake sijaipata, ila namuomba afuate taratibu kwani anajua njia za kufuata na amekuwa katika chama kwa muda mrefu, awe muwazi kuwa nataka nini ndani ya chama,” alisema.

Alisema kwa mujibu wa Ibara ya 26 Ibara ndogo ya (2) ya Katiba ya chama hicho, mali za chama zinasimamiwa na wadhamini hivyo ni vema akauliza hayo anayouliza.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo