Mgeja ahofia athari za uendeshaji nchi wa matukio


Suleiman Msuya

Khamis Mgeja
MWENYEKITI wa Taasisi ya Tanzania Demokrasia Foundation, Hamis Mgeja, amesema nchi inaendeshwa kwa matukio, hali ambayo inayotishia kuchelewesha jitihada za maendeleo na kukuza uchumi.

Mgeja alisema hayo jana wakati akizungumza na JAMBOLEO, ambapo alibainisha kuwa huu ni wakati wa kujikita katika uvumbuzi na utafiti utakaosaidia kuendeleza nchi.

Alisema iwapo utaratibu huo wa kuendesha nchi kwa misingi ya matukio utaendelea, ni dhahiri jitihada za kuchochea maendeleo zitakwama kutokana na matukio hayo kuchukua muda mrefu.

Mwenyekiti huyo alisema iwapo mfumo au utaratibu huo unaoonekana kugusa maslahi ya mtu mmoja mmoja utapewa nafasi katika kuongoza nchi, hauwezi kutatua changamoto zilizopo na kutaka mamlaka husika kuelekeza nguvu katika ubunifu na utafiti wa kuondoa umaskini.

Mgeja alisema umefika wakati kwa viongozi wastaafu hasa marais na viongozi wa dini, kushauri kuhusu misingi ya uongozi, itakayogusa maslahi ya watu wote bila yoyote kuona anaonewa.

Alisema Tanzania ni nchi ya kila mtu na hakuna mtu yoyote mwenye hati miliki, hivyo dhana ya kuheshimiana inahitajika.

Mwenyekiti huyo alisema inasikitisha kumuona Rais mstaafu Benjamin Mkapa, akijikita katika utatuzi wa migogoro ya nchi zingine, huku Tanzania ikiwa na viashiria vya watu kutokubaliana na chuki zikiongezeka.

“Kwa sasa hali ya nchi inaonekana imezingirwa na giza kwani wananchi hawajui wanaelekea wapi hasa katika misingi ya kidemokrasia, nchi inaenda kwa matukio na si kwa uvumbuzi,” alisema.

Mgeja alisema kwa hali ilivyo sasa, hakuna mtu aliye salama kwani ni jambo la kawaida kukuta mtu leo ameitwa Polisi au amekamatwa bila hoja za msingi.

Akizungumzia changamoto zinazotokea kwa sasa, alisema zinatokana na kukosekana kwa viongozi walioandaliwa kama alivyofanya hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

“Mwalimu alizingatia misingi ya kuandaa viongozi hali iliyochangia uadilifu na kuheshimiana kati yao, hivyo uamuzi wa viongozi walioandaliwa kuachwa, ndio matokeo yanayoonekana sasa,” alisema.

Mgeja alisema pamoja miongoni mwa changamoto zilizo ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), zilizochangia waondoke ilikuwa kukiukwa kwa misingi iliyojengwa na Mwalimu.

Kuhusu dawa za kulevya, alisema hilo ni tatizo la kidunia linalohitaji umakini wa hali ya juu pamoja na uchunguzi na kusema anamuunga mkono Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rogers Siyanga, ambaye ameweka bayana kuwa atazingatia misingi ya sheria katika kufanya kazi hiyo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo