Mke wa Rais: Vitendo vya udhalilishaji vimekuwa sugu


Hussein Ndubikile

Mwanamema Shein
MKE wa Rais wa Zanzibar, Mwanamema Shein, amesema vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto vimekuwa sugu katika jamii kwani vinasikika kila siku lakini havijapata ufumbuzi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Ikulu ya Zanzibar, Mwanamwema alitoa kauli hiyo jana katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani wakati akifungua kongamano la siku moja liliozungumzia udhalilishaji.

Kongamano hilo liliandaliwa na Taasisi ya Mwanaharakati, Bibi Siti Bint Saad.

Alisema licha ya kuwepo kwa kampeni dhidi ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia iliyoanzishwa mwaka 2014, bado jamii ina wajibu wa kutafuta mbinu na mikakati zaidi hasa ya kuelimisha ubaya wa vitendo hivyo.

Tuna wajibu wa kuchukua hatua za haraka kwani wahenga walisema ‘usipoziba ufa, utajenga ukuta’, sote tuache muhali, tuchukue hatua ili tuepuke kujenga ukuta kwani ni dhahiri vitendo vya udhalilishaji haviwezi kutusaidia kuwa na jamii bora ya waungwana na wastaarabu wenye maadili mema, alisema.

Aliitaka jamii kulinda haki za watoto na kuwakinga na vitendo vya udhalilishaji kwa kuziimarisha familia kwani familia zisizo imara huvunjika na kusababisha matatizo kwa watoto hasa kukosa malezi bora na haki zao nyingine.

Aliipongeza taasisi hiyo na nyingine kwa kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Saba katika kukabiliana na vitendo hivyo vibaya.

Mke wa Rais alisisitiza kuwa baadhi ya tafiti zilizofanywa hivi karibuni zinaonesha idadi ya talaka imeongezeka katika jamii sababu ambayo inatajwa kusababisha watoto kukosa ulinzi na watu wabaya kupata nafasi ya kuwadhalilisha.

Aliwataka wanandoa kuendelea kustahamiliana na kuwataka wazee wazidi kuzilinda ndoa za vijana wao kwa kuwasisitiza umuhimu wa kuvumiliana na kusameheana ili wajukuu wapate malezi bora.

Mwanamwema aliwasihi pia viongozi wa dini kuelimisha ubaya na athari za talaka.

Aliisisitiza kuwa katika kukabiliana na vitendo hivyo ni lazima wazazi wawe mstari wa mbele kuhakikisha watoto wanapata haki zao ikiwemo elimu huku akisisikitishwa kusikia kuwa katika jamii bado kuna wazazi wanaowakatisha masomo watoto wao ili waolewe.

Aliunga mkono kaulimbiu ya kongamano hilo inayosema kwamba; “Kina Mama Tumesema Unyanyasaji wa Kijinsia Sasa Sasi”.

Kwa upande wake, Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto, Maudline Cyrus Castico alisema wizara hiyo kwa kushirikiana na taasisi zinazopiga vita vitendo hivyo   inatekeleza wajibu wake kwa ushirikiano mkubwa na taasisi hizo zikiwemo za Serikali na zisizo za kiserikali.

Alifafanua kuwa Serikali inayoongozwa Dk. Shein haitakaa kimya ili kuhakikisha inatokomeza vitendo hivyo na mikakati mbalimbali imewekwa kufikia azma ya malengo yaliyowekwa na kueleza kuwa vitendo hivyo vilikuwepo tangu zamani lakini vilikuwa havitolewi taarifa.

Mwenyekiti wa taasisi hiyo, Nasra Mohammed Hilal alielezea umuhimu wa kushirikiana katika kupiga vita vitendo hivyo na kusisitiza kuwa kongamano hilo ni kati ya maagizo na maazimio ya taasisi yake.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo