…'Kutaja majina bila ushahidi si sahihi’


Charles James

IMAMU Mkuu wa Msikiti wa Swiratwal Mustaqima, Shekhe Haroun Matambo, amesema njia inayotumika kutaja majina ya watu katika vita dhidi ya dawa za kulevya, si sahihi na hata kitabu kitakatifu cha Quran kinakataza.

Akizungumza kwenye mawaidha ya Ibada ya Ijumaa jana kwenye msikiti huo Mabibo, Dar es Salaam, Shekhe Matambo aliunga mkono vita hivyo lakini akakosoa kuwa utaratibu unaofanyika sasa wa kutaja majina kabla ya uchunguzi haufai.

Kauli hiyo imekuja wakati vita iliyoanzishwa hivi karibuni na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ikipamba moto dhidi ya watuhumiwa wa uuzaji na utumiaji wa dawa hizo, huku watu wa kada mbalimbali wakiwamo viongozi wa dini, wanasiasa, wafanyabiashara na wasanii wakitajwa.

Shekhe Matambo alisema vita dhidi ya dawa za kulevya si ya nchi moja pekee bali ni ya kimataifa, lakini akashauri ni vema sheria na utaratibu wa kupambana na watu hao vikafuatwa.

Alisema njia ya kutaja majina ya watu si nzuri, kwa sababu Serikali inaweza kujikuta ikipoteza fedha nyingi kulipa waliotuhumiwa endapo watashindwa kuwasilisha vielelezo vya ushahidi kujihusisha na dawa hizo.

“Hata kitabu cha Quran kwenye Surat Hujirat aya ya sita, Mwenyezi Mungu anasisitiza kuwa usiifanyie kazi haraka habari ambayo umeletewa na mtu bila kuifanyia uchunguzi na upelelezi, ili usije kumvunjia mtu heshima yake mbele ya jamii ambayo inamwangalia.

“Serikali ndiyo yenye mamlaka, kama wana majina ya watu wanaojihusisha na biashara hii haramu, wangewaita kimyakimya na kuwahoji wakiwa tayari na vidhibiti, kisha wawapeleke mahakamani lakini kwa njia hii wanaweza wakajikuta wanalipa watu fidia nyingi baada ya kuharibu majina yao,” alisema Shekhe Matambo.

Alisema yeye na Waislamu wengine wanaungana na Serikali katika vita hivi lakini akasisitiza kuwa ni vema utaratibu mzuri ukatumika ili usije kuumiza watu huku akisema kipo kitengo maalumu cha kupambana na dawa za kulevya, ambacho kilipaswa kushughulika na watu hawa na si hali hii inayoendelea.

“Nampongeza ndugu yangu Kamanda Sirro (Simon), juzi nilimsikia hata yeye akisema inawezekana wapo watu wana visasi vyao, hivyo wakawa wanachongeana matokeo yake mmoja akaumia hivyo akasisitiza watu wawe na uhakika na habari wanazotoa kwa Jeshi hilo, hiyo ni kauli nzuri na ninaiunga mkono,” alisema Shekhe huyo.

Shekhe Matambo alitoa mwito kwa Serikali kushirikiana na viongozi wa dini katika kukabiliana na vita hivi huku akitaka busara, hekima na utaratibu wa kisheria kufuatwa bila kuharibu heshima za watu.

Pia alisema anaungana na wabunge waliotaka Serikali ifute biashara ya michezo ya kubahatisha (BET) kutokana na kuharibu kundi kubwa la vijana ambao wanaacha shule na wengine kuiba fedha majumbani mwao ili wakacheze.

“Napingana na Naibu Waziri wa Fedha, Dk Ashantu Kijaji ambaye alisema Serikali haiwezi kufuta kubeti kwa sababu kunaiingizia Serikali faida kubwa, anapaswa kufanya uchunguzi yakinifu kati ya faida inazopata Serikali na athari ambayo jamii inakumbana nayo kwa mchezo huo.

“Mwenyezi Mungu anasema kwenye Quran sura ya tano, kwamba kila mtu afanye kazi na si kupata fedha kwa njia haramu, na hata Rais Magufuli anasisitiza watu wafanye kazi na si kubeti kama Dk Kijaji anavyotaka kutuaminisha,” alisema Shekhe Matambo.

Alisema Serikali inapaswa kupambana na pombe za viroba ambayo vimegeuka sumu kwa vijana na wengi wamejiingiza kwenye ulevi huo, kwa sababu kwanza upatikanaji wake ni rahisi kwa maana ya bei.

“Viroba vimekuwa tatizo kwa asilimia kubwa ya vijana hasa madereva bodaboda, wanakunywa sana na h i inasababisha ajali nyingi barabarani, lakini pia kuua nguvukazi ya Taifa ambapo vijana ndilo kundi kubwa linalotegemewa kufanya kazi ili kuifikia Tanzania ya viwanda inayotakiwa na Rais Magufuli,” alisema Shekhe Matambo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo