JPM amkabidhi Waziri Mkuu ‘zigo’ vita ya dawa za kulevya


Suleiman Msuya

Rais John Magufuli
RAIS John Magufuli amekabidhi kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa mzigo wa mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini.

Baada ya kukabidhiwa jukumu hilo, Majaliwa alitaja wizara saba zitakazoshiriki moja kwa moja katika mapambano hayo.

Hatua hiyo imekuja ikiwa ni siku chache baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuanzisha operesheni ya kudhibiti dawa hizo.

Magufuli pia amekabidhi mapambano hayo kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rogers Sianga na viongozi wengine wanaohusika akiwataka kutoogopa mtu katika vita hivyo.

Alizungumza hayo jana Ikulu baada ya kuwaapisha wateule wake akiwamo Kamishna wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya na Kamishna Mkuu wa Uhamiaji, Dk. Anna Makakala, mabalozi na watendaji wengine.

“Waziri Mkuu nipo nyuma yako katika mapambano haya naomba uongeze mapambano usiogope mtu kwa sababu ya uwezo, sura, dini au jambo lolote,” alisema.

Rais Magufuli amepiga marufuku kiongozi au mtumishi umma kuhangaika na utetezi au kutoa msaada kwa Watanzania waliohukumiwa kifungo cha maisha au kunyongwa katika nchi mbalimbali duniani.

Alisema mapambano hayo ni vita vikubwa hivyo ni jukumu la Waziri Mkuu na watu wake kuhakikisha wanasimama imara kukabiliana nalo kwa maslahi ya Watanzania.

Alisema eneo hilo linakabiliwa na changamoto nyingi huku akikiri kuwa hadi alipofanya uteuzi wa kamishna wa tume hiyo hakuwa na taarifa kuwa anapaswa kufanya hivyo bali amemteua kutokana na vyombo vyake na kwamba vyombo husika havikumpa jina.

“Lakini kusema ukweli sikujua kuwa ninapaswa kuteua kamshina naamini hata Waziri Mkuu hakujua kuwa yeye ni Mwenyekiti wa Baraza la Kupambana na Dawa za Kulevya, walimficha,” alisema.

Alisema iwapo sheria isingeelekeza Waziri Mkuu kuwa mwenyekiti wa baraza hilo nafasi hiyo angechukua yeye ili kuhakikisha mapambano yanakuwa makubwa na kumtaka Majaliwa kutorudi nyuma.

Alisema hata mawaziri wanaopaswa kuwa wajumbe wa Baraza hilo hawakujua hali aliyosema inasababishwa na wasaidizi hao kutotoa taarifa.

Rais Magufuli alisema pamoja na kuwepo kwa sheria nzuri ya kupambana na dawa za kulevya, jitihada za kukabiliana na hali hiyo zimekuwa za kuisuasua.

Alisema mapambano hayo ni ya watumishi wote wa Serikali na kuwa kama yupo asiyetaka Serikali ifanye kazi yake ni vema akapeleka mapendekezo bungeni ili kufanya mabadiliko.

“Suala la dawa za kulevya lisiangalie cheo cha mtu hata kama akiwa kiongozi wa CCM. Aachwe afe mwenyewe kwani hakutumwa na chama,” alisema na kuongeza:

“Wapo vijana wengi wanaoathirika na dawa ya kulevya hivyo ni jambo la ajabu kama mtu atatetewa kwa kuwa ni kiongozi wa CCM. Hiyo haitakubalika na mimi nikigundua sitamvumilia.”

Alisema Serikali ina mambo mengi ya muhimu ya kufanya ila kwa sasa itahakikisha inapambana na dawa za kulevya popote bila kumuonea mtu.

“Niwaombe Watanzania hii ni vita kubwa, hivyo hakuna sababu yoyote ya suala hili kulifanya kwa mzaha kwani ni athari kwa nchi katika uchumi,”alisema.

Atoa onyo

Kuhusu Watanzania waliohukumiwa na kutuhumiwa kuuza dawa za kulevya ughaibuni, alisema hadi sasa taarifa zinaonesha wapo 1,007 katika nchi mbalimbali na kuzitaka mamlaka husika kuwaacha wanyongwe.

Alisema hakuna Serikali inayoweza kutetea watu wanaojihusisha na dawa za kulevya, Waziri wa Mambo ya Nje na mabalozi, waacheni wapate haki yao.

“Kama mtu ameshikwa katika nchi yoyote ambayo sheria zake ni kunyonga muache anyongwe, nasema hili kwa dhati simung’unyi maneno kwani tukicheka cheka Taifa letu litaangamia muwaache wanyongwe,” alisema.

Alisema kesi za dawa za kulevya nchini ni nyingi ambapo alibainisha kuwa Dar es Salaam pekee zipo kesi 50 na kuvitaka vyombo vyote vinavyohusika kushiriki kikamilifu kuhakikisha wanashinda kesi hata kama si kwa asilimia 100.

Rais alisema Watanzania hao 1,007 wamegawanyika katika nchi mbalimbali ambazo ni Msumbiji (20), Nepal (4), Iran (63), India (26), China (265) na 68 wamehumiwa kunyongwa.

Pia Brazili wapo (120), Uturuki (38), Ugiriki (25) Afrika Kusini (269), Malaysia na Thailand (16), Indonesia
(1), Comoro (3), Nigeria (1), Kenya (66), Uganda (15), Ghana (1), UIngereza (24), Japan (6) na wengine wengi.

Kamishna wa Uhamiaji

Akizungumzia Idara ya Uhamiaji, Rais Magufuli alimtaka Kamishina Jenerali Dk. Makakala kufanya mabadiliko makubwa ndani ya idara hiyo kwa kile alichodai wapo watu wanajiona wao ni kila kitu.

Alisema uamuzi wa kumteua mwanamke umezingatia uwajibikaji wake na kuwa alichokuwa anakifanya chuo cha uhamiaji aoneshe kwa vitendo aliyokuwa anayafundisha.

Rais Magufuli alisema wapo watu ambao wamekaa katika Idara lakini wamekuwa wakifanya mambo ambayo yanaenda kinyume cha utumishi.

“Mfano wa hivi karibuni tulipokea wageni wa asili ya Asia (Mabohora) zaidi ya 32,000 lakini hadi leo naulizia mapato ya visa hakuna taarifa nataka uanze na idara ya fedha kuifanyia mabadiliko,” alisema.

Alimtaka Kamishna Jenerali huyo kuhakikisha utaratibu wa kutoa hati ya kusafiria kiholela unadhibitiwa pamoja na uraia kwani inasababisha idara hiyo kushindwa kuwa chanzo cha mapato.

Mabalozi

Katika hatua nyingine, Rais Magufuli amewataka mabalozi wote aliyowateua kuiwakilisha nchi katika nyanja zote kuchochea uchumi na uwekezaji.

Majaliwa

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Mkuu alisema mapambano dhidi ya dawa za kulevya ndiyo yameanza huku akiwapongeza wakuu wa mikoa ambao wameonesha kuanza kukabiliana na tatizo hilo.

Alisema kupitia mawaziri wa wizara takriban saba anaamini jitihada zilizoanzishwa zinatapata nguvu, huku akisisitiza kutoonewa mtu yeyote katika mapambano hayo.

Majaliwa alisema ni wajibu wa vyombo vya dola kusimamia haki katika kukabiliana na hali hiyo kwani kutofanya hivyo inaweza kuwa sababu ya kuingia kwenye migogoro isiyo na sababu.

“Nasisitiza kuwa tumejipanga kukabiliana na hali hiyo ndiyo maana nimekuja na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambaye atasimamia usafirishaji na mawasiliano, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi.

“Nyingine ni Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Kilimo, Ufugaji na Uvuvi, Mambo ya Ndani na Mambo ya Nje ambazo kwa pamoja zitatusaidia kukabiliana na hali hii,” alisema.

Kamishna wa dawa za kulevya

Kwa upande wake, Kamishna Sianga alisema amejipanga kushirikiana na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi ili kupambana na hali hiyo.

Alisema atahakikisha makundi mbalimbali yaliyoathirika yanapata tiba na huduma ya elimu ya kuelewa madhara kama njia ya kukabiliana kwa hatua ya awali.

Sianga alisema kipaumbele chake ni kukabiliana na biashara ya bangi na mirungi ambazo zinapatikana nchini kabla ya kuongeza nguvu katika dawa ambazo zinatoka nje.

Kamishna wa uhamiaji

Kwa upande wake, Dk. Makakala alisema amejipanga vilivyo kukabiliana na changamoto ambazo Rais amezianzisha huku akisisitiza ushirikiano zaidi kwa watumishi wenzake.

Wengine walioapishwa jana ni Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Omar Yusuph Mzee, Balozi wa Tanzania nchini Ubelgiji, Joseph Sokoine na Balozi wa Tanzania nchini Uganda, Grace Mgovano.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo