Wasichana 4,000 wanusurika kukeketwa


Mwandishi Wetu, Serengeti

WASICHANA zaidi ya 4,000 wilayani hapa wameokolewa dhidi ya ukeketwaji kwenye makabila ya Wakurya na Wangoreme.

Katibu Tawala wa Wilaya, Cosmas Qamara alibainisha hayo kwenye maadhimisho ya Siku ya Kupinga Ukeketaji katika Kituo cha Nyumba Salama yenye kaulimbiu: Tujenge Ushirikiano Imara Kati ya Afrika na Dunia kutokomeza ukeketaji kufikia mwaka 2030.

Qamara alisema katika msimu uliopita wasichana 5,621 walikuwa wameandaliwa kukeketwa kati yao 4,100 sawa na asilimia 74 waliokolewa na 1,473 kukeketwa sawa na asilimia 26 ya walengwa.

Alisema mafanikio hayo yalitokana na mradi wa Tokomeza Ukeketaji Serengeti, unaotekelezwa na Amref Health Africa Tanzania, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Washehabise, Shirika la Imara, Nyumba Salama, Dawati la Jinsia la Polisi na wadau wengine chini ya ufadhili wa UN WOMEN, mabadiliko katika jamii yalionekana.

“Naliagiza Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua kali za kisheria wote wanajihusisha na vitendo vya ukeketaji, hatuwezi kuendekeza mambo yasiyo na msingi kwa maslahi ya mtu binafsi lazima tufike mahali suala hili likomeshwe kabla ya mwaka 2030,’’ alisema Qamara.

Ofisa Mradi wa Tokomeza Ukeketaji Serengeti, William Mtwazi alisema katika kipindi cha mwaka mmoja cha mradi wa Tokomeza Ukeketaji waliokoa wasichana 241 na kuwapeleka Nyumba Salama kwa usalama wa maisha yao.

Alisema watuhumiwa 32 wa makosa ya ukeketaji walikamatwa na kesi zilizo mahakamani ni 10 huku tatu zikiwa tayari zimehukumiwa na washitakiwa waliofungwa ni wanne.

‘’Katika siku hii maalumu ya kupinga ukeketaji duniani, tunazitaka jamii zinazoendeleza ukeketaji, kuacha mara moja kwa kuwa madhara yake ni makubwa kwa watoto wa kike na wanawake kwa jumla,’’ alisema Mtwazi.

Ofisa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Wilaya, Alfred Kyebe alisema mikakati inahitajika kukomesha vitendo hivyo ambavyo vinakumbatiwa na wazee wa kimila, mangariba na wazazi.

Alisema watoto wengi wanapofikishwa Polisi huwa wameandaliwa kusema uongo kwa lengo la kunusuru watoto wao na huchangia kuharibu ushahidi wa kesi nyingi.

Akizungumza kwa niaba ya wazazi, Christopher Genya alisema chanzo cha kukithiri ukeketaji ni mitizamo hasi ya baadhi ya wazazi ambao wanaona ukeketaji una faida kimila na desturi.

Alisema umefika wakati wa kuachana na ukeketaji na badala yake kusomesha watoto wa kike ili kujenga Taifa lenye usawa ambalo linathamini utu wa mwanamke kabla ya mwaka 2030.

Baadhi ya watoto waliokimbia ukeketaji walio Nyumba Salama waliiomba Serikali iwasaidie kupiga vita unyanyasaji wa kijinsia na kuwachukulia hatua wanaojihusha na vitendo hivyo kwa kuwa ukeketaji hauna faida.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo