Mihadarati kutikisa majaji na mahakimu


*Kamishina asema baadhi wamekuwa wakikwamisha vita
*Wengine wajifanya madaktari ili kutetea watuhumiwa

Suleiman Msuya na Hussein Ndubikile

Kaimu Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma
SASA ni dhahiri kwamba vita dhidi ya mihadarati itatikisa pia majaji na mahakimu nchini baada ya jana Kamishna wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Rogers Sianga kutangaza kuandaa orodha ya wanaokwamisha vita hivyo, ili wachukuliwe hatua stahiki.

Akizungumza Dar es Salaam jana kwenye mkutano ulioitishwa na Mkuu wa Mkoa huo Paul Makonda, Sianga alisema wapo majaji na mahakimu ambao wamekuwa wakiharibu kesi za dawa za kulevya kwa makusudi.

Katika mkutano huo ambao alikabidhiwa majina 97 ya vigogo wa dawa za kulevya na Makonda, Sianga alisema katika kuendeleza vita hivyo wameandaa ripoti ya majaji, mahakimu, watumishi wote ambao wamekuwa wakiharibu kesi zinazofikishwa mahakamani.

Kamishina huyo alisema ushahidi unaonesha kuwepo tabia ya baadhi ya majaji na mahakimu kuharibu ushahidi jambo ambalo linakwamisha jitihada za Serikali kupambana na dawa za kulevya nchini.

“Katika kuonesha kuwa tuko tayari kukabiliana na tatizo hili, tunataka kuanza na majaji na mahakimu ambao kwa makusudi wamekuwa wakivuruga na kuharibu kesi za dawa za kulevya, tunaanza nao, ila wapo watumishi ambao wameidhinisha viuatilifu ambavyo haviruhusiwi tutashughulika nao,” alisema.

Kamishina Sianga alisema hakuna mtu aliye juu ya sharia, hivyo dhana ya usawa katika mihilimi ya Dola ikiwamo Bunge na Mahakama, lazima izingatiwe bila kuangalia mtu fulani.

Alitolea mfano kesi ya Tanga ambako mtuhumiwa aliingiza kilo 50 na jaji kutoa uamuzi kuwa hakuna ushahidi ni lazima taarifa ziende kwa Jaji Mkuu.

Aidha, alisema yuko mtu alikutwa na kete 180 tumboni, lakini uamuzi wa jaji katika kesi hiyo ukasema mhusika alikuwa na vidonda vya tumbo, hali ambayo inakwamisha jitihada za Mamlaka.

Aliongeza kuwa kuna mikoa ambayo majaji na mahakimu walijivisha majukumu ya udaktari kwa kutetea washitakiwa waziwazi kuwa hawajihusishi na biashara ya mihadarati hiyo wakati walikamatwa na vidhibiti.

Alifafanua kuwa wafanyabiashara wa dawa hizo wakiachwa wataliletea Taifa madhara makubwa, ikiwamo kuchangia ugumu wa maisha na kuharibu nguvukazi ya Taifa.

Pia alisema matumizi ya dawa za kulevya yanasababisha madhara mengi katika jamii yakiwamo ya kiakili, kiafya na kiuchumi.

Aidha, alisema wanatafuta watumishi walioingiza viuatilifu tani 21 ambavyo vinatumika kuchanganywa na dawa za kulevya huku wakijua ni kosa kisheria.

Alisema hakuna ofisa aliyehusika atakayeachwa na hawataangaliwa vyeo badala yake watafikishwa kwenye vyombo vya sheria na kuchukuliwa hatua kama watu wengine.

“Kuna walioshiriki kuingiza viutalifu kinyume na sheria hawataachwa, wote waliohusika watakamatwa na kuchukuliwa hatua kama watu wa kawaida na Kamishna Mihayo Msikhela ameanza kazi hiyo,” alisema.

Alisema kila mtu anapaswa kutimiza majukumu kwa mujibu wa sheria na endapo atakwenda kinyume, amejipanga kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi ili kukabiliana na hali hiyo.

Aidha, alisema atahakikisha makundi ambayo yameathirika yanapata tiba na huduma ya elimu ya kuelewa madhara kama njia ya kukabiliana kwa hatua ya awali.

Sianga alisema kipaumbele chake ni kukabiliana na biashara ya bangi na mirungi ambayo inapatikana nchini kabla ya kuongeza nguvu katika dawa zinazotoka nje.

Alisema madhara ya mirungi ni kupata saratani na kupunguza nguvu za kiume huku bangi ikisababisha mtu kuwa na maruweruwe.

Sianga alisema takwimu za mwaka jana zinaonesha tani 20 ziliingia katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, hali ambayo inaonesha tatizo ni kubwa.

Akizungumza kwenye kipindi cha Mizani ya Wiki, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ukimwi na Dawa za Kulevya, Dk Faustine Ndungulile alisema takwimu zinaonesha zaidi ya Watanzania 250,000 wanatumia dawa za kulevya.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo