…Adaiwa kudhalilisha watoto wa mihadarati


Suleiman Msuya

KITENDO cha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, kuwaonesha hadharani watoto wenye umri wa chini ya miaka 18 na kuwatangaza wameathirika na Ukimwi kimekosolewa kuwa kimewaongeza watoto hao matatizo mengine.

Wanasheria na wabunge wametoa maoni hayo baada ya Makonda juzi kuwaonyesha watoto hao hadharani akisema wameacha dawa za kulevya huku mmojawapo akiathirika kwa Ukimwi.

Katika maoni yake, Mwanasheria James Marenga alisema alichofanya Makonda si sawa kisheria, huku akitoa angalizo kwa viongozi wengine kusoma sheria za nchi kabla ya kufanya mambo yao.

Marenga alisema baadhi ya vyombo vya habari vinapaswa kupongezwa kwa kutambua changamoto hiyo na kuficha sura za watoto hao.

Alisema ingawa sheria inaelekeza kuwa iwapo kitendo kinachofanyika ni kwa faida ya mtoto inawezekana kuwaweka wazi, lakini tukio la juzi ni kuongeza tatizo kwa watoto hao.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Mbunge wa Viti Maalumu na Mujumbe wa Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii, Suzan Lyimo alisema kitendo hicho ni kinyume na sheria ya mtoto na kimethibitisha, kwamba Makonda hatoshi kwenye nafasi aliyonayo kwa kuwaongeza matatizo watoto hao na kuwadhalilisha.

Lyimo alisema sheria ya mtoto iko wazi kuhusu haki za mtoto hivyo anasikitishwa mtu aliyeapa kulinda Katiba anaivunja kwa makusudi.

“Kimsingi Makonda hatoshi katika nafasi aliyomo, nadhani hata katika ngazi ya ukuu wa wilaya alionesha kufeli, kilichopo ni kubebana, ndiyo maana kila siku anaibuka na mambo yanayokwenda kinyume na taratibu,” alisema.

Alisema kitendo cha kuwaonesha watoto hao hadharani kinahatarisha maisha yao, kwani upo uwezekano wa kuwa alikuwa na mpenzi na hakumwambia kuwa ameathirika hivyo kumdhuru.

Mbunge huyo alisema halikadhalika kitendo hicho kimeweka mazingira mabaya kwa watoto hao kwa miaka ijayo, kwani inaweza kuwa sababu ya kunyanyapaliwa.


Alisema yeye akiwa mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii, atahakikisha kitendo hicho kinajadiliwa Bunge lijalo ili kuweka mambo sawa.

Mbunge Viti Maalumu, Anatropia Theonest (Chadema), aliungana na Lyimo kuwa kitendo hicho kinaongeza tatizo lingine kwa watoto hao.

“Kiuhalisia watoto hao wako kwenye matatizo ambayo yaliwapata wakiwa wadogo, halafu mtu mwingine kwa sababu ya kutafuta sifa anawaongeza tatizo, akiamini ndiyo njia sahihi ya kuwasaidia kumbe anapotea,” alisema.

Alisema viongozi kama Makonda ni janga kwa Serikali, hivyo hakuna sababu ya kuwavumilia kwani wanahatarisha usalama wa watu na nchi.

Dk. Hellen Kijo-Bisimba alisema ni wakati wa wasimamia haki kushikamana ili kukomboa Taifa kwa alichodai ni upungufu mwingi na ukiukwaji wa haki za watoto.

Mwenyekiti wa Bodi ya Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukita), Deus Kibamba alisema Makonda anajitahidi kufanya watu waache kujadili hoja za nchi na kumjadili mtu, jambo ambalo si sahihi.

Alisema zipo sheria zaidi ya tano ambazo zinaelekeza nini kifanyike kwa watoto kama wale, hivyo ni bahati mbaya kuna wakuu wa mikoa ambao wanavunja sheria na Katiba na si kuilinda.

“Inaniuma kukaa kujadili sokomoko ambalo analileta Makonda katika nchi kwa udhaifu wake wa kutojua sheria na Katiba au labda anafanya hivyo ili aonekane,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo