Rufaa ya Nangole Longido yatupwa


Seif Mangwangi, Arusha

Onesmo ole Nangole
MAHAKAMA ya Rufaa imetupilia mbali rufaa iliyokatwa na Chadema kupinga kutenguliwa ubunge kwa mbunge wa Longido, Onesmo ole Nangole.

Hatua hiyo imetokana na kukiuka amri ya Mahakama iliyowataka kufanya marekebisho kwenye maeneo mawili ya rufaa yao na badala yake mawakili wakafanya marekebisho sehemu kubwa ya rufaa.  

Akisoma uamuzi wa jopo la majaji watatu, Bernad Luanda, Mussa Kimpeka na Stela Mgasha, Msajili wa Mahakama hiyo, Amir Msumi alisema Mahakama imeondoa rufaa hiyo kutokana na kukiukwa kwa amri yake.

Alisema warufani waliamriwa kufanya marekebisho kwa kuongeza wadaiwa wawili ambao ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali na aliyekuwa Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Longido, lakini badala yake rufaa imefanyiwa marekebisho na kuongeza mambo ambayo hawakuamriwa, hivyo Mahakama inaiondoa rufaa hiyo.

Wakati wa kuanza kusikilizwa kesi hiyo Februari 20, Wakili Dk Masumbuko Lamwai, aliyekuwa akimtetea mgombea wa CCM, Dk Steven Kiruswa aliwasilisha pingamizi mahakamani kuiomba Mahakama hiyo kuitupilia mbali rufaa hiyo iliyokatwa na mgombea wa Chadema, kwa kuwa ilikiuka amri na maelekezo yake ya kufanya marekebisho kwa kuongeza wadaiwa wawili tu.

Aidha, Mahakama hiyo iliwaamuru wakata rufaa kulipa gharama za kesi za wakili mmoja badala ya watatu, ambao ni Dk Lamwai, Edmund Ngemela na Daud Haraka.

Baada ya uamuzi huo, aliyekuwa mgombea ubunge kupitia CCM, Steven Kiruswa, aliipongeza Mahakama kwa kutenda haki kutokana na kasoro zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mkuu Oktoba mwaka juzi.

Alisema Mahakama imetenda haki hivyo kupata matumaini ya mfumo wa haki kutupilia mbali rufaa hiyo na hiyo inathibitisha uamuzi wa Mahakama Kuu ulikuwa sahihi na kusisitiza kuwa ukweli umebainika na ndiyo maana haki imepatikana.

Dk Lamwai alisema hukumu imejikita kwenye marekebisho, hivyo anaomba upande ulioshindwa kukubali matokeo na kuwezesha uchaguzi kurudiwa ili wananchi wa Longido wapate mwakilishi.

Alisema kesi hiyo imechelewesha muda na kuwanyima haki ya maendeleo wananchi wa Longido na haiwezekani kukaa bila mbunge.

Wakili Method Kimomogolo aliyekuwa akimtetea Nangole, alisema wanatafakari uamuzi huo na kuangalia usahihi wake, ili wasonge mbele na kudai kuwa rufaa haijatupwa, kwa sababu haikusikilizwa na bado ipo nafasi ya wao kusikilizwa hivyo wataendelea kuwasiliana  na mteja wao ili kuona kama watakata rufaa nyingine.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo