Makonda ataja polisi, wasanii wa mihadarati


Salha Mohamed

Paul Makonda
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ameibuka na kutaja askari zaidi ya 10 na wasanii saba wanaodaiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya na kuwataka kuripoti leo kituo kikuu cha Polisi.

Aidha, ametoa siku saba kwa vijiwe vinavyojihusisha na uuzaji na utumiaji wa dawa hizo kuondoka na kumtaka Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro na timu yake, kukosa sifa za kuendelea kuwa askari endapo watashindwa kumaliza tatizo hilo.

Makonda alisema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mkoa huo kukithiri watumiaji na wauzaji wa dawa za kulevya nchini katika operesheni aliyofanya usiku wa kuamkia jana.

“Dar es Salaam umekuwa mji wa wauzaji, wasafirishaji na watumiaji ‘unga’ na mbaya zaidi sasa tunaanza kuhudumia mikoa mingine na mwishowe linakuwa lango la watu kupitisha dawa za kulevya kwenda nje ya nchi.

 “Wapo askari waaminifu na waadilifu ambao wanafanya kazi kubwa kuhakikisha vita hivi vinazaa matunda lakini wapo wasio  waadilifu ambao wamekuwa sehemu ya kuhakikisha mapambano haya hayafanikiwi,” alisema.

Alisema katika operesheni hiyo, alijiuliza sababu ya dawa kutokwisha huku askari wakiwapo ambapo hata waendesha pikipiki wanawajua.

“Polisi wanashindwaje kufahamu kama huyu anafanya hiyo biashara? Sasa nimepata taarifa kwamba polisi wanashirikiana na wafanyabiashara wa dawa za kulevya na hatimaye biashara hii kuwa ngumu kutokomezwa,” alisema.

Aliwataka askari hao kukamatwa na kuwekwa mahabusu kwa kushiriki na hata kuwapigia simu wauzaji kuwa wanakwenda kuwakamata na kuwataka kuwaingizia fedha mtandaoni na anapokwenda huwakosa.

Alisema polisi wanawajua wauzaji huku kila Jumamosi wakienda kuchukua fedha.  

Makonda alisema ameamua kutimiza azma ya Rais John Magufuli ya kumaliza tatizo hilo huku akibainisha kuwa fahari yake si kuona idadi ya watu waliokamatwa, bali mkoa unakosa sehemu ya dawa za kulevya.

“Nilifanya utafiti mdogo nikakutana na vijana wanaotamkwa kutumia dawa, walio kwenye vituo vya kusaidia vijana wanaotumia dawa, nimekutana na madereva teksi wakiwamo wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) kujua kwa nini tatizo la dawa za kulevya halitokomei ndani ya mkoa wetu,” alisema.

Alisema katika utafiti huo alibaini kuwa wanaofanya biashara hizo ni wenye uwezo mkubwa, wa kati, wasambazaji na kufikia watumiaji.

“Mimi na ndugu zangu tumekesha leo (jana) usiku kucha, kuona maeneo na sehemu ambazo biashara hizi wanafanya…kwa masikitiko makubwa tumekuta biashara inafanywa hadharani tena si ngumu hata kuifahamu na kila mtu anaifahamu.

Alisema katika biashara hiyo, wapo wananchi wa kawaida   na wageni na mbaya zaidi baadhi ya vyombo vya Dola vikifahamu.

Makonda aliongeza: “Nimeamua kuingia mwenyewe kwenye hivi vita kwa sababu najua siku moja Mungu ataniuliza nilipopewa ukuu wa mkoa watoto waliangamia kwa dawa za kulevya, sitaki kufika Mbinguni bila jibu.”

Alisema yuko tayari kupoteza ukuu wa mkoa, kutangulia mbele za haki, lakini awe na jibu kwa Mungu wake kuwa dawa za kulevya hazikubaliki mkoani humo.

Makonda aliongeza kuwa idadi ni kubwa kwa wauzaji na wasambazaj,  huku akibainisha kuwapo wanaosemekana kutumia dawa hizo ambapo wakihojiwa husema na kuwataja kuwa wanatumia wote.

“Hawa nao ni vema nikakutana nao kesho (leo), wapo wengi …hawa wengine nimeshawatia mikononi mwa sheria nawahitaji ni vijana wenzangu nafikiri tutaelewana vizuri,” alisema.

Alisema yapo maeneo ambayo wamepata leseni ya biashara  lakini wanafanya biashara ya dawa za kulevya na kuonekana wazi ambapo watu wamedai kupata sehemu hizo.

Alisema mapambano hayo si rahisi lakini kwa kuwa walikula kiapo na Mungu kuwapa nafasi ya kuongoza, alitaka dawa za kulevya mkoani mwake kuwa historia.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo