CCM yasherehekea miaka 40 bila JPM, Dk Shein


Fidelis Butahe, Dodoma

Miaka 40 ya Chama cha Mapinduzi
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) jana kimeadhimisha miaka 40 tangu kuanzishwa kwake bila uwepo wa mwenyekiti wake, Rais John Magufuli huku ikielezwa kuwa kiongozi mkuu huyo wa nchi atachagua siku na mahali pa kuadhimisha sherehe hizo.

Aidha, chama hicho kimetangaza kuanza kufanya mikutano ya ndani nchi nzima kuanzia ngazi za chini.

Mbali na kukosekana kwa Magufuli, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohammed Shein na Makamu wa Rais, Samia Suluhu, nao hawakuhudhuria sherehe hizo zilizofanyika katika ukumbi wa mikutano wa CCM Dodoma.

Pia, marais wastaafu, Jakaya Kikwete, Benjamin Mkapa na Ali Hassan Mwinyi nao hawakuhudhuria.

“Nawaletea salamu kutoka kwa mwenyekiti wetu Rais Magufuli…, yeye atachagua siku, wapi na tarehe ya kuadhimisha miaka 40,” alisema Abdulrahman Kinana, Katibu Mkuu wa CCM wakati akizungumza na maelfu ya wanachama wa chama hicho Mkoa wa Dodoma waliohudhuria sherehe hizo huku akieleza mambo mazuri yaliyofanywa na Rais huyo wa Awamu ya Tano kwa kuibadilisha nchi katika kila sekta, sambamba na kurejesha uwajibikaji.

Baadhi ya viongozi waliohudhuria sherehe hizo ambazo Katibu wa Itikadi na Uenezi wa chama hicho, Humphrey Polepole alibainisha kuwa mkoa wa Dodoma umepata bahati kutokana na viongozi wengi kuhudhuria ni Spika wa Bunge, Job Ndugai na naibu wake, Dk Tulia Ackson.

Wengine ni mawaziri wakuu wastaafu, Mizengo Pinda na John Malecela,  kada mkongwe wa chama hicho, Job Lusinde, makamu mwenyekiti wa chama hicho, Philip Mangula.

Kukosekana kwa mwenyekiti huyo wa CCM kulizua maswali miongoni mwa wanachama waliokuwepo katika ukumbi huo kabla ya ufafanuzi kutolewa na Kinana, huku Katibu wa Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole akieleza utaratibu wa maadhimisho hayo kuwa yanafanyika kila mkoa nchini.

Katika maadhimisho ya miaka 39 sherehe hizo zilifanyika  mkoani Singida huku yale ya 38 yakifanyika mkoani Ruvuma na Mbeya yalifanyika ya 37 na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CCM, akiwemo  Rais mstaafu Jakaya Kikwete ambaye alikabidhi kijiti cha uenyekiti kwa Dk Magufuli.

Akihusisha maadhimisho hayo kufanyika kila mkoa na kubana matumizi, Kinana alisema maadhimisho si sherehe na kuwataka wananchi kuachana na utaratibu wa sherehe kwa sababu wanaonufaika ni wachache.

“Wanaopata kadi za mialiko na kula vizuri ni walewale. Maadhimisho ya siku ya uhuru pale Ikulu kuna watu wanaalikwa? Nahakika mambo yote haya kutakuwa na malalamiko lakini ndio tunajenga uwajibikaji. Tuiunge mkono Serikali katika kusimamia matumizi na fedha za umma,” alisema Kinana.

Awali kabla ya maelezo ya Kinana, Polepole alisema jana haikuwa siku ya uzinduzi au kilele cha maadhimisho hayo bali wamelenga kufanya mikutano ya ndani nchi nzima.

“Tumeona tufanye tofauti si katika uwanja wa mpira, tumeona tukae tujadiliane tumetoka wapi, tupo wapi na tunakwenda wapi. Maadhimisho haya mkoani hapa yanafanyika kila mkoa nchini na tunafanya hivi mwaka mzima,” alisema Polepole.

Alisema lengo ni kujadiliana na kutoka na mwongozo kwa mwaka 2017 ikiwa ni pamoja na kuwafanya wananchama wa chama hicho kuwafikia wananchi.

Akitoa salamu zake kwa maelfu ya wanachama wa CCM, Majaliwa alisema Serikali itahakikisha inatekeleza ahadi zake kwa wananchi. “Wajibu wetu wana CCM ni kukisema chama chetu, kuisema serikali yetu na kuhakikisha chama kinakuwa imara,” alisema.

Katika maadhimisho hayo, Mangula alieleza sababu za chama hicho kuwa cha mapinduzi na kubainisha mambo kadhaa mazuri yaliyofanywa na Serikali.

Kinana na siri za ushindi CCM

“Chama chetu kina sifa za kuona mbali na kujua kifanye nini. Tunatazama nchi inakwenda wapi na watu wanafanya nini. Tukiona mbali mazuri tunayapeleka mbele mabaya tutayasawazisha, tunafanya mageuzi kila kipindi na kufanya tahmini kila mara, ya wazi na faragha,” alisema Kinana.

Alisema CCM kina njia mbalimbali za kupata wagombea wake kwa kutaka kila mwanachama ashiriki na kubainisha kuwa huko ni ndio kwenda na wakati akifafanua “Tunafanya tahmini ya namna chama kinavyokubalika. Hii tunafanya wenyewe kwa kutumia njia zetu. Mwaka jana tumefanya tathmini ya mwaka mmoja wa uongozi wa Rais Magufuli.”

Alisema chama hicho kikishindwa watu wanaulizana kimeshindaje bila kujua mambo kinayoyafanya kupitia tathmini hizo na vikao mbalimbali na kubainisha kuwa tahmini yam waka 2015 ilikuwa kabambe kutokana na kufanyika kwa miezi 12.

“Tuliagiza kuanzia ngazi za chini za chama kutazama wanavyokiona chama na kutuletea maoni na mapendekezo yao. Tulifanya hivi kukiimarisha chama chetu kiendelee kuongoza na kushinda, pili kupunguza urasimu na umangimeza ndani ya chama kama watu kukaa maofisini na kujishughulisha na mambo yao wenyewe na kutokwenda kwa wananchi,” alisema Kinana.

Alisema lengo jingine ni kupunguza gharama za kuendesha chama kutokana na wali kuwa na vikao vingine huku watu wakilipwa posho za mara kwa mara.

Huku akitolea mfano wa uchaguzi wa mgombea udiwani katika moja ya Kata nchini alisema: “Kuna mmoja alishindwa katika kura ya maoni kwa kupata kura tisa na alikuwa Katibu wa Uenezezi ila aliyeshinda alipata kura 56, wahusika wakaanza kuulizana watamuachaje katibu mwenezi huyo ambaye alishindwa na mwanachama wa kawaida. Watu wa aina hii hatuwataki tena CCM.”

Alsema kazi iliyopo sasa ni kutahmini mageuzi ndani ya chama hicho ikiwa ni pamoja na muundo wa vikao vya chama hicho kuanzia ngazi ya shina hadi Taifa.

“Tutajadili katika Halmshauri Kuu na Kamati Kuu hivi karibuni ila Rais Magufuli amesema kutokana na kuwa mabadiliko ni mengi yapelekwe kwenye mkutano mkuu wa chama. Lengo la CCM ni kuwajali wananchi ndio maana Rais Magufuli ameanza kuchukua hatua kupunguza kodi mbalimbali ili kuwaondolea ugumu wa maisha wananchi katika biashara na shughuli zao mbalimbali,” alisema Kinana.

Alisema chama hicho kinafanya uchaguzi wa viongozi wake mwaka huu na kuwataka wanachama kuchagua watu makini
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo