Rais Magufuli, Mungu anakuona

Mashaka Mgeta

Mashaka Mgeta
FEBRUARI 2, mwaka huu, Rais John Magufuli alihutubia kilele cha Siku ya Sheria, akiweka wazi namna Mahakama iliyo sehemu ya mihimili mitatu ya nchi, inayovyokabiliwa na changamoto lukuki.

Kabla ya ‘kuzimwaga’ changamoto hizo, Rais Magufuli alitambua na kupongeza kazi nzuri zinazofanywa na Mahakama katika kuhakikisha kila raia anapata haki kwa kadri inavyoainishwa kwenye matamko ya haki za binadamu.

Ieleweke kwamba kwa muda mrefu sasa, Mahakama inayotarajiwa kuwa kimbilio la wanyonge, imejikuta ‘ikichafuka’ kutokana na watendaji wake hususani baadhi ya mahakimu na majaji kukosa uadilifu.

Watendaji hao wamedaiwa kwa nyakati tofauti wakishirikiana na watu wenye mamlaka na nguvu za kiuchumi na kisiasa, kuwakandamiza wanyonge wasiokuwa na uwezo kama wao.

Lakini hali haipo katika mtazamo huo pekee, wapo watendaji wa Mahakama, hata kama ni kwa idadi ndogo, wanaotajwa kupanga na kushiriki mbinu za kisheria, kuuza haki za watu na hujuma dhidi ya taifa kwa ujumla.

Mbinu hizo zinadaiwa kufanyika katika hatua tofauti ikianzia upelelezi, uundwaji wa mashtaka, ushahidi na mwenendo wa kesi. Wanaoistahili haki wanaikosa.

Tanzania inakuwa miongoni mwa nchi zisizokuwa salama katika mukhtadha wa haki za watu. Rais Magufuli anapozungumza na watendaji wa Mahakama, anajiweka kando na unafiki, anasimamia ukweli akibainisha changamoto zinazopaswa kutekelezwa na mhimili huo.

Anabainisha mbinu tofauti zinazotumika ‘kuharibu’ mashauri yaliyopo mahakamani, ikiwamo mtindo maarufu kama ‘kupaki kesi’, lengo likiwa ni kufanikisha azma ya kuubadili ukweli kuwa uongo ama mwenye haki kutoistahili.

Ni wazi kwamba Rais Magufuli ‘alivyojifunua’ kwa ukweli na uwazi, akijielekeza katika utendaji kazi wao, majaji na mahakimu wanapaswa kujitafakari.

Watumie ujasiri, taaluma na maadili yao kukwepa kila aina ya shinikizo zinazowafanya washiriki katika ‘kuuza’ haki za watu ama hujuma kwa taifa.

Akishamaliza kuelezea changamoto zinazoikabili Mahakama, akajitokeza mjane aliye mkazi wa Tanga, Swahaba Shosi, akielezea namna wenye mamlaka na nguvu za fedha wanavyoitumia mahakama kutaka kumpora haki zake.

Akifanikiwa ‘kuokolewa’ na Rais Magufuli baada ya askari wa ulinzi na usalama kufanikiwa kumdhibiti asifikishe ujumbe alioukusudia, Shosi akaeleza kwa kirefu namna watendaji wa umma ikiwamo Mahakama, na miongoni mwa waliomo katika sekta binafsi, wanavyoshirikiana kupora haki zake.

Kwa kadri ya maelezo ya Shosi yanayogota kwenye msingi wa kunyimwa haki ya kurithi mali za marehemu mumewe, akazitaja taasisi husika kuwa ni pamoja na polisi, Mahakama, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (CAG).

Kwa kadri Shosi alivyojieleza mbele ya Rais Magufuli, pasipo kujikita katika hoja tofauti zilizotolewa na wanaojitambulisha kuwa ni miongoni mwa watoto wa marehemu, ilidhihirisha wazi kuwa na uhakika wa kile alichokuwa akikiwasilisha.

Hilo linaweza kuwa si jambo la maana sana katika Makala haya, isipokuwa ni vizuri kubaini kwamba uwasilishi wake uliakisi sehemu ya hoja za Rais Magufuli dhidi ya udhaifu ama changamoto zinazoikabili Mahakama.

Haki za wanyonge zinapoiukwa na walio kwenye mamlaka hasa katika jeshi la polisi, taifa haliwezi kubaki salama. Watu wake hawawezi kuwa na furaha kwa kadri inavyopaswa.

Ndio maana (pengine) ‘akifunuliwa’ kwa namna ya pekee, Rais Magufuli akakemea ‘uovu’ unaojitokeza kwenye Mahakama za ndani, kisha dakika chache baada anajitokeza mjane anayelalamikia udhaifu kama uliotajwa na Kiongozi Mkuu huyo wa nchi.

Ni kama kusema katika hili, Mungu alimuona Rais Magufuli katika dhamira na utashi wake wa kusema na kuisimamia kweli. Kwamba yapo mazingira ambapo Mahakama inatumika (kupitia watendaji wasiokuwa waadilifu ama kwa shinikizo), kupora haki za watu.

Wapo walioamini kuwa Rais Magufuli ananukuu taarifa zinazofikishwa kwake kutoka vyombo mahususi vilivyo chini ya ofisi yake.

Tafakari iliyopo ni kwamba, ilikuwaje siku ambapo Rais Magufuli ameguswa kuikosoa Mahakama na kuionya isishiriki kupora haki za watu ama hujuma dhidi ya uchumi wa nchi, akajitokeza Shosi akiwa na madai yanayounga mkono hoja za Rais?

Kwa matukio hayo mawili, Mahakama katika ngazi zote, inapaswa kujitafakari, kujitathmini na kupata mwelekeo mpya wa kuhakikisha kusudio kuu la kuwapo kwake kati ya mihimili mitatu ya nchi, linafanikiwa.

Kama ilivyo kwa kila mhimili katika utawala wa nchi kuwa na umuhimu wake, Mahakama ina wajibu mpana kwa dhamana inayoainishwa hata kwenye ulimwengu wa kiroho, kwamba haki ya mtu inamstahili kila aliyeumbwa na Mwenyezi Mungu.

Wakati Rais Magufuli akiibua hoja ambazo si rahisi kwa wakuu wa nchi kuzitoa, Mahakama inapoingia katika uongozi wa Kaimu Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma, isijipambanue na ‘kuzaliwa upya’.

Mahakama isimamie misingi ya haki, itende haki na kutoa haki kwa watu wote pasipo kujali asili inayotokana na itikadi za kisiasa, dini, kabila ama vinginevyo.

Kwa maoni: 0754691540
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo