Watakiwa kudhibiti ujenzi mabondeni


Leonce Zimbandu

Sophia Mjema
WATENDAJI wa kata na mitaa wametakiwa kudhibiti ujenzi wa makazi mabondeni ili kuiepushia Serikali migogoro na wananchi, ukiwamo ulitokea katika bonde la Mkwajuni.

Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema, alitoa rai hiyo kwenye kilele cha Wiki ya Upandaji Miti katika kata ya Msongola mwishoni mwa wiki iliyopita.

Alisema watendaji kushuhudia wananchi wakijenga katika maeneo hatarishi na kushindwa kudhibiti mapema, ni tatizo sugu na kukosa uamuzi.

“Watendaji wanapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuondoa kero kwa wananchi ili mabonde hayo yatumike kupandwa miti,” alisema.

Alisema iwapo watendaji watawajibika vizuri, malalamiko ya wananchi kuhusu migogoro ya ardhi yatapungua, ikiwamo ujenzi holela kwenye vyanzo vya maji.

Mjema alitaka wananchi wahamasishwe na kupewa elimu ya kutosha kuhusu umuhimu wa kutunza maeneo oevu kwa kupanda miti ya asili ikiwamo mipingo, mininga na mivule.

Diwani wa Kata ya Msongola, Azizi Mwalile alisema amefurahishwa na hatua ya Serikali kuteua sherehe za kilele za upandaji miti kwa mkoa wa Dar es Salaam kufanyika kwenye kata yake.

Alisema hiyo ni heshima kwake, hivyo aliwataka wananchi kupanda miti katika maeneo yao ili kunufaika nayo, ikiwamo kuvuna mbao, dawa na kudhibiti saratani.

“Viongozi wa kata ya Msongola tumepata elimu ili kuhamasisha wananchi kupanda miti katika maeneo yao,” alisema.

Mwenyekiti wa Kamati ya shule ya Msingi Yange yange, Mrisho Goa alisema shule yake itakuwa mfano katika kata ya Msongola baada ya viongozi wa mkoa kupanda miti siku hiyo.

Alisema anatarajia baada ya mwaka mmoja ugeni huo utafika tena katika shule hiyo ili kukagua maendeleo ya miti waliyopanda.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo