Mahakama yaombwa kuruhusu washitakiwa kusafirishwa


Grace Gurisha

SERIKALI imewasilisha maombi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwasafirisha Ali Hatibu Haji maarufu kama Shikuba na wenzake wawili kwenda nchini Marekani kukabiliana na tuhuma za kujihusisha na dawa za kulevya.

Maombi hayo yaliwasilishwa jana kwa nyakati tofauti na Wakili wa Serikali Mkuu, Edwin Kakolaki akishirikiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Veronika Matikila mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Cyprian Mkeha.

Kakolaki alidai kuwa maombi hayo yameanzishwa na Waziri wa Katiba na Sheria na kwamba Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) alipatiwa nakala kwa ajili ya kufuatilia, ambapo aliyawasilisha maombi hayo chini ya sheria ya kusafirisha wahalifu na kuomba yasikilizwe kwa njia ya mdomo.

Alidai kuwa maombi hayo ni kwa ajili ya kuwakamata na kuwasafirisha kwenda nchini Marekani wajibu maombi hao watatu kwa ajili ya kujibu mashtaka ya kujihusisha na dawa za kulevya.

Aliwataja wanaotakiwa kusafirishwa kuwa ni Shikuba, Iddi Salehe Mfuru na Tiko Emmanuel Adam. Pia aliomba Mahakama itoe amri ya kuwahifadhi watuhumiwa wakati wa nasubiri kibali cha kuwasafirisha nje ya nchi kwenda kukabiliana na mashtaka yanayowakabili.

Wakili wa Shikuba, Majura Magafu akishirikiana na Hudson Ndusyepo alieleza kuwa wamesikia maombi ya upande wa mashtaka na akaomba wapewe muda. Magafu alidai kuwa suala la kumtoa raia wa nchi yako nje ya nchi siyo suala rahisi.

Kwa sababu walikwishafikishwa mbele ya mahakama aliomba ahirisho ili waweze kupata nafasi ya kupitia makablasha waliyopewa.Alibainisha kuwa makablasha hayo ni hati ya ushahidi ambao unatarajiwa kutolewa nje ya nchi.

Hakimu Mkeha aliipanga kesi hiyo hadi leo kwa ajili ya kuyasikiliza maombi hayo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo