Bei petroli chini, dizeli juu


Celina Mathew

MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) imetangaza bei kikomo za mafuta.

Bei hiyo ya  petroli imeshuka kutoka Sh 2,060 hadi Sh 2,057 kwa lita sawa na punguzo la asilimia 13 huku dizeli ikipanda  kutoka Sh 1,913 hadi Sh 1,925 kwa lita sawa na ongezeko la asilimia 12 ambapo bei hizo zinaanza kutumika rasmi leo nchi nzima.

Aidha, kutokana na kupanda huko kwa bei, mafuta ya taa sasa yamepanda na yatauzwa Sh 1,858 kutoka Sh 1,852 ambayo ilikuwa bei ya awali.

Akizungumza Dar es Salaam jana kwa niaba ya Mkurugenzi wa Ewura, Felix Ngamlagosi,  Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka hiyo, Titus Kaguo  alisema kushuka au kupanda kwa bei hizo za mafuta ni kutokana na mabadiliko katika soko la dunia, mfumuko wa bei na gharama za usafirishaji ikilinganishwa nba mwezi uliopita.

Alisema bei za jumla na rejareja kwa petroli, mafuta ya taa na dizeli zimebadilika ikilinganishwa na toleo lililopita la Machi mosi na kwamba petroli imepungua kwa Sh tatu sawa na asilimia 0.13. Aidha bei ya jumla imepungua Sh 5.65 kwa lita sawa na asilimia 0.29.

Pia bei ya rejareja kwa dizeli imeongezeka Sh 12 kwa lita sawa na asilimia 0.63 ambapo bei ya jumla imeongezeka kwa Sh 9.11 kwa lita sawa na asilimia 0.50.

Aidha, bei ya mafuta ya taa imepanda Sh saba kwa lita sawa na asilimia 0.36 wakati bei ya jumla imepanda kwa Sh 3.68 kwa lita sawa na asilimia 0.21.

“Kwa kiasi kikubwa mabadiliko haya yanatokana na mabadiliko ya bei za mafuta katika soko la dunia, mfumuko wa bei na gharama za usafirishaji tofauti na mwezi uliopita,” alisema.

Aliongeza kuwa Machi hakuna mzigo wa mafuta uliopokewa nchini kupitia bandari ya Tanga na kwamba bei za rejareja za mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa zimeongezeka Sh saba kwa lita, sawa na asilimia 0.32, Sh saba kwa lita sawa na asilimia 0.34, Sh saba kwa lita sawa na asilimia 0.44 sawia.

Vilevile bei za jumla za mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa zimeongezeka Sh 3.68 kwa lita sawa na asilimia 0.19. Sh 3.68 kwa lita sawa na asilimia 0.20 na Sh 4.32 kwa lita sawa na asilimia 0.28 sawia.

“Ongezeko la bei za mafuta linatokana na ongezeko la faida ya wauza  mafuta wa jumla na rejareja kutokana na marekebisho yaliyofanywa kukidhi matakwa ya mfumuko wa bei kwa mujibu wa kanuni ya ukokotoaji wa bei za mafuta katika mwaka 2016,” alisema.

Aidha, aliukumbusha umma kuwa bei kikomo za mafuta kwa eneo husika zinapatikana kupitia simu za mkononi kwa kupiga *152*00# kisha wafuate maelekezo na kwamba huduma hiyo inapatikana bure kupitia mitandao yote ya simu nchini.

Kaguo alisema kwa mujibu wa sheria ya mafuta ya mwaka 2015, bei za bidhaa za mafuta ya petroli zitaendelea kupangwa na soko, hivyo wao Ewura wataendelea kuhamasisha ushindani kwa kutoa taarifa za bei kikomo za bidhaa hiyo, kwa lengo la kusaidia wadau kufanya uamuzi stahiki kuhusu ununuzi wake.

“Kampuni za mafuta ziko huru kuuza bidhaa za mafuta ya petroli kwa bei ya ushindani, mradi bei hizo ziwe chini ya bei kikomo kama ilivyokokotoa kulingana na kanuni ya kukokotoa bei za mafuta zilizochapishwa na Ewura na ambayo ilichapishwa na Gazeti la Serikali Namba 70/2016 la Februari mwaka jana,” alisema.

Alivitaka vituo vyote vya mafuta kuhakikisha vinabandika bei za bidhaa hiyo kwenye mabango bayana yakionesha bei, punguzo, vivutio vya biashara au promosheni zinazotolewa na kituo husika.

“Pale ambapo inawezekana kuchagua, wateja wanashauriwa kununua bidhaa za mafuta katika vituo vinavyouza mafuta kwa bei ndogo zaidi ili kushamirisha ushindani.

“Ni kosa kuuza mafuta bila mabango ya bei bayana kwa wateja, adhabu kali itatolewa kwa kituo husika kwa kutotekeleza matakwa ya kisheria kwa mujibu wa kanuni husika,” alisema.

Alitaka wanunuzi kuhakikisha wanapewa stakabadhi ya malipo zikionesha jina la kituo, tarehe, aina ya mafuta yaliyonunuliwa na bei kwa lita ambapo itatumika kama kidhibiti cha mnunuzi wa mafuta, endapo kutajitokeza malalamiko ya ama kuuziwa mafuta kwa bei ya juu kuliko bei kikomo au yenye kiwango cha ubora kisichofaa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo