Mauaji ya askari Rufiji yatikisa Bunge


*Kamati ya Ulinzi na Usalama yateta faragha na mawaziri

Joyce Kasiki, Dodoma

TUKIO la mauaji ya askari wanane lililotokea wiki iliyopita wilayani Kibiti mkoani Pwani, jana liliwalazimisha wabunge wakiongozwa na Spika Job Ndugai kutaka chombo hicho cha kutunga sheria kuahirisha shughuli zake siku hiyo ili wajadili mauaji hayo.

Walifikia uamuzi huo, baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu asubuhi.

"Mimi niungane na waheshimiwa wote mlioonyesha kuguswa sana na suala hili la askari wetu kuuawa na kufikia wanane, wakati mmoja kuuawa kwa kweli ni jambo linalosikitisha. Kwa hiyo kwa niaba ya Bunge zima ningependa kutoa pole na rambirambi kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini na kipekee kwa Waziri wa Mambo ya Ndani kwa jambo hili kubwa ambalo limetushtua wote katika nchi yetu." alisema Spika Ndugai akiunga mkono hoja za wabunge.

Awali, mbunge wa Bukombe Dotto Boteko (CCM) alisema Aprili 13 katika Kijiji cha Makengeni, Rufiji, askari wanane waliuawa na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi na kwamba askari hao walikufa wakati wakitekeleza majukumu ya kulinda raia na mali zao.

Alisema tukio hilo siyo la kwanza, huku akikumbusha tukio lingine lililotokea wilayani Kibiti mkoani Pwani Februari 21 mwaka huu ambapo watu watatu waliuawa, akiwemo mkuu wa upelelezi Wilaya ya Kibiti, Peter Kubeza.

"Kama askari hawapo salama kwa kiwango hiki, raia wa kawaida hali yao ikoje?| alihoji Biteko na kuongeza:

“Jambo hili limetokea Kibiti, lakini linaweza kutokea Kongwa, Bukombe hata mahali kwingine kokote na kama Taifa halijachukua hatua madhubuti ni hatari.

Naomba tuahirishe shughuli za Bunge tujadili jambo hili moja, ili Bunge kama chombo cha uwakilishi wa wananchi kije na kauli ya kuitaka Serikali kutoa kauli ya kueleza kwa nini mambo haya yanaendelea kujitokeza na Serikali wakati wote inatoa kauli lakini matukio hayo yanaendelea kujitokeza."

Mbunge wa Mtambile Masoud Abdallah Salim (CUF) aliomba busara ya Spika Ndugai itumike ili wabunge wajadili suala hilo ambalo limetia hofu kwa wananchi.

Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mollel (CCM) aliungana na wajumbe waliotangulia, huku akikazia kwa kunukuu Ibara ya 14 ya Katiba.

Akijibu miongozo hiyo, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba alisema Serikali inalichukulia tukio hilo kwa uzito mkubwa ili kuhakikisha wanarejesha hali ya usalama katika maeneo hayo na nchi nzima kwa jumla kama alivyoeleza Waziri Mkuu katika kauli yake aliyoitoa hivi karibuni.

Nchemba alitumia fursa hiyo kuwatoa hofu wananchi na kusema kuwa tukio hilo limewapa chachu zaidi ya kupambana na uhalifu katika kuhakikisha wananchi wanakuwa katika mazingira salama wao na mali zao.

Kamati ya ulinzi na usalama

Katika kuonyesha uzito wa tukio hilo, Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje ya Ulinzi na Usalama nayo jana ilipanga kukutana mchana baada ya kuahirishwa kwa shughuli za Bunge asubuhi.

Kikao hicho pia kilihusisha mawaziri wenye dhamana ili kupata taarifa rasmi kuhusu matukio hayo.

Ndugai alisema kamati hiyo itaeleza namna ilivyojipanga ili kuyakabili matukio mengine yanayoweza kujitokeza na kuhatarisha hali ya usalama ya polisi na mali zao .
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo