Nzigilwa akemea unyanyasaji kwa wasio na hatia


Mashaka Mgeta

Eusebius Nzigilwa
ASKOFU Msaidizi wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Eusebius Nzigilwa, ameonya dhidi ya vitendo viovu vinavyofanywa kwa wasio na hatia, lengo likiwa ni kulinda dhamana walizokabadhiwa ukiwamo uongozi.

Askofu Nzigilwa alisema hayo juzi alipohubiri katika adhimisho la Misa ya Pasaka, Wakristo nchini wanapoungana na wenzao duniani kukumbuka kufufuka kwa Bwana Yesu Kristo.

Alisema uovu dhidi ya watu wasio na hatia ulifanyika pia dhidi ya Bwana Yesu, alipotatufiwa ushahidi wa uongo, lakini licha ya kutofanikiwa, aliuawa na kufufuka siku ya tatu.

Kwa mujibu wa Askofu Nzigilwa, tukio hilo linaashiria ukweli usiobadilika kuhusu wema kushinda uovu, ikiwa ni moja ya mafundisho mengi yanayotokana na kuadhimisha sikukuu ya Pasaka.

Alisema mateso na kifo cha Bwana Yesu vilitokana na hofu ya makuhani na Wayahudi, kwamba kutokana na kazi alizofanya, alitishia kuwapo kwao kwenye madaraka ya kidunia, pasipo kujua kwamba utawala wake haukuwa wa duniani.

Askofu Nzigilwa alisema hata katika dunia ya sasa, wapo watawala wanaoundia hujuma watu wema, wakitaka kuwaangamiza ili kukidhi hofu zao na nia ya kulinda kuwapo kwao madarakani.

Kwa mujibu wa Askofu Nzigilwa, dunia haipaswi kuwa mahali mtu asiye na hatia anaangamizwa ili kulipa maslahi ya watu wengine na kwamba uovu kama huo unapofanyika hata kama ni katika kipindi cha mpito, lazima utashindwa.

Alisema ipo haja kwa watawala na wenye dhamana kutambua karama tofauti zilizo kwa watu, kwamba zinapotumika ipasavyo zinachangia ujenzi wa Taifa.

Pia alisema jamii inapaswa kuishi kwa upatanisho hasa inapotokea kutokuelewana kati ya watu wa pande mbili au zaidi.

“Kuna mtu anaweza kusema, mimi siwezi kumsaheme kabisa yule, kama Yesu aliteswa hadi kufa na akasamehe, wewe umetendwa nini kuliko yeye hata ushindwe kusamehe?” Alihoji.

Askofu Nzigilwa aliasa watu kujiepusha na hulka ya kufurahia mahangaiko ya binadamu wengine na kwamba kinachopaswa kufanyika ni kusaidiana ili kuondokana na kadhia zilizopo.

Kwa upande mwingine, alisema watu wanaokabiliwa na mahangaiko wanapaswa kutokata tamaa, bali kuwa na imani kwamba wakati utafika wa kupata matumaini mapya.

Alisema binadamu anapitia njia mbalimbali ikiwamo kuhangaika, kukumbwa na shida ingawa wakati mwingine hupata furaha.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo