Kubana matumizi kunaathiri uchumi


Suleiman Msuya

Benki Kuu ya Tanzania
SERA za Serikali ya Awamu ya Tano za kubana matumizi na kuongeza ukusanyaji wa mapato, zimeanza kuathiri ukuaji wa uchumi ambao unaonekana kushuka badala ya kupanda.

Ripoti ya Benki ya Dunia (WB), kuhusu hali ya uchumi nchini imeeleza kuwa katika robo ya tatu ya mwaka jana, uchumi ulishuka hadi kufika asilimia 6.2 kutoka asilimia 7.9 ya robo ya pili ya mwaka huo.

Waandaaji wa ripoti hiyo walipolinganisha ukuaji wa uchumi wa robo ya tatu ya mwaka jana na mwaka juzi walibaini kwamba uchumi umeshuka kutoka asilimia 7.3 hadi 6.2.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo taarifa zake zinaonesha kwamba mazingira ya ukuaji wa robo ya nne ya uchumi pia ni magumu.

Ripoti hiyo ilitaja sababu kubwa tatu kuwa ni kudhoofika kwa mazingira ya ufanyaji biashara, kupungua kasi ya utoaji mikopo na kupungua kwa kasi ya utekelezaji wa bajeti hasa katika miradi ya maendeleo.

Kutokana na hali hiyo ripoti inaonesha kuwa ukuaji wa uchumi wa mwaka jana unatarajiwa kuwa asilimia 6.9 pungufu ya matarajio ya Serikali ya ukauji wa asilimia 7.2.

Ripoti hiyo imeonya kuwa sera za Serikali tangu kuingia utawala wa Rais John Magufuli hasa katika kupunguza matumizi ya Serikali, ikitolea mfano katazo la semina za Serikali katika hoteli binafsi kwamba zinaharibu ukuaji wa sekta binafsi.

Katika hilo ripoti hiyo imefafanua kwamba sekta binafsi inategemea sana kuhudumia Serikali katika mahitaji ya huduma na bidhaa na kuonya kuwa sera za kupunguza mahitaji ya huduma na bidhaa serikalini zitapunguza kazi za sekta binafsi.

Pili imeonya kuwa sera hizo zikitekelezwa mara kwa mara zitatoa ishara ya hatari kwa sekta binafsi hali ambayo itasababisha uwekezaji katika sekta hiyo kukwama na hivyo kuathiri ukuaji wa uchumi kwa siku zijazo.

Aidha, ripoti hiyo imeonya Serikali kwamba iwe makini katika utekelezaji wa sera kuepuka matokeo hasi ya sera hizo katika sekta binafsi.

Akifafanua ripoti hiyo mmoja wa waandaaji kutoka WB, Abebe Adugna alisema katika kuhakikisha kuwa hali hiyo haitokei Serikali inapaswa kuhamasisha uwekezaji huku ikiweka mazingira rafiki na wawekezaji.

Alisema pia Serikali inapaswa kuangalia sekta mbalimbali kama ujenzi, usafirishaji, kilimo na huduma za jamii hasa katika rasilimali watu ili kuhakikisha kuwa inaweza kukabili changamoto za kiuchumi ambazo zinaweza kutokea.

“Kiujumla uchumi si mzuri katika nchi zote za Bara la Afrika kwani takwimu zinaonesha kuwa umeshuka hadi kufikia asilimia 1.5 ambayo haijawahi kutokea kwa miaka ya hi9vi karibuni,” alisema.

Umaskini wakithiri
Adugna alisema pia Serikali inapaswa kuongeza jitihada katika kusaidia familia maskini ambapo Tanzania inaonesha kuwa zaidi ya Watanzania milioni 12 wanaishi kipato cha chini ya dola moja kwa siku.

Mkurugenzi Mkazi wa WB katika nchi za Burundi, Tanzania, Malawi na Somalia, Bella Bird akizungumza kabla ya uzinduzi wa ripoti hiyo ya tisa ya hali ua uchumi nchini alisema uchumi wa Tanzania bado uko imara pamoja na kutoongezeka ikilinganishwa na nchi za Jangwa la Sahara na Afrika Mashariki.

Alisema ripoti hiyo ya tisa imejikita katika muktadha wa kuimarisha sekta ya fedha nchini ili kuamsha midahalo kutoka kwa wadau na wanafalsafa kuhusu uchumi wan chi.

Bird alisema wao kama WB wameangalia katika maeneo  mbalimbali ambapo alisisitiza kuwa uchumi wa Tanzania umeonesha ustahimilivu katikati ya ukuaji unaosuasua katika nchi za ukanda wa Afrika Kusini mwa Sahara.

“Uchumi wan chi hizi ulishuka hadi kufika asilimia 1.5 kiwango kibaya zaidi kuweza kutokea kwa zaidi ya miaka 20 na visababishi kutoka nje ndio sababu kubwa,” alisema.

Aidha, alisema wakati bei za biadhaa zikibaki kuwa chini, chumi nyingi zinazotegemea rasilimali zimehangaika kudhibiti matokeo ya mshituko wa biashara.

“Kinyume chake Tanzania imebaki moya ya chumi tatu katika Afrika ya Kusini mwa Sahara pamoja na Rwanda na Ethiopia ambazo zinaendelea kuonesha ustahimilivu katika mazingira yenye changamoto,” alisisitiza.

Mkurugenzi mkazi alisema nafasi ya Tanzania kiuchumi ipo imara huku akitahadharisha kuwa hakuna nafasi ya kubweteka ili kuweza kufikia asilimia 7 ya ukuaji au 10 ifikapo mwaka 2020/21 ili kufikia uchumi wa viwanda.

Bird alisisitiza kuwa kufikia viwango hivyo inawezekana iwapo idadi ya wananchi wanaishi chini ya mstari wa maskini itaondolewa na kuajiri zaidi ya vijana 800,000 ambao wanaingia katika soko la ajira.

Aidha alishauri Serikali kuendelea na sera makini ya uchumi, umuhimu wa uwekezaji wa umma na kuendeleza na kusisimua ukuaji wa siku zijazo na kutengeneza ajira kwa kufungulia uwezo wa sekta binafsi.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Ashatu Kijaji alisema ripoti inaonesha Tanzania inafanya vizuri na kuahidi kuongeza juhudi zaidi hasa katika kutekeleza miradi mbalimbali.

Alisema ripoti imeonesha changamoto kubwa ipo katika kupata fedha kutoka nje jambo ambalo anakiri kuwa lipo na kuwa wamejipanga kukabiliana na hali hiyo.

Kuhusu sekta binafsi kushuka alisema hayo ni mambo ambayo yanatokea katika Serikali mpya na kwamba wao wamejipanga kufanya kazi nao kwani bila wao ni vigumu kufukia Tanzania ya viwanda bila sekta hiyo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo