Ruzuku ya mil 460/= yatolewa kwa wachimbaji wadogo


Joyce Kasiki, Dodoma

Wachimbaji wadogo
SERIKALI imetoa ruzuku ya Sh milioni 460 kwa ajili ya uchimbaji wa madini mkoani Kigoma katika miradi saba ya uchimbaji mdogo wa chokaa na shaba inayomilikiwa na watu binafsi.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Medard Kalemani alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Josephine Genzabuke (CCM).

Genzabuke katika swali lake alitaka kujua Serikali imechukua hatua gani kuendeleza utafutaji na uchimbaji wa madini hasa ikizingatiwa kuwa mkoa huo una madini mbalimbali yakiwemo ya chokaa, dhahabu na platinum.

Akifafanua hatua hiyo ya Serikali, Kalemani alisema fedha hizo zilitolea   kipindi cha mwaka 2015 na kati ya miradi hiyo, mitano ni miradi ya chokaa na ipo katika wilaya za Uvinza, Kasulu na Kibondo.

Alisema Serikali imeendelea kutoa elimu ya uchimbaji salama, matumizi bora ya baruti, utunzaji wa madini na kuboresha mazingira, pamoja na elimu ya fursa ya biashara ikiwemo upatikanaji wa mikopo ya masharti nafuu.

Kwa sasa alisema Serikali  inaendelea kutoa huduma za ugani kwa wachimbaji wadogo wa madini na kuboresha mazingira ya uwekezaji katika sekta ya madini, ili uwekezaji huo uwanufaishe Watanzania na kukuza pato la Taifa.

Katika  swali la nyongeza Mbunge huyo alitaka kujua  kama Serikali inaweza kusaidia wananchi wa eneo la Kakere kijiji cha Kakonko, kuwa wachimbaji rasmi wa madini ya chokaa badala ya kuwazuia kuchimba madini hayo kama inavyofanyika hivi  sasa.

Pia alitaka kujua mpango wa Serikali wa kutenga eneo la wachimbaji wadogo wa chokaa ili kuepusha migogoro inayoweza kutokea baadaye.

Akijibu swali hilo, Kalemani alisema Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na Sheria ya Mazingira inasema mtu yeyote anaweza kumiliki eneo la uchimbaji na kwa kutekeleza hilo,  wapo wananchi wamepewa leseni za uchimbaji wa madini mbalimbali yakiwemo ya chokaa.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo