JPM asamehe wafungwa 2,219


Mwandishi Wetu

Rais John Magufuli
SAA chache baada ya kuhutubia Taifa katika maadhimisho ya miaka 53 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yaliyofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma, Rais John Magufuli ametangaza msamaha kwa wafungwa 2,219.

Kwa mujibu wa taarifa ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira, wafungwa watakaofaidika na msamaha huo ni waliotumikia nusu ya vifungo vyao, wagonjwa, wazee, walioingia na mimba au watoto gerezani na wenye matatizo ya akili.

Rais ametoa msamaha huo kwa mujibu wa Ibara ya 45 (1) (d) ya Katiba, jambo ambalo limekuwa likifanywa pia na marais waliomtangulia hasa katika sherehe ya Muungano na Uhuru.

Katika maelezo yake, Meja Jenerali Rwagasira alisema wagonjwa watakaoachwa ni wenye virusi vya Ukimwi, kifua kikuu na saratani ambao hali zao kiafya zimethibitishwa na mganga mkuu wa mkoa au wilaya.

“Wafungwa wazee wenye umri wa miaka 70 au zaidi.  Umri huo uthibitishwe na jopo la waganga chini ya uenyekiti wa mganga mkuu wa mkoa au wilaya,” alisema.

Alisema msahama huo hautahusu waliohukumiwa kunyongwa, maisha, kujihusisha na usafirishaji na matumizi ya dawa za kulevya, rushwa, unyang’anyi na kukutwa na silaha.

Wengine ni wenye makosa ya kubaka na kunajisi, kuwapa mimba wanafunzi wa shule za msingi na sekondari, wizi, kutumia vibaya madaraka, kuzuia watoto kusoma, utekaji watoto na biashara ya viungo vya binadamu na ujangili.

“Wanaotumikia kifungo kwa makosa ya wizi na ubadhirifu wa fedha za umma, kutoroka au kujaribu kutoroka chini ya ulinzi halali na wafungwa warejeaji wa makosa na wafungwa waliowahi kufungwa gerezani hawatasamehewa,” alisema.

Alisema ni matarajio ya Serikali kwamba baada ya kuachwa watarejea katika jamii kushirikiana na wenzao kujenga Taifa huku akiwaonya kutorudia makosa ili kuepuka kurejea kifungoni.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo