Shekhe aomba vita vya mihadarati viendelee


Hussein Ndubikile

Mussa Shabani
SHEKHE wa Mkoa wa Dodoma, Mussa Shabani, ameiomba Serikali kuendeleza vita dhidi ya dawa za kulevya ili kudhibiti mmomonyoko wa maadili katika jamii na upotevu wa nguvukazi ya Taifa.

Alitoa mwito huo akiwa Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa kongamano la mmomonyoko wa maadili na athari za dawa za kulevya lililoandaliwa na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Kupambana na Kudhibiti Dawa za Kulevya.

Alisema vita hivyo havipaswi kukoma na badala yake Serikali iwachukulie hatua za kisheria watakaoibainika kujihusisha na matumizi na biashara hiyo, huku akisisitiza viongozi wa dini kutoa mafundisho kwa waamini wao dhidi ya athari ya dawa hizo.

"Tuhakikishe kila mtu anakuwa mlinzi ndani ya familia na jirani zake tusiachie Serikali pekee, kwani vita hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu," alisema Shekhe Shabani.

Alisisitiza kuwa endapo jamii itashuhudia watu wanaotumia na kuendesha biashara ya dawa za kulevya wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria za nchi kasi ya vitendo hivyo viovu itapungua.

Aliongeza kuwa asilimia kubwa ya vijana ndio walioathiriwa na dawa hizo hali inayochangia mmonyoko wa maadili na kutaka wazazi kuwaangalia kwa umakini ili kuwaepusha wasijiingize kwenye utumiaji na uuzaji dawa hizo.

Mwenyekiti wa Halmashauri Kuu ya Bakwata Taifa, Shekhe Hamis Mataka alisema Baraza litaendelea na programu ya umuhimu wa kupambana na dawa hizo itakayoanzia ngazi ya Msikiti katani, wilayani hadi mkoani.

Shekhe Mataka alisema Bakwata itazindua kitabu kitakachoitwa Kiongozi kikiwa na mafundisho ya kujenga jamii kimaadili na kupambana na dawa za kulevya.



Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo