Wataka kesi ya kujifanya ofisa usalama iondoshwe


Wankyo Gati, Arusha

UPANDE  wa Jamhuri umeiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, kuiondoa kesi ya kujifanya Ofisa Usalama wa Taifa (TISS) na kujipatia chakula kwenye hoteli moja ya kimataifa jijini hapa, inayomkabili aliyekuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) wa Mkoa wa Arusha, Lengai ole Sabaya.

Akitoa maombi hayo juzi, Wakili wa Serikali Grace Madikenya mbele ya Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Gwantwa Mwakuga, alisema upande wa Jamuhuri hauna nia ya kuendelea na kesi hiyo kwa kuwa shahidi muhimu yuko nje ya nchi kwa miezi 18.

“Sasa tumeona tutamtesa mteja wetu, hivyo kwa nia njema kabisa tumeamua kuiondoa mahakamani kesi hii, maana miezi hii ni mwaka mmoja na miezi sita,” alisema.

Maombi hayo yalipingwa na wakili wa utetezi, Edna Haraka na kuiomba Mahakama iendelee na kesi hiyo, kwani upande wa mwendesha mashitaka unatumia Mahakama kama kichaka cha kumnyima haki mteja wao na kumnyanyasa.

Alidai kuwa upande huo hauna nia njema na mshitakiwa na kuiondoa kesi hiyo si mara ya kwanza, ni mara ya pili, mara ya kwanza waliomba hivyo na Mahakama ilipoifuta walimkamata mteja wao na kumnyima dhamana.

“Sasa leo tupo hapa kusikiliza shahidi wa tatu na badala ya kuleta shahidi wanaleta maelezo ya shahidi na stori ya kuiondoa ili waendelee kumnyanyasa mteja wetu, hapana ofisi ya Mwanasheria Mkuu inatumika vibaya kwa kivuli cha Mahakama,” alisema.

Edna alisema Serikali ya sasa inasisitiza mpango wa kuharakisha mashauri kusikiliza wa BRN, sasa wakati inafanyika hivyo wengine wanachelewesha kwa sababu zao.

Hakimu Mwakuga baada ya kusikiliza pande zote, alisema atatoa uamuzi Aprili 28.

Sabaya anakabiliwa na mashitaka ya kujifanya Ofisa Usalama wa Taifa na kujipatia huduma ya chakula na malazi kwenye hoteli ya kimataifa ya Highway jijini hapa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo