Dola inaihujumu CUF – Maalim Seif



 Asema uvumilivu sasa basi

Fidelis Butahe

Maalim Seif Sharif Hamad
KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Shariff Hamad ametaja hujuma tano zinazofanywa na dola kwa kushirikiana na Profesa Ibrahim Lipumba kukisambaratisha chama hicho na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), akasema uvumilivu sasa umefikia mwisho.

Maalim Seif aliyetumia dakika 80 kuzungumza na wanahabari amesema wana ushahidi wa hujuma hizo za makusudi na kwamba sasa litakalotokea anayestahili kulaumiwa ni watawala na vyombo vya dola.

Kiongozi huyo ambaye amekatiza ziara yake visiwani Zanzibar kwa kile alichokieleza kuja Dar es Salaam kuzungumza na vyombo vya habari kueleza hujuma hizo, mbali na kuzitaja alisema hawezi kufanya kazi na Profesa Lipumba kwa kuwa si mwanachama wa CUF.

“Nawaambia watawala walio nyuma ya hujuma hizi chafu dhidi ya CUF, msitulazimishe kutusukuma kwenye ukuta. Tumevumilia kiasi cha kutosha sasa basi, mlio nyuma ya hujuma hizi mtabeba dhamana ya mnayoyaandaa,” alisema na kubainisha kuwa  atafanya ziara Dar es Salaam siku za hivi karibuni.

Katika hotuba yake ya dakika 80, Maalim Seif akiwa  sambamba na viongozi wakuu wa CUF, alitoa wito kwa Watanzania wapenda demokrasia kusimama imara kulinda haki huku akiania mkakati mpya wa sita unaofanywa na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (Rita) kusajili bodi feki ya wadhamini ya chama hicho kufanikisha njama ovu.

Alibainisha kuwa amepigania haki Zanzibar kwa muda mrefu huku akilindwa na Mungu lakini siku zote waliompangia njama wameondoka wao na kumuacha.

Alitaja Jeshi la Polisi, Hazina na Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa vinara wa hujuma hizo kutokana na kuendeleza mikakati yao kwa kumtumia Profesa Lipumba, mwenyekiti wa CUF anayetambulika Ofisi ya Msajili wa vyama vya Siasa.

Alisema zama za watawala kuwanyamazisha Watanzania na kutaka matakwa ya mtu mmoja tu ndio yasimame, zimeshapita na hazirudi tena.

“Huu ni wakati wa wapenda demokrasia na amani nchini kusimama pamoja kulinda demokrasia yetu na kuzilinda taasisi zetu zinazosimamia demokrasia yetu,” alisema.

“Kinachotafutwa hapa sio CUF. Kinachotafutwa hapa ni kuua taasisi zetu zinazosimamia demokrasia. Tukiruhusu kufanikiwa katika hili, hatutaweza kuzuia mengine. Tusiposimama pamoja tutamalizwa mmoja mmoja tusitoa mwanya huo.”

CUF kiliingia katika mgogoro baada ya Profesa Lipumba ambaye alijiuzulu wadhifa wake kuandika barua ya kutaka kurejea jambo ambalo lilizua mgogoro na kusababishwa kufukuzwa uanachama lakini Ofisi ya Msajili iliibuka na kueleza kuwa inamtambua kama mwenyekiti.

Kufuatia hali hiyo, CUF kupitia kwa Baraza lake la Wadhamini walifungua kesi mahakamani kupinga uamuzi huo, huku Profesa Lipumba ofisini na kukifanya chama hicho kuwa na taswira mbili tofauti za uongozi.

Hujuma tano

Akizitaja hujuma hizo,  Maalim Seif alisema ya kwanza ni kutumika kwa vyombo vya dola kumzuia kufanya shughuli zake Tanzania Bara huku vyombo hivyo hivyo vikimlinda kwa nguvu Profesa Lipumba.

“Pili, kwa kutumia dola Profesa Lipumba ameteka na kuvamia kwa nguvu ofisi za chama za wilaya mbalimbali nchini  chini ya ulinzi wa dola. Tatu, ni wizi wa fedha za ruzuku Sh milioni 369 uliofanywa kwa ushirikiano kati ya Lipumba, msajili, hazina na benki,” alisema.

Alidai hujuma aya nne ni njama za kujaribu kumuengua katika nafasi yake ya ukatibu mkuu huku ya tano ikiwa ni Bunge kuridhia kupokea wagombea feki wa Bunge la Afrika Mashariki ambao walishafukuzwa uanachama wa CUF.

Rita yatajwa kuhusika

Alisema tangu zilipoanza njama za kukihujumu CUF, kikwazo kinachowakwamisha vyombo hivyo kufanikiwa ni Bodi ya Wadhamini ya chama hicho ambayo imechukua hatua za kukilinda chama kupitia mahakama.

“Tuna taarifa zisizo na shaka. Kuna shinikizo la kumtaka Ofisa Mtendaji Mkuu wa Rita kusajili wajumbe feki wa bodi ya wadhamini ya CUF kwa kutumia majina yaliyowasilishwa na Lipumba ili kutimiza malengo yao matano,” alisema Maalim Seif.

Aliyataja malengo hayo kuwa ni kuitumia bodi hiyo feki kufuta kesi zote zinazomkabili mwenyekiti huyo, Msajili wa Vyama vya Siasa, kufungua akaunti mpya ya Benki ili kuwezesha kupatikana fedha za ruzuku, kumuondoa katibu Mkuu kwenye wadhifa wake na bodi hiyo kudhibiti Ofisi za Makao Makuu ya CUF zilizopo Mtendani, Zanzibar.

“Wanataka kuhujumu majina halali yaliyowasilishwa na kikao halali cha Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la chama kilichofanyika makao makuu visiwani Zanzibar Machi 19, mwaka huu,” alisema.

Alisema bodi ya Wadhamini cha chama hicho ilishasajiliwa tangu mwaka 1993 kwa kuzingatia Sheria ya Wadhamini na kwamba kinachofanyika kila baada ya kipindi fulani ni kuweka kumbukumbu za bodi hiyo.

Alisema CUF kimefanya mabadiliko machache ya baraza hilo na kuyawasilisha RITA lakini Profesa Lipumba ametakiwa kuandaa majina yake na kuyafikisha katika ofisi za wakala huyo kwa malengo matatu.

Alisema kwa kutumia njama hizo watawala wanadhani watakuwa wamekidhibiti CUF na kwamba watakuwa wamezima hoja za chama hicho kupokwa ushindi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

“Tunajua Msajili wa Vyama anaishawishi Rita kukubali uhuni huu. Anaonekana ana maslahi binafsi katika hili. tunasubiri uamuzi wa Rita ili tuone kama nao wanatumika,” alisema.

Uvumilivu basi

Kuhusu kuvumilia kwa muda mrefu hujuma na njama hizo alisema, “kama Rita watamtambua Lipumba litakalotokea watawala watabeba dhamana. Siwezi kusema zaidi ya hapo.”

“Tumekuwa wapole na waungwana maana hii nchi ya amani. Tungetaka machafuko nchi hii yangeshatokea tangu zamani. Wasijisifu, si vyombo vya dola vinavyotunza amani ni CUF…, watu wakidhamiria kufikia malengo yao utaua watanzania wote, utaua wachache tu.”

Alisema hata akikamatwa sambamba na viongozi wengine wa chama hicho, wapo wanachama wengine wataendeleza mapambano ya kudai haki, demokrasia na utawala wa sheria.

“Wapo wanaosema kuwa nawachelewesha ila siku zote nimekuwa nikizuia jambo hili nikitegemea upande wa pili utaliona hili. Kama watatufikisha tukabanwa na ukuta litakalotokea watajibu wao,” alisema.

Alisema ikiwa Lipumba atachukua ofisi za CUF Zanzibar, hawezi kuwazuia vijana kupambana ili jambo hilo lisitokee.

Amjibu Lipumba

Alisema licha ya kufukuzwa Profesa Lipumba amendelea kujiita mwanachama wa CUF sambamba na kuchukua majukumu kadhaa yasiyomhusu ikiwa ni pamoja na kufukuza wanachama, kuunda mabaraza ya maamuzi na kutumia fedha za chama.

“Siwezi kukaa na Lipumba kwani sio mwanachama na uamuzi wa kumfukuza ushafanywa na vikao siwezi kuingilia” alisema.

“Profesa Lipumba anasema eti nashindwa kufanya kazi zangu ataniondoa ajabu hii! Lini nimeshindwa kufanya kazi. Lini mwenyekiti akampangia kazi Katibu Mkuu?”

Alisema hata kama Profesa Lipumba angekuwa mwenyekiti halali hampi madaraka na kuchukua uamuzi kama anaoufanya sasa.

Njama ovu 10

Katika mkutano huo na wanahabari, Maalim Seif alitaja mbinu 10 ovu zinazofanyika tangu Serikali ya Awamu ta Tano kuingia madarakani.

Alizitaja mbinu hizo kuwa ni kupiga marufuku mikutano ya kisiasa, kuzuia matangazo ya moja kwa moja ya Bunge, kuminya bajeti ya Bunge, kuwakamata na kuwafungulia mashataka wabunge, kuzipa mahakama maagizo.

Nyingine ni kuwakamata watumiaji wa mitandao ya kijamii na kuwafungulia mashtaka, kuwatisha wanahabari, kuwatisha na kuwakamata wasanii, kuzitisha jumuiya za kiraia na wakuu wa mikoa na wilaya kujipa mamlaka kinyume na sheria.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo