JPM aweka mpinzani mwingine serikalini


*Ni Katibu Mkuu Wizara ya Maji akitokea ACT-Wazalendo
*Akiuka kauli yake Zanzibar mwaka jana kuhusu wapinzani

Mwandishi Wetu

Profesa Kitila Mkumbo
AMEJIRUDI. Ndivyo kitendo cha Rais John Magufuli kumteua Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, Profesa Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji kinavyoweza kutafsiriwa.

Profesa Kitila aliteuliwa jana kuchukua nafasi ya Mbogo Futakamba anayestaafu.

Tafsiri kwamba Rais Magufuli amejirudi inaweza kutumika kwenye tukio hilo kwa kurejea kauli aliyopata kuitoa akiwa Zanzibar kwenye ziara ya kushukuru wananchi wa kisiwa hicho baada ya Uchaguzi Mkuu, aliposema hakuna mpinzani atakanyaga ukuu katika Serikali yake.

Rais Magufuli alisema anamshangaa Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kwamba pamoja na kushinda uchaguzi kwa asilimia 92, ameweka wapinzani kwenye Serikali yake, lakini yeye hawezi kufanya hivyo.

“Kusema ukweli anayoyafanya Rais Shein yanaonesha ana moyo wa ajabu sana, mimi siwezi kuruhusu mpinzani akanyage katika Serikali yangu,” alisema.

Lakini jana, taarifa kutoka Ikulu ilibainisha kuwa Rais Magufuli amemteua Profesa Mkumbo kushika wadhifa huo akitokea Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Profesa Mkumbo anakuwa mpinzani wa pili kupewa wadhifa ndani ya Serikali ya Magufuli, wa kwanza akiwa Dk Augustino Mrema aliyeteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Parole. Mrema ni Mwenyekiti wa TLP.

Katika uteuzi wa jana wengine walioteuliwa ni Dk Leonard Akwilapo ambaye amekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kabla ya uteuzi huo alikuwa Naibu Katibu Mkuu katika Wizara hiyo.

Kutokana na uteuzi huo, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Maimuna Tarishi anahamishiwa kuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge) kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Mussa Uledi ambaye uteuzi wake umetenguliwa.

Aidha, Rais Magufuli alimteua Dk Ave Maria Semakafu kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu kuchukua nafasi ya Dk Akwilapo, kabla ya uteuzi huo Sekamafu alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Shirikishi cha Afya na Sayansi cha Muhimbili (MUHAS).

Kwa mujibu ya taarifa ya iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa wateule hao watakula kiapo mbele ya Rais leo Ikulu Dar es Salaam kuanzia saa tatu asubuhi.

Profesa Mkumbo

Akizungumza na JAMBOLEO baada ya uteuzi huo, Profesa Mkumbo alisema amepokea kwa mikono miwili uteuzi huo na kuahidi kufanya kazi na Rais Magufuli kwa moyo mmoja.

Alisema ni kweli yeye ni mpinzani, lakini amekuwa akifanya kazi UDSM kama mtumishi wa umma, hivyo kitakachopungua kwa sasa ni kuachana na siasa ili kusimamia wizara husika.

“Nimepokea uteuzi huu kwa moyo mmoja na naahidi kufanya kazi kwa nguvu zote kama nilivyokuwa hapa UDSM, ila siasa itabidi nikae pembeni kwa sasa,” alisema.

Aidha, alipoulizwa kuwa uteuzi huo aliujua au aliusikia baada ya kutangazwa na Ikulu, alisema hayo ni mambo ya ndani na hawezi kuyazungumza huku akisisitiza kuwa amepokea nafasi hiyo na atafanya kazi bila tatizo.

Kuhusu kauli yake ya Aprili mwaka jana kuwa Rais asiteue wahadhiri wa vyuo vikuu kushika nafasi za utendaji ili kuwapa nafasi ya kufanya utafiti na kutoa taaluma, alisema ni kweli hajabadilika ila hana budi kupokea uteuzi huo.

“Huu utaratibu wa kuteua wasomi tu ambao ni walimu na wanataaluma kutoka vyuo vikuu hasa UDSM, si mzuri maana Rais haoneshi kuandaa wengine kuchukua nafasi zao, tuachwe wasomi tufanye kazi za kitafiti na kitaaluma,” sehemu ya maneno ya Mkumbo Aprili 17, mwaka jana.

Pamoja na uteuzi huo kuhusu watu wengi Profesa Mkumbo ndiye aliibua mijadala katika mitandao ya kijamii ambapo watu walijikuta wakijadili na wengine kutoamini kuwa amepewa nafasi hiyo.

Mmoja wa watu ambao walituma ujumbe kwenye mitandao ya kijamii ni Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ambaye alisema Mkumbo hakujua uteuzi huo kabla.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo