Kabudi akonga nyoyo Sheria ya Ndoa


Mwandishi Wetu, Dodoma

Profesa Palamagamba Kabudi
WAZIRI wa Sheria na Katiba, Profesa Palamagamba Kabudi, jana aligeuka kivutio na kuzua mjadala kuhusu Sheria ya Ndoa inayoruhusu wasichana wenye umri wa miaka 14 kuolewa na wavulana kuoa.

Waziri huyo alivuta hisia za wabunge wakati wa kipindi cha Maswali na Majibu Bungeni wakati akijibu maswali ya wabunge kuhusu sheria hiyo ambayo ilipingwa mahakamani na Serikali kwa swali la msingi lililoulizwa na Mbunge wa Songwe, Philip Murugo (CCM).

Profesa Kabudi alijibu swali hilo kwa kutumia mifano ya makabila likiwamo analotoka yeye akisema haiwezekani kubadili mila na desturi, imani ya dini na itikadi kwa sheria peke yake.

“Ni kweli ipo sheria ya ndoa mchakato wake unaendelea, niseme leo kuna jambo ambalo haliko sahihi kwenye hiyo sheria, inaruhusu mtoto wa kike kuolewa na umri wa miaka 14 na mtoto wa kiume kuoa akiwa na umri wa miaka 14. Kifungu kile mwaka 1971 kiliwekwa ili kukidhi matakwa ya jamii mbili, Wamasai na Mabohora,” alisema Kabudi na kuongeza:

“Ikifika wakati hali imebadilika umuhimu upo tutalijadili. Umri wa miaka 14 si kwa msichana tu hata mvulana anaruhusiwa kuoa kama Mahakama imeruhusu.

“Nami nakubali umri huo mvulana hajafika kuoa na msichana kuolewa. Jambo hili linataka mwafaka wa kijamii kama ambavyo mwaka 1970 ilikuwa ni muhimu kuwaangalia Wamasai na Mabohora ambao ni sehemu ya Tanzania. Lakini maadam mchakato unaendelea, inshallah siku itafika na jambo hilo litapita.

“Mambo ya mila, desturi na itikadi hayataki haraka, yanataka mwafaka. Kuna umuhimu sasa wa vyuo vyetu kufundisha ‘Legal Anthropology’, huwezi kubadili mila, desturi imani ya dini na itikadi kwa kutumia sheria peke yake, utakuwa unajidanganya,” alisema Kabudi na kufafanua:

“Mimi natoka kwenye kabila ambalo lina mila isiyo nzuri ya ukeketaji. Sheria ipo, imezuia lakini kwa sababu bado ni suala la imani na itikadi za watu, leo wamelihamishia kwa watoto wachanga.”

Alifafanua: “Sasa nazungumza kama Profesa wa Sheria, ni hatari na Waitara Chacha anajua kuna mila na desturi za anakotoka leo, mimi siafikiani nazo, lakini zinahitaji elimu, zinahitaji uelewa. Ni vigumu mtu anayetoka nje ya eneo hilo kuelewa, kwamba mapenzi ni pamoja na kipigo.”

Kauli hiyo ya Kabudi ilimwinua Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara (Chadema) kuomba kutoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Bunge, lakini Mwenyekiti Mussa Zungu alimnyima nafasi huku Waziri huyo akiomba wakitoka wakazungumze zaidi.

Mbunge huyo ni mmoja wa waliouliza maswali ya nyongeza baada ya swali la msingi la Murugo.  

Awali akijibu swali la msingi, Kabudi alisema kazi ya kurekebisha sheria ni endelevu, ili kuhakikisha sheria zinaendana na mabadiliko yanayotokea katika jamii.

Profesa Kabudi alisema: “Sheria za nchi hubadilika kulingana na mabadiliko ya kijamii, kiuchumi, kisiasa, kitamaduni, kisayansi na kiteknolojia, jambo ambalo haliwezi kuathiri sheria zilizopo na kusababisha zipitwe.”

Alisema katika kukabiliana na hali hiyo, Serikali iliunda Tume ya Kurekebisha Sheria ambayo ni chombo maalumu, chenye dhamana ya kufanyia mapitio sheria zilizopo, ili kukidhi malengo na makusudio ya kutungwa kwake.

“Serikali imekuwa ikiwasilisha miswada ya sheria bungeni ili Taifa libaki na sheria zinazochochea ukuaji wa uchumi, uboreshaji wa huduma na ustawi wa jamii,” alieleza.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo