Bashe afichua mpango wa kuteka wabunge 11


*Asema yeye ni mmoja wa walio kwenye orodha
*Abainisha kudokezwa na baadhi ya mawaziri

Sharifa Marira, Dodoma

Hussein Bashe
WAKATI matukio ya uvamizi na watu maarufu kutekwa yakiendelea kutikisa Taifa, Mbunge wa Nzega, Hussein Bashe (CCM) amezua takaruki bungeni baada ya kufichua kuwepo mpango wa yeye na wabunge wengine 10 kutekwa.

Amesema taarifa hizo amepewa na baadhi ya mawaziri, wakimhadharisha kuwa makini, kwa maelezo kwamba yeye na wenzake wanaweza hata kupoteza maisha kwa sababu tayari wameingizwa kwenye orodha.

Mbunge huyo kijana anayesifika kwa tabia yake ya kuikosoa Serikali, bila woga alitoa kauli hiyo jana baada ya kuomba Mwongozo wa Kiti cha Spika, akitaka kikao cha jana cha Bunge la Bajeti kiahirishwe ili kujadili matukio ya utekaji nchini.

Katika maelezo yake huku akitumia Kanuni ya 47 ya Bunge, Bashe alisema: “Zipo taarifa binafsi nimezipokea kutoka kwa baadhi ya mawaziri wakinihadharisha.

“Wamenitaka niwe makini, kwa sababu ni miongoni mwa wabunge 11 ambao wamewekwa katika orodha. Nimeelezwa nikikaa barabarani vibaya tunaweza hata kupoteza maisha.”

Aliongeza: “Kikundi hiki (cha utekaji) kilicho ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa ambacho kimeamua kuchukua mamlaka haya ya kuteka watu, kinaharibu heshima ya Serikali yetu na chama changu ambacho mimi na wabunge wenzangu tuliomba ridhaa ya kuongoza Watanzania na si kuwahatarishia maisha.”

Hata hivyo, Mwongozo alioomba mbunge huyo uliofanana na wa Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbililinyi ‘Mr Sugu’ (Chadema), ulipingwa na Naibu Spika, Dk Tulia Ackson kwa maelezo kuwa si jambo la dharura na litatatuliwa na mamlaka zilizopo.

Bashe alitoa kauli hiyo kukiwa na kumbukumbu ya kupotea kwa Mkuu wa Idara ya Sera na Utafiti wa Chadema, Ben Saanane tangu Agosti 8 mwaka jana na tukio la siku nne zilizopita, la kutekwa na kuachwa kwa msanii wa muziki wa kizazi kipya, Musa Ibrahim ‘Roma Mkatoliki’ na wenzake wanne.

Wakati Bashe akieleza kuwapo Watanzania wengi wanaotekwa lakini kwa kuwa si maarufu, utekaji wao haujulikani, Mbilinyi alimtaka Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba kujiuzulu kwa kushindwa kudhibiti matukio hayo.

Ilivyokuwa

Baada ya kipindi cha maswali na majibu jana asubuhi, wabunge wengi walisimama kwa nia ya kuomba Mwongozo, ndipo Dk Tulia alipompa nafasi Bashe.

Katika Mwongozo wake, Mbunge huyo alieleza kuwa matukio ya utekaji yamekuwa yakitokea mfululizo bila hatua stahiki kuchukuliwa.

“Kumekuwa na matukio ya sintofahamu nchini, si tu kwa wabunge ila hata raia. Kuna kikundi kinateka watu na miongoni mwa waliowahi kutekwa ni Msukuma (Joseph -Mbunge wa Geita Mjini-CCM), mimi mwenyewe na Malima (Adam-aliyekuwa Mbunge wa Mkuranga-CCM) wakati wa mkutano mkuu wa CCM,” alisema Bashe.

Huku akihoji kupotea kwa Saanane ambaye alikuwa msaidizi wa mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Roma, alisema hao ni wanaojulikana, lakini wapo Watanzania wengine wanaotekwa.

Katika Mwongozo wake, Bashe aliomba Kiti cha Spika kuridhia kujadili jambo hilo na kuunda kamati maalumu ya kuchunguza utekaji na ikishindikana jukumu hilo lipelekwe kwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, kufanya uchunguzi na kutoa taarifa kwa ajili ya usalama wa wananchi.

“Hali ya nchi si salama, Watanzania wana taharuki na wanajadili mambo haya katika mitandao ya kijamii kila kukicha, lakini hakuna kauli ya matumaini kutoka serikalini. Waziri wa Mambo ya Ndani yuko wapi?’’ Alihoji Bashe.

Mbilinyi katika Mwongozo wake, alisema Taifa ni kama liko gizani kutokana na utaratibu mpya uliozuka kwa kuteka watu aliodai kuwa ni mpya nchini.

“Utamaduni huu kwa mara ya mwisho ulitokea Zanzibar alipotekwa Kassim Hanga, lakini tangu operesheni hii ya kukamata watu ianze, kila anayehusika na usalama wa nchi, likiwamo Jeshi la Polisi wakiulizwa wanasema hawana taarifa,” alisema Mbilinyi akiongeza:

“Amepotea Saanane, Roma na wengine, kuna miili ya watu iliokotwa Mto Ruvu lakini viongozi wako kimya.”

Huku akimtaka Mwigulu kujiuzulu kama anaona hashirikishwi katika mambo yanayoendelea nchini, Mbilinyi alisema haiwezekani Waziri kukaa kimya na kutoa tafsiri kuwa amefumbwa midomo.

“Najiuliza kama anabanwa kwa kiasi hicho huyu ni mtu potential (mwenye uwezo) aligombea hata urais, ana miaka mingi ya kuwa kiongozi. Kwa nini asijiuzulu alinde heshima yake kuliko kukaa kimya?” Alihoji.

Mbilinyi alisema hata Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, alijiuzulu, lakini baadaye akawa Rais.

Alisema Roma alipatikana siku chache baada ya kiongozi mmoja wa Serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam kutamka wazi kuwa msanii huyo atapatikana kabla ya Jumapili ya Aprili 4.

“Mtu aliyesema anamrudisha Roma, tumlazimishe, maana tunajua anafahamu mambo haya, hivyo atueleze aliko Saanane na ile miili sita ilikuwa ya watu gani,” alisisitiza.

Licha ya miongozo hiyo kuonekana kuliteka Bunge, Dk Tulia alisema kwa mujibu wa kanuni ya 47 ambayo husomwa pamoja na ya 48, ili kuweka masharti ya matumizi ya kanuni ya 48 (4), inaeleza jambo lolote litahesabiwa kuwa la maslahi kwa umma, iwapo utatuzi wake utategemea hatua zaidi kuliko utekelezaji wa kawaida wa sheria peke yake.

"Miongozo iliyotolewa na Bashe na Mbilinyi itatatuliwa na taratibu za kawaida za sharia, hivyo sihesabu kama jambo la dharura kama lilivyowasilishwa,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo