Utata waibuka mchanga wa dhahabu


Suleiman Msuya

Makontena yenye mchanga wa dhahabu
WAKATI Rais John Magufuli akiunda ya kuchunguza taarifa za makinika ya dhahabu kutoka migodini kama una asilimia 90 ya madini hayo, wataalamu wamebainisha kwamba kiwango hicho kikithibitishwa, Tanzania itakuwa imevunja rekodi ya kuzalisha tani 4,000 kwa mwaka, kiasi ambacho hakijawahi kutokea tangu dunia iumbwe.

Aidha, wamesema ili kujenga kiwanda cha kuchenjua dhahabu nchini takriban megawati 500 za umeme wa uhakika zinahitajika kwa kiwanda kimoja jambo Tanzania haiwezi kulifanikisha kwa nishati iliyopo.

Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya Rais kuunda tume hiyo kuchunguza mchanga kwenye kontena 282 alizobaini alipotembelea bandari ya Dar es Salaam hivi karibuni zikiwa katika mchakato wa kusafirishwa.

Akizungumza katika kipindi cha Mizani ya Wiki kinachorushwa na kituo cha Televisheni cha Azam,  Meneja Mkuu wa Uhusiano wa Serikali wa kampuni ya Accacia, Assah Mwaipopo alisema Serikali ina haki ya kuhakiki, lakini haiwezi kutokea yanayosemwa yakawa kweli.

Mwaipopo alisema katika historia, inaonesha kuwa nchi inayozalisha dhahabu kwa wingi duniani ni Afrika Kusini ambayo inazalisha tani 600 hadi 400 na kiwango cha dunia kwa takwimu za mwaka 2015 ni tani 2,500 tu hadi sasa.

Alisema wanaosema kuwa mchanga huo una dhahabu asilimia 90 wanatoa tafsiri potofu na kubainisha kuwa hata miche ambayo wanavuna katika hatua ya kwanza dhahabu si asilimia 90.

Meneja huyo alisema ni vigumu kutorosha dhahabu hasa kampuni ya Accacia ambayo imesajiliwa katika Soko la Hisa la London, Uingereza na kusisitiza kuwa taarifa hiyo itaondoa utata.

“Mfano ukisema kontena moja lina asilimia 90 ya dhahabu ni kwamba kuna tani 18 za dhahabu katika kontena la tani 20; ni vigumu kwani kwa kontena 260 zilizo bandarini  unataka kuiambia dunia bandari ya Dar es Salaam ina tani 4,000, ni taarifa ya kushitua dunia,

“Haijatokea kwa mwaka mmoja dunia ikavuna tani 3,000, kwani nyingi sana ni 2,500 hivyo taarifa zinazosemwa si sahihi ila ngoja Serikali ijiridhishe,” alisema.

Mchakato

Mwaipopo alisema mchakato wa kuchimba dhahabu una hatua muhimu ambazo zinahitajika ili kupatikana dhahabu ambapo katika hatua ya kwanza dhahabu huwa kubwa.

Alisema katika hatua ya pili kemikali zinazovuta dhahabu hutumika ili madini hayo kutenganishwa.

Alisema uchenjuaji unahusu tani moja ya makinikia ili kupata gramu mbili, hivyo haiwezi kuwa kama inavyosemwa kwamba asilimia 90 ya mchanga huo ni dhahabu.

Mwaipopo alisema pia hutumia kemikali ya carbon kupata dhahabu kabla ya kufikia makapi ila kama ingewezekana wangeishia kwenye makinikia.

Alisema kemikali ya synite ni aghali na baada ya matumizi inapaswa kuharibiwa hivyo ni ngumu kuiingiza nchini.

“Katika kuchenjua tunapata gramu 0.02 ambayo inatoka kwenye tani moja kwani yale ni makapi tunayaita dhahabu athari,” alisema.

Alisema kibiashara ingekuwa heri mchakato wa dhahabu kuishia kwenye makinikia ila gramu 150 kwa tani na ukiibadilisha tani iwe gramu utapata gramu 0.02 kwenye wastani wa tani moja.

Mhandisi huyo alisema katika mgodi wa Buzwagi wanapata tani 18 za shaba ambapo kwa gharama ya soko haina tija kubwa.

Kuhusu gharama za kusafirishia, alisema si kubwa sana kwani kontena moja linasafirishwa kwa dola 2,000 za Marekani na kuchenjua haizidi dola 1,000 hivyo tani 3.6 itakayopatikana itarejesha gharama na faida.

Mahitaji

Akifafanua kuhusu kiwanda cha kuchenjua dhahabu nchini alisema kiuhalisia kiwanda hicho kinahitaji uwekezaji wa muda mrefu ambao utazingatia ukweli kuhusu makinikia yaliyopo.

Alisema uwezo wa migodi iliyopo nchini ni kuzalisha makinikia tani zaidi 50,000 na kuwa ili kiwanda kifanye kazi yanahitajika makinikia tani 150,000 kwa mwaka.

Mwaipopo alisema pia kiwanda kimoja kitahitaji umeme wa megawati 500 hivyo kwa Tanzania ni vigumu kupata umeme huo kwani uliopo ni wa megawati 2,000.

“Kama yupo mwekezaji anayetaka kuwekeza anakaribishwa, lakini ni vema akahakikishiwa uendelevu wa uwekezaji wake kwani kiwanda kinachofanya kazi hiyo ya kuchenjua makinikia kina thamani ya zaidi ya dola milioni 500,” alisema.

Alisema mgodi wa Buzwagi umeanza kwisha hivyo utakaobaki ni Bulyanhulu jambo ambalo linaweka bayana kuwa makinikia yatakuwa tani 30,000 kwa siku zijazo.

Mtaalamu  

Dk Elisante Mshiu alisema dhahabu ni dhahabu wakati unatumia ila kijiolojia inapatikana kwenye ukanda wa miamba.

Alisema Tanzania ina kanda sita ila kanda ya Ziwa Victoria zipo kanda nane mbili zikiwa Kenya.

Mshiu alisema nchini kanda maarufu ya dhahabu ni Sukuma Land   ambayo inahusu Buzwagi, Bulyanhulu na Geita.

Dk Mshiu alisema hoja ya Serikali kutaka mtambo wa kujengwa nchini ni lazima wataalamu washirikishwe ili kuuhakikishia umma kuwa makinikia yatakuwapo ya kutosha.

Kuhusu kontena za tani 20 bandarini kuwa na dhahabu asilimia 90 alisema ni kitu ambacho hakiwezekani kwani kwa uzito wa dhahabu hiyo magari yasingetembea.

“Yote yanayofanywa yanafaa kupewa nafasi ila kiuhalisia haiwezekani kontena la tani 20 likawa na asilimia 90 kwa uzito wa dhahabu gari haliwezi kutembea,” alisema.

Kamati iliyoundwa na Rais inaongozwa na Profesa Abdulkarim Mruma na wengine ni Profesa Justinian Rwezaura,  Profesa Joseph Buchweishaija, Dk Yusuf Ngenya, Dk Joseph Yoweza, Dk Ambrose Itika, Mohamed Makongoro na Hery Gombela.

Aidha, Bunge kupitia Spika Job Ndugai litaunda tume ya kibunge kuchunguza sakata hilo la mchanga wa dhahabu.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo