Tume yathibitisha faru John amekufa kizembe


Suleiman Msuya
Kassim Majaliwa

IKIWA takribani miezi mitatu baada ya kuibuka kwa sakata la kupotea faru aliyebatizwa jina la John, Tume ya Uchunguzi iliyoundwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, imethibitisha kuwa faru huyo alikufa.

Aidha, Tume hiyo imependekeza kwa Serikali kuwachukulia hatua waliohusika kumhamisha faru John bila kufuata utaratibu hali ambayo ilisababisha kifo chake.

Akiwasilisha matokeo ya Tume hiyo ya uchunguzi, Mwenyekiti wake, Profesa Samwel Manyele ambaye ni Mkemia Mkuu wa Serikali alithibitisha kuwa John amekufa, baada ya sampuli 45 kuthibitisha bila shaka.

Alisema kupitia wataalamu walioshiriki kazi hiyo, Afrika Kusini matokeo yanaonesha sampuli na vielelezo vyote ni vya mnyama huyo.

“Mzoga, fuvu, pembe (zote tatu) damu, zote ni za Faru John, zilichukuliwa wakati wa kumwekea kifaa maalumu cha kutambua aliko,” alisema.

Alisema jumla ya sampuli za vielelezo 45 zilitumika na kuonesha kuwa ni Faru John ambaye alikuwa dume mweusi, hata pembe ambazo ziliwasilishwa kwa Waziri Mkuu ni za kwake.

Alisema faru huyo alifia Sasakwa Grumeti ambapo alikuwa amehifadhiwa, huku kukiwa na upungufu mwingi uliotajwa kusababisha kifo chake.

 Sababu

Mwenyekiti huyo ambaye alisema John alikufa kutokana na kukosa matunzo, uangalizi wa karibu na matibabu alipougua, pia kutofuata taratibu zilizowekwa kisheria ukiwamo upungufu wa kiuongozi kwa wizara, hifadhi hata taasisi zake.

Alisema katika uchunguzi wao, walibaini upungufu mbalimbali ikiwa ni pamoja kukosekana kibali rasmi cha kumhamisha John pamoja na kuonesha kuwa mchakato uliridhiwa na Wizara.

“Hapakuwa na kibali rasmi kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori cha kuruhusu kumhamisha Faru John kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) kwenda Grumeti,” alisema.

Alisema Tume inashauri taratibu za kuhamisha wanyama walio katika hatari ya kutoweka ziwe bayana, ziainishwe kwenye kanuni na sheria, kwani hakuna kiongozi au mtaalamu aliyeona umuhimu wa kibali. 

“Tume ililitazama sula hili kwa jicho lingine. Kama mbuzi na ng’ombe wanasafirishwa kwa vibali mikoani kote, iweje faru huyo asafirishwe bila kibali,” alisema.

Alisema kutokana na upungufu wa kiutendaji uliofanywa na ofisi ya Mkurugenzi wa Wanyamapori nchini na Mhifadhi wa NCAA na kuruhusu Faru John kuondolewa bila kibali, Tume inashauri hatua za kiutawala zichukuliwe dhidi ya wahusika.

Manyele alisema migongano ya kimaslahi kati ya watumishi waliolenga kusimamia taratibu na wenye kusimamia maslahi binafsi ni sababu nyingine ya faru huyo kuhamishwa.

“Maslahi binafsi hadi kufikia ngazi ya wizara, ambako wizara iliingilia kati na kupendelea upande wenye maslahi binafsi, hali hiyo ilisababisha kutoelewana kwa makundi hayo mawili, hadi kufikia hatua ya kushitakiana kwa kutumia kauli ya kuuzwa kwa Faru John,” alisema.

Alisema Tume inashauri Serikali iunde tume huru kuchunguza migogoro ya kimaslahi kati ya watumishi wa NCAA dhidi ya uwekezaji ndani ya hifadhi na hatua stahiki zichukuliwe.

Mkemia Mkuu alisema upungufu wa kiuongozi katika kushughulikia masuala ya watumishi ni mwingi hata baada ya mtumishi Lemanya kuwasilisha malalamiko yake kwa uongozi wa NCAA ya kudaiwa kupokea Sh milioni 50 baada ya kumhamishwa faru huyo, malalamiko yake hayakushughulikiwa na uongozi.

“Tume inaunganisha (2) na (3) na kushauri Serikali ifanye tathmini ya kina kuona kama uongozi uliopo sasa NCAA unatosha kuendelea kuongoza taasisi hiyo kwa maslahi mapana ya Taifa.

Aidha, alisema uwepo wa taasisi nyingi zenye mamlaka sawa juu ya masuala ya uhifadhi wa wanyamapori mipaka yao ya kiutendaji inakuwa vigumu kujulikana.  

Alisema Tume inashauri sheria husika zipitiwe upya na kubainisha majukumu mahsusi ya kila taasisi, pia uwezekano wa kujumuisha mamlaka hizo.

Ushauri

Alisema Tume inashauri kufanyika utambuzi wa wakazi halali ndani ya bonde la Ngorongoro na maeneo mengine ya Serengeti na kuzuia uhamiaji katika maeneo hayo.

Pia inashauri kuanzisha na kuimarisha maabara ya utambuzi wa vinasaba vya wanyamapori chini ya GCLA ili kutoa msukumo kwa vyombo vya haki jinai katika kupeleleza na kuchunguza kazi zinazohusu ujangili.

Halikadhalika alisema Tume inaomba Serikali iimarishe vikosi vya kuzuia ujangili kwa kushirikisha na Jeshi la Wananchi, kwa namna inavyoonekana itafaa.

 “Mwingiliano kati ya mifugo na wanyamapori unatoa mwanya kwa majangili kutumia nafasi hiyo kufanya uhalifu.  Tume inashauri pia kuwapo udhibiti na sheria kali ya kuzuia mifugo katika maeneo ya hifadhi,” alisema.

Pia alisema vibali vya uwindaji wanyama wanaoelekea kutowekwa (faru na tembo) vifutwe na sheria ipitiwe upya ili kuzuia vibali hivyo.

Alisema viwanja wa ndege ndani ya hifadhi, vifanyiwe tathmini ya kina juu ya manufaa ya uwepo wao, usimamizi na uendeshaji wao ili kulinda maslahi ya Taifa.

Profesa Manyele alisema Tume inashauri kuanzishwa kwa kanzidata ya vinasaba vya wanyamapori ambayo itasaidia kutambua nyara na kuwezesha vyombo vya uchunguzi na upelelezi kukamilisha kazi zao.

Alisema mahojiano yalishirikisha watendaji 18 ambapo mchakato mzima ulionesha kwa asilimia 100 kuwa Faru John amekufa.

Majaliwa

Akizungumza baada ya kupokea ripoti hiyo, Waziri Mkuu alisema ataipitia ripoti hiyo ili kuilewa na kama kutakuwa na hatua za kuchukua Serikali itafanya hivyo.

Majaliwa alisema walilazimika kuunda tume hiyo kutokana na matukio mbalimbali ya ujangili, hivyo kupitia ripoti hiyo watakuwa na pa kuanzia.

“Nitaipitia ripoti hii kwa umakini kwani kifo cha Faru John kiliibua maswali mengi, naamini utakuwa mwanzo mzuri kwa Serikali kukabiliana na janga hili la ujangili,” alisema.

Aidha, alisema gharama ambazo zimetumika kwa tume hiyo zitabainishwa baadaye, baada ya kila taasisi kuwasilisha gharama iliyotumika kwa watumishi wake.

 Aidha, Tume iliilalamikia Wizara ya Maliasili na Utalii kuvujisha siri za ndani kati ya wizara na taasisi zingine jambo ambalo si sawa.

“Katika kutekeleza jukumu hili zito, Tume ilishuhudia kuvuja kwa siri za mawasiliano kati ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Wizara juu ya vibali na usafirishaji wa sampuli kwenye magazeti,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo