Aliyemlenga Nape bastola akamatwa



 *Mwigulu aweka wazi kuwa si askari Polisi
*Awataka makamanda wawashauri viongozi

Sharifa Marira, Dodoma
Mwigulu Nchemba
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba, amesema mtu aliyemshikia bastola aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amekamatwa na si askari Polisi.

Mwigulu alisema hayo jana kwenye mahojiano na waandishi wa habari baada ya kufungua Mkutano wa Mwaka wa Maofisa Waandamizi wa Polisi na Makamanda wa Mikoa na Vikosi.

"Kama nilivyokuwa nimeagiza uchunguzi ufanyike kumbaini mtu aliyemshikia Nape bastola hadharani ni kwamba si askari Polisi na amekamatwa, hivyo taratibu za kuwajibishwa zitaendelea huko kwenye Mamlaka husika," alisema Mwigulu bila kufafanua ni Mamlaka ipi.

Hata hivyo, Mwigulu aliulizwa kama mtu huyo ni raia wa kawaida au ofisa wa Idara ya Usalama wa Taifa kama inavyoarifiwa na baadhi ya mitandao ya kijamii, lakini alikataa kufafanua suala hilo.

Wiki jana, Nape alinyooshewa bunduki na mtu huyo wakati akishuka kwenye gari lake karibu na hoteli ya Protea, Oysterbay, Dar es Salaam alipokwenda kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu kutumbuliwa kwake.

Awali kwenye mkutano huo, Mwigulu alitaka maaskari kufanya kazi yao kwa weledi na kutenda haki kwani katika ziara alizofanya mikoani kwa nyakati tofauti, alilalamikiwa na wananchi kubambikiwa na kubadilishiwa kesi, jambo ambalo linakiuka misingi ya kazi za kipolisi.

"Kuna malalamiko juu ya askari kubambika na kuwabadilishia watu kesi, hili haliko sawa tuwape watu haki zao, sisi tupo kwa ajili ya wanaoonewa hata Rais wetu anasisitiza kuwa Serikali yake ni ya wanyonge na tufanye kazi kwa haki," alisema Mwigulu.

Alitaka polisi kutotumia taarifa za mahasimu peke yao kuhukumu, kwani kumekuwa na tabia ya kutengenezeana kesi hali inayofanya wakosefu kubaki uraiani na wasio na hatia kufungwa.

Mwigulu pia alisema polisi wataendelea kushirikiana na taasisi zinazohusika na dawa za kulevya ili kupambana na vita hivyo ambavyo vimeanza nchini.

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Balozi Adadi Rajabu, alishauri makamanda wa Polisi wa mikoa kueleza viongozi wao wa mikoa wanapotaka kufanya jambo linalokwenda kinyume na haki na taratibu za nchi wasifanye hivyo.

"Makamanda wa mikoa tumieni nafasi mliyonayo kuonya viongozi wenu wa mikoa, mnapoona wanataka kuanzisha jambo ambalo linakwenda kinyume, msisubiri waharibu ndipo mseme, mkiacha jambo likishatokea ni vigumu kulifuta na kuleta picha mbaya kwa jamii," alisema Adadi.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Ernest Mangu, alisema sifa ya polisi ni nidhamu na kwamba hawatavumilia maaskari watakaokwenda kinyume na maadili.

Alisema katika suala la utendaji, Jeshi hilo litaendelea kuendesha operesheni zikiwamo za kupambana na dawa za kulevya ambapo hadi sasa wameteketeza mashamba kadhaa ya bangi na mirungi, kupambana na ujangili, biashara za magendo kutoka nje na ucheleweshaji na ubambikaji kesi.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo