Serikali yaonya dhidi ya ukatili


Ibrahim Yassin, Mbozi

SERIKALI wilayani hapa, imewataka wananchi kuachana na vitendo vya ukatili kwa kufanya mauaji yanayoipa sifa mbaya wilaya hiyo badala ya kufanya kazi za uzalishajimali
kwa kujiunga kwenye vikundi.

Wilaya hii imekuwa na sifa mbaya kutokana na matukio ya mauaji yanayotokana na imani za kishirikina za kupata mafanikio baada ya ramli za waganga wa kienyeji.

Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, John Palingo, alipozungumza na wanakijiji cha Ipapa kata ya Ipunga alikokwenda kusikiliza kero zao.

Palingo ambaye ni Mkuu wa Wilaya, alisema vitendo vya ukatili na mauaji vimekithiri wilayani hapa hali iliyofanya mkoa wa Songwe kushika nafasi ya pili kwa ukiukaji wa haki za binadamu ikiwa ni pamoja na kupoteza nguvukazi ya Taifa.

Alisema baadhi ya watu wamekuwa wakienda kwa waganga wa kienyeji kupiga ramli chonganishi, huku wakiambiwa wakafanye mauaji na kuchukua baadhi ya viungo kwenye miili yao kwa imani ya kupata utajiri kitu ambacho ni upotoshaji mkubwa.

Aidha, aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi  uhalifu unapotokea ili wahusika wakamatwe kwani bila hivyo, Jeshi haliwezi kujua wahalifu ni akina nani.  

Akijibu kwa niaba ya wenzake, Julius Mwampashe, mkazi wa kijiji hicho kupitia mkutano huo, alisema wako tayari kutoa ushirikiano kwa kamati ya ulinzi uhalifu utakapotokea kwa masharti ya kutowataja.

Mwampashe aliongeza kuwa kumekuwa na ugumu kwa baadhi ya wananchi kutoa ushirikiano hasa kwa Jeshi la Polisi pindi uharifu unapotokea kutokana na kuwataja na kusababisha maisha yao kuwa hatarini.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo