Mradi mkubwa wa umeme wazinduliwa


Suleiman Msuya

MKURUGENZI Mkazi wa Benki ya Dunia (WB) kwa Tanzania, Malawi, Burundi na Somalia, Bella Bird amezindua mradi wa kuzalisha umeme kwenye maporomoko ya Mto Rusumo ambao utatoa megawati 80 kwa nchi tatu Afrika Mashariki.

Bird alizindua chanzo hicho cha umeme jana katika eneo la Rusumo ambapo mawaziri wa sekta hiyo kutoka nchi wanufaika; Rwanda, Burundi na Tanzania walishiriki.

Alisema mradi huo ni moja ya mikubwa katika ukanda huo na anaamini utachochea kuinua uchumi, ajira na maendeleo kwa nchi husika.

Mkurugenzi huyo alisema mradi huo umeonesha umuhimu wa ushirikiano wa nchi husika kwani utagusa maisha ya wananchi moja kwa moja na kukuza uchumi.

“Mfano mradi ukikamilika utasaidia wanawake wanaokutana na ukatili, kuongeza uzalishaji, kuinua shughuli za kilimo na mawasiliano ya aina mbalimbali,” alisema.

Bird alisema Tanzania, Burundi na Rwanda zitakuza familia zao ambapo kila nchi itapata mgao kulingana na hitaji la makazi.

“Burundi watapata megawati 27 hivyo kuongeza asilimia 50 ya hitaji la umeme na itapunguza gharama ya kununua uniti moja kwa senti nne tofauti na za sasa ni senti 10 kwa uniti moja,” alisema.

Alisema Rwanda gharama ya kununua umeme ni senti 26 na Tanzania senti 12 hivyo itakuwa mkombozi katika maeneo husika na kuchochea maendeleo.

Alisema hakuna shaka kuwa uwepo wa umeme ni moja ya vitu ambavyo vinachochea maendeleo, kwani jamii imekuwa ikililia hitaji hilo kila uchwao ili kuendeleza biashara zao.

”Umeme unatengeneza ajira, matumaini, kujiamini na inajulikana kuwa katika kufikia maendeleo chanzo sahihi ni uwepo wa umeme wa uhakika,” alisema.

Alisema hiyo ni moja ya jitihada za ukanda wa Maziwa Makuu kutekeleza mikakati ambayo imewekwa na Umoja wa Mataifa (UN), kupitia aliyekuwa Katibu Mkuu, Ban Ki-moon na Rais wa WB, Dk Jim Yong Kim miaka minne iliyopita ili kuendelea.

Bird alisema katika kipindi hicho, WB ilikubali kutoa dola za Marekani bilioni 1.3 ambapo hadi sasa imetoa dola bilioni 1 za Marekani.

Mkurugenzi mkazi huyo alisema matarajio yao ni kuona mradi huo unakamilika kwa wakati ifikapo 2019 na kwamba wao wamefanya kinachowahusu.

Alisema katika kutekeleza miradi yao pia wanashirikiana na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB) hivyo wanawashukuru kwa ushirikiano wao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo