Majaliwa aonya wakandarasi wabovu


Mwandishi Wetu

Kassim Majaliwa
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali haitavumilia wakandarasi wasio na uwezo na ambao wanapewa kazi lakini wanashindwa kuzimaliza kwa muda uliopangwa.

Atoa kauli hiyo juzi wakati akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Chalinze na wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira (CHALIWASA) katika ofisi zao, karibu na daraja la Mto Wami, Bagamoyo mkoani Pwani.

Alikwenda kukagua mradi wa upanuzi wa mtambo wa maji Chalinze na ujenzi wa mfumo wa kusafirisha na kusambaza majisafi na matangi ya kuhifadhi maji ambao umechukua muda mrefu lakini haujakamilika. Awamu ya kwanza ilianza Septemba mosi 2001 na kukamilika Desemba mosi 2003.

Alimwagiza Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge ahakikishe ujenzi wa mradi huo unafikia asilimia 80 la sivyo, wakamilishe taratibu za kukatisha mkataba na kutafuta mkandarasi mwingine.

Agizo la Waziri Mkuu linatokana na taarifa aliyopewa kwamba mkandarasi wa mradi huo, Overseas Infrastructure Alliance (OIA) Pvt Ltd ya India, alipaswa kumaliza kazi hiyo Februari 22 lakini hadi sasa mradi huo umekamilika kwa asilimia 23 tu.

“Nimeelezwa kwamba mmempa nyongeza ya siku 100 ambayo inakwisha Mei 31, kama kazi yake haitakuwa ya kuridhisha na kufikia angalau asilimia 80, itabidi Waziri uendelee na taratibu zako za kukatisha mkataba, tuanze kutafuta mkandarasi mwingine,” alisema.

“Hii kampuni niliikuta Lindi kwenye mradi mwingine wa maji kama huu. Nilitoa maagizo ya kuharakisha ujenzi ukamilike lakini hawakufanya hivyo hadi Rais alipokwenda na kuagiza mkandarasi anyang’anywe pasipoti yake ya kusafiria mpaka atakapomalizia kazi.

“Kwa kifupi hii kampuni haina uwezo wa kufanya hizi kazi, na ndiyo maana hadi sasa wamekamilisha asilimia 23 tu ya mradi wakati walipaswa kuwa wamemaliza hivi sasa,” alisema Waziri Mkuu na kuongeza:

“Waziri endelea na utaratibu wa kuwaondoa kisheria kwa sababu hata tukiwaongeza muda bado hawatakamilisha kazi.

“Nimesikitika sana kukuta mkandarasi hajafikia malengo. Mtu akipewa kazi anapaswa awe na uwezo wa kifedha wa kuifanya ile kazi ili hata Serikali ikichelewesha malipo yake, yeye aendelee na kazi,” aliongeza Waziri Mkuu.

Akizungumzia kuhusu ufanisi wa mradi huo, Waziri Mkuu alimtaka Mkurugenzi Mtendaji wa CHALIWASA, Christer Mchomba, ahakikishe anapeleka maji hadi majumbani mwa wateja na kuweka mita ili wananchi walipe bili zao badala kuishia kutoa huduma hiyo kwenye vibanda.

 “Kazi ya kupeleka maji majumbani ni yenu CHALIWASA na si ya Wizara. Pelekeni maji na mfunge mita ili watumiaji waweze kulipa bili zao. Pia toeni elimu kwa wananchi kupitia mikutano ya hadhara, waelezeni mipango yenu na wapi mlipofika. Kazi yenu si kutandika mabomba tu, bali kutekeleza majukumu mliyopewa kwa niaba ya Serikali,” alisema.

Kuhusu mitambo inayotumika, Waziri Mkuu alisema mashine zilizopo ni za siku nyingi tangu mwaka 2003; hivyo alimwagiza Waziri Lwenge afuatilie upatikanaji mashine za kisasa kwani hilo suala ni kubwa na haliwezi kubebwa na CHALIWASA.

“Bora mngeanza kuagiza mashine mpya hivi sasa, badala ya kusubiri zichakae kabisa, ndipo muanze kufikiria kuagiza,” alisema.

Mapema, akitoa taarifa ya mradi huo, Mchomba alisema awamu ya tatu ya ujenzi wa mradi huo ilisainiwa Mei 18 mwaka juzi kati ya DAWASA na OIA yenye ubia na kampuni ya Pratibha Industries kutoka India kwa dola milioni 41.36 ambazo ni fedha za mkopo nafuu kutoka benki ya Exim ya India.

“Kazi zilizopangwa kufanyika ni upanuzi wa mtambo wa maji ili kuongeza uzalishaji kutoka mita za ujazo 500 hadi 900 kwa siku; ujenzi wa mfumo wa mabomba ya kusambaza maji wenye kilometa 1,022; ujenzi wa matangi makubwa 19 ya kuhifadhia maji; vituo tisa vya kusukumia maji na vibanda 351 vya kuchotea maji,” alisema.

 Alisema hadi sasa mkandarasi huyo ameshalipwa dola milioni 15.81 sawa na asilimia 38 na anaendelea na utandazaji mabomba ambapo hadi sasa ameshatandaza mabomba yenye urefu wa kilometa 141 sawa na asilimia 12.4.

Alisema mradi huo umelenga kunufaisha vijiji 68 ambavyo 19 viko Kaskazini mwa Mto Wami na 49 Kusini.

Akizungumzia utendaji kazi wa mkandarasi huyo, Mchomba alisema Serikali imechukua hatua za kimkataba kwa kumtoza gharama ya kuchelewa kumaliza mradi kuanzia Februari 23.

“Pia mkandarasi amepewa notisi ya siku 100 kumtaka aongeze kasi ya kazi, vinginevyo tutasitisha mkataba ifikapo Mei 31 kulingana na kipengele namba 8.7 cha mkataba,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo