JPM aonya wamiliki wa vyombo vya habari


Charles James

Dk John Magufuli
WAMILIKI wa vyombo vya habari nchini wametakiwa kuwa makini na habari zinazochapishwa kwenye vyombo vyao na wasidhani kuwa uhuru walionao hauna mipaka.

Onyo hili lilitolewa jana na Rais John Magufuli wakati akiapisha mawaziri wawili aliowateua juzi Alhamisi; Dk Harrison Mwakyembe aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Profesa Palamagamba Kabudi aliyeteuliwa kuwa Waziri wa Sheria na Katiba.

Uteuzi wa mawaziri hao ulifanywa na Rais katika mabadiliko madogo kwenye Baraza la Mawaziri ambapo Dk Mwakyembe alihamishiwa Wizara ya Habari akitoka Sheria baada ya Nape Nnauye kutenguliwa huku Profesa Kabudi ambaye ni Mbunge wa Kuteuliwa akichukua nafasi ya Dk Mwakyembe.

Akizungumza baada ya kuwaapisha mawaziri hao sambamba na mabalozi wawili, Rais Magufuli aliwataka waandishi wa habari na wamiliki wa vyombo hivyo kuwa makini na kuepuka kuandika habari za uchochezi ambazo zinaweza kuiingiza nchi pabaya.

“Waandishi kuweni waangalifu na kalamu zenu kwa sababu siku Tanzania ikiingia kwenye machafuko na nyie mtakua sehemu ya watu waliochangia kutokea kwa machafuko, angalieni nchi zote ambazo zilifikia pabaya chanzo kilikuwa ni kalamu zetu, hata Rwanda mauaji ya kimbari yalichangiwa kwa kiasi kikubwa na waandishi wav habari,” alionya.

“Hata mkiangalia magazeti yote ya leo (jana) yamejaza picha ya mtu aliyefanya kosa moja tu na hata kurasa za ndani zimejaza habari hiyo hiyo, kwani hakuna habari zingine za kuandika? Sasa Dk Mwakyembe nenda kasimamie kwa umakini tasnia ya habari na kuchapa kazi, Serikali iko na wewe na siko tayari kuona nchi ikichezewa,” alisema Rais Magufuli.

Alionya wamiliki kwa kuzipa uzito habari mbaya huku akitolea mfano wa chombo kimoja cha televisheni kwamba kimekuwa kikirusha habari ya maandamano ya wakulima au wafugaji kwa kuzipa kipaumbele na muda mrefu.

“Nawaambia wamiliki wa vyombo vya habari kuweni makini na angalieni, kama mlifikiri mna uhuru wa namna hiyo si kwa ukubwa huo, si kwa utawala wangu, Mwakyembe nenda kapige kazi Serikali iko imara na kama kuna watu walishindwa kuchukua hatua wewe nenda kachukue.

“Kuna vyombo vya habari vimetangaza kutoandika habari za mtu fulani, wakati huo huo wanaandika mbaya tu, kama hamtaki kumwandika si msiandike kabisa? Acheni kuandika yote mazuri na mabaya,” alisema Rais Magufuli akimaanisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda aliyesusiwa na vyombo vya habari.

Akizungumza baada ya kuapishwa, Dk Mwakyembe alimshukuru Rais kwa kumwamini na kumpa wadhifa huo na kuahidi kuitumikia nafasi hiyo kwa uaminifu mkubwa. Profesa Kabudi alisema shukrani za kipekee anazipeleka kwa Mwenyezi Mungu kwa kumwezesha Rais kumpa nafasi hiyo kubwa na kuahidi kuifanya kwa nguvu kubwa na uaminifu.

“Jana (juzi) na usiku ulikuwa mgumu sana kwangu, nimerudia kuisoma Zaburi ya 15, inasema, ‘Nani ee Mwenyezi Mungu atakayekaa hemani mwako? Nani atakaeishi juu ya mlima wako mtakatifu?’ Huku nikimwita Mungu anisaidie mimi na wewe.

“Siwezi kuzungumza chochote kabla ya kuonana na wewe na uongozi wa juu wa Serikali, kwani mkamia maji hayanywi, nami sitaki kuyakamia, niseme tu ahsante Rais na ninakuahidi utumishi wa nguvu zangu zote,” aliahidi Profesa Kabudi.

Katika hafla hiyo pia Rais Magufuli alimwapisha Dk Abdallah Possi kuwa Balozi nchini Ujerumani, George Masima aliyepangiwa Israel na Sylvester Mabumba kuwa balozi wa visiwa vya Comoro na Stella Mgasha kuwa Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo