Nape aahidi kumuunga mkono Mwakyembe

Suleiman Msuya

Nape Nnauye
ALIYEKUWA Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, ameahidi kumwunga mkono Waziri mpya Dk Harrison Mwakyembe na kuendeleza uaminifu wake kwa Rais John Magufuli.

Nape alitoa kauli hiyo jana Dodoma wakati akikabidhi ofisi kwa Dk Mwakyembe ikiwa ni utaratibu wa kawaida wa Serikali yanapotokea mabadiliko.

“Tofauti na maneno ya mitandaoni, nitabaki kuwa mtiifu kwa Rais, Serikali na CCM,” alisema Nape.

Nape aliondolewa kwenye wadhifa huo wiki iliyopita baada ya kuongoza wizara hiyo kwa takriban miezi 15, alimshukuru Rais Magufuli kwa kumwamini na kumpa dhamana kubwa ya kusimamia wizara kwa kipindi hicho, huku akiwa mbunge kwa mara ya kwanza.

Aidha, aliahidi kuendelea kushirikiana na wizara kwa ukaribu akikiri kuwa yeye ni mdau mkubwa wa sekta za wizara hiyo.

Heshima aliyonipa Rais ni kubwa mno na nitaendelea kumwunga mkono katika dhamira yake njema ya kuleta mageuzi nchini,” alisema.

Alishukuru watendaji wote wa wizara kwa kumpa ushirikiano wa kutosha kwa kipindi chote alichofanya nao kazi na kuwaomba kutoa ushirikiano huo huo kwa  Dk Mwakyembe.

Waziri Mwakyembe aliahidi kushirikiana na Nape kwa kuwa ni mdau mkubwa katika sekta hiyo.

Aidha, Mwakyembe aliahidi kuendeleza mazuri yaliyoanzishwa na Nape katika kuimarisha ufanisi wa wizara hiyo na kuhakikisha inakuwa moja ya wizara za mifano nchini.

Alisema Nape amefanya kazi kubwa ya kuitangaza wizara hiyo hivyo matarajio yake ni kuona jitihada hizo zinaendelezwa kwa kasi zaidi.

“Naahidi kushirikiana na aliyekuwa waziri, kwani mchango wake ni mkubwa sana hivyo yale mazuri lazima twende nayo kwa kasi ile ile,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo