Heri kusaidia wenye ulemavu kuliko ‘mateja’


Joseph Kulangwa

Joseph Kulangwa
TANZANIA kama zilivyo nchi zingine duniani, imekuwa ikipigana vita dhidi ya dawa za kulevya ambazo kwa kiasi kikubwa zimekuwa zikiathiri vijana na hivyo nguvukazi ya nchi.

Matumizi na biashara ya dawa hizo ni tatizo lililokithiri maeneo mengi duniani na nchi kadhaa zimekuwa zikitumia gharama kubwa kwa mapambano hayo, kwa mihadarati ambayo mbali na kufifisha nguvu za vijana, imekuwa ikikatiza maisha yao.

Athari za matumizi ya dawa hizo ni kubwa na dhahiri, kwani husababisha watumiaji kuharibikiwa akili na miili na hivyo kukaa bila kujishughulisha na hata kufanya kazi za kuingiza kipato.

Kuharibikiwa huko kumekuwa kukiwakuta watumiaji ambao wakati mwingine huwa na kazi nzuri lakini baadaye kujikuta wakizitelekeza na kuingia katika maisha mapya ya mashaka na hatari zaidi.

Lakini wafanyabiashara ya dawa hizo wamekuwa wakijinufaisha kwa kujipatia kipato kikubwa na kumiliki mali kubwa kubwa na za kifahari, huku watumiaji ambao mara zote ni wadogo na masikini, wakibaki na umasikini wao na hata pengine kupokwa maisha.

Kwa kuwa vita dhidi ya dawa za kulevya ni ngumu na ya hatari, ndiyo sababu nchi nyingi hutumia pia gharama kubwa kupambana huku mataifa kama Mexico, viongozi wakitumia hata mitutu ya bunduki kukabiliana na wafanyabiashara na watumiaji hao.

Tanzania haijaanza leo kupambana na dawa za kulevya, ingawa mwaka huu vita hivyo vimeonekana kujitokeza waziwazi hasa kutokana na njia inayotumika kupambana kwa kutangaza watuhumiwa hadharani na hata wakati mwingine bila ushahidi wa kutosha.

Kama kuna mtu anapinga vita dhidi ya dawa za kulevya ni dhahiri haitakii mema nchi hii na watu wake; hivyo kuna haja ya makusudi ya kuunganisha nguvu Wataznania wote kukabiliana na dawa hizo na kuzitokomeza ili kubaki na raia wema.

Lakini hata hivyo, kutokana na maendeleo duniani, kila vita vinahitaji sayansi, kwa maana ya kutafiti, kujiridhisha, kuthibitisha na kuchukua hatua, badala ya kukurupuka bila utaratibu na hivyo kukosa ushahidi na uhakika wa mapambano na kuishia kulalamikiwa.

Tanzania ni moja ya nchi ambazo hivi sasa zinatajwa duniani kuwa si tu vituo, bali hata njia za kupitishia dawa hizo na matokeo yake vijana wake wengi wamejikuta kwenye uraibu na kuitwa ‘mateja’.

Ili kukabiliana na uraibu huo, baadhi ya watu waliopata kutumia dawa hizo na kuacha, wameanzisha vituo vya kurekebisha tabia za watumiaji na kuondoa uraibu, huku Serikali nayo ikisisitiza matumizi ya dawa za methadone kwa ‘mateja’.

Serikali hivi sasa ina mipango pia, ya kuhakikisha kwamba inawakusanya ‘mateja’ hao na kuwatafutia maeneo ya kufanya uzalishaji mali ili kwamba waachane na matumizi ya dawa hizo hatari.

Pamoja na kuanzishwa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda akizungumza na ‘mateja’ na wadau wa kupambana na mihadarati Dar es Salaam, aliahidi kuwatafutia maeneo ya kuzalishia mali.

Bila shaka hilo ni wazi zuri, lakini linahitaji nguvu kubwa kuhakikisha na kuthibitisha kwamba ‘mateja’ hao kweli wameachana na matumizi ya mihadarati na kurudi kwenye hali inayoruhusu uzalishaji mali, ikiwa ni pamoja na ufundi kwa walio na ujuzi.

Kwa kuwa haina uthibitisho wa asilimia 100 kuwa watumiaji walioacha huacha moja kwa moja kwa kuwa wengine hurudia kama ilivyopata kutokea kwa Rehema Chalamila ‘Ray C’ na wengine, itakuwa nguvu kwa watu hao kuaminiwa haraka katika maeneo yao ya ufundi.

Pamoja na nia njema ya Serikali kutaka kuwasaidia ‘mateja’ hao ambao bila shaka kwa kiasi kikubwa ‘hujitakia’ kuwa na hali hizo, mimi nadhani mwelekeo ungelenga zaidi watu wenye ulemavu mitaani walio na elimu lakini hawana cha kufanya.

Sina nia mbaya na ‘mateja’, lakini kinachofanyika ni kuwalea na kufundisha wengine kwamba kumbe kutumia mihadarati na kasha kutangaza kuacha, ni njia ya Serikali kumtafutia ‘teja’ eneo la baishara au uzalishaji mali. Kwa imani hiyo, itakuwa kazi kubwa, ngumu na ya muda mrefu, kukabiliana na matumizi ya dawa hizo.

Litakuwa jambo la kushangaza sana, kwamba wakati wenye ulemavu wengi tena wenye ujuzi na sifa za kuajiriwa au hata kukopeshwa, wamekuwa wakinyanyapaliwa na kuachwa wakitaabika, huku ‘mateja’ wakipewa kipaumbele.

Rais John Magufuli bila shaka kwa kutambua umuhimu lakini pia usawa wa kibinadamu kwa watu wenye ulemavu, katika uongozi wake aliamua kuwapa nafasi katika ngazi za juu zikiwamo za naibu uwaziri na ukatibu mkuu. 

Bila shaka alibaini kwamba mchango wao ni mkubwa, kwa kuamini kuwa ulemavu wa viungo si wa akili, lakini mateja ‘walioguswa’ akili hatuwezi katu kuwalinganisha na wenye ulemavu wa viungo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo