Taasisi ya Kikwete yaweka historia upasuaji


Salha Mohamed

TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imefanya upasuaji wa kihistoria kwa wagonjwa kuwekwa mishipa sita ya damu iliyoziba kwenye moyo baada ya kuivuna kutoka miguuni.

Upasuaji huo ulifanyika kwa kushirikiana na madaktari kutoka hospitali ya Saifee nchini India ikiwa ni ahadi ya kiongozi wa Mabohora kwa Rais John Magufuli.

Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Magojwa ya Moyo na Mishipa ya Damu JKCI, Dk Bashir Nyangasa alisema upasuaji huo umeokoa Sh milioni 400 endapo wangesafirishwa nje ya nchi.

Alisema wamefanya upasuaji kwa wagonjwa 20 ambapo kati yao 12 walifanyiwa upasuaji bila kufungua vifua, ambapo walizibua mishipa ya damu iliyokuwa imeziba huku mmoja ukiwa uliziba kwa asilimia 100.

"Tumefanyia wagonjwa wanne kwa kuvuna mishipa kwenye miguu na kuipandikiza kwenye moyo, namshukuru Mungu katika uhusiano na watu wa nje kila wanavyokuja hufanya lililo bora zaidi," alisema.

Alisema kambi zilizopita walikuwa wanavuna mishipa ya damu miguuni na kuiweka kwenye moyo kwa mishipa miwili au mitatu, lakini kwa ushirikiano huo walifanyia mishipa sita.

"Mishipa sita ni historia kufanyika nchini, mishipa hiyo iliyowekwa mgonjwa, kuunganisha kila mshipa huchukua dakika sita hadi nane lakini hawa walifanya kwa dakika nne hadi tano," alisema.

Alisema walitanua milango ya moyo ambayo ilikuwa haipitishi damu vema, walibaini pia matatizo katika mishipa ya damu ya moyo na kuweka betri kwa mgonjwa.

Alifafanua: “Kuna wagonjwa wawili ambao matundu yao ya moyo yalikuwa yameziba na walipewa matibabu na wanaendelea vizuri pamoja na mtoto wa miaka minane ambaye valvu yake ya moyo ilikuwa imesinyaa”.

Mkurugezi wa Tiba ya Moyo, Dk Peter Kisenga alisema kupitia ushirikiano huo, walijifunza mambo mbalimbali kutoka kwa madaktari hao wa India katika upasuaji, hasa bila kufungua vifua na kuzibua mishipa iliyoziba kabisa.

Aidha, miongoni mwa madaktari kutoka hospitali ya Saifee, Yunus Loya alishukuru kwa mapokezi mazuri waliyopata na walibadilishana uzoefu wa kufanya upasuaji.

Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabohora nchini, Zainuddin Adamjee alisema wataendelea kushirikiana na Tanzania kutoa huduma za kijamii na kwamba Februari walileta madaktari wengine kufanya kazi Arusha.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo