Gwajima kuliombea Taifa kwa siku tatu


Abraham Ntambara

Askofu Josephat Gwajima
ASKOFU wa Kanisa la Ufufuo na Uzima Josephat Gwajima amewataka waumini wake kutomjadili Rais John Magufuli kwani ni mamlaka kutoka kwa Mungu na kuwa anaamini kiongozi huyo ameshazipata taarifa za kuhusu mtu aliyemtaja kwa jina la Daud Albert Bashite.

Aidha, Gwajima amesema amechoka kuzungumza na wanadamu kuhusu suala hilo na kueleza kuwa sasa anamkabidhi Mungu ili achukue hatua ambapo yeye atafanya ibada ya kufunga na kuomba kwa siku tatu kuanzia Machi 29 hadi 31 mwaka huu.

Alisema katika maombi hayo pia atawaombea Rais, Waziri Mkuu, Makamu wa Rais, Baraza la Mawaziri, Jaji Mkuu, Spika wa Bunge na Wabunge ili Mungu ashughulike nao.

Askofu Gwajima alisema hayo Dar es Salaam jana, wakati wa mahubiri yake kanisani kwake Ubungo, ambapo aliwataka waumini wake kila mmoja kumwendea Mungu kwa kufunga, kuomba na kusema kuwa maombi hayo watajibiwa.

“Nawaambia tena, kila mtu na asikie, sauti yangu inanyamaza, kwa habari ya kuongea na wanadamu kuanzia Jumatano, koo langu na sauti yangu,inemwelekea Bwana wa Majeshi aliyeumba Tanzania na vyote vilivyomo,” alisema Gwajima.

Alieleza kuwa hakuna sababu ya kulia kana kwamba hakuna Mungu akiwataka wasiogope kwani yupo Simba wa Yuda aliyeshinda ili pate kuifungua siri hiyo.

Aliwataka Watanzanua kutoililia mamlaka ya Rais kwa kuwa ndiyo yanayolilinda Taifa na kulifanya litulie.

“Rais anaweza akawa sawa au asiwe sawa, lakini hilo  haiwahusu ninyi bali mumwachie Mungu,” alisema Gwajima.

Alifafanua kwamba mamlaka ya Rais ni sawa na mamlaka ya Mchungaji Kiongozi kama yeye ambapo alisema kuwa kama hayupo na akawa amaharibikiwa, kanisa pia litakuwa limeharibikiwa.

Aliwataka kuachana na Rais na kuwataka kumwendea Rais wa Mbinguni ambaye ni Yesu Kristo ambaye watamweleza haja zao, akifafanua kuwa Rais Magufuli alisema amekwisha sikia hivyo waachane naye.

Askofu Gwajima alisema ni mwiko kanisani kwake kusikia mtu akimsema Rais vibaya ambapo aliwataka kukaa kimya kuhusu habari zake kwa kuwa amekwisha sikia na kwamba ni mwenye hekima, akili na amewekwa na Mungu.

Alisema wamheshimu na kumsaidia kwa nguvu zote Rais, lakini kuhusu mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam wasimsaidie na kusema kwamba hatakubali hilo hadi haki itendeke kwani anataka kuona Tanzania yenye usawa kwa kila Mtanzania.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo